Wednesday, November 2, 2016

WADAU WA UJENZI WAKAGUA UWANJA WA KIMATAIFA WA MWL. JULIUS NYERERE (TB III)

Mwenyekiti wa Ujumbe maalum wa wadau wa Ujenzi, Bi. Elizabeth Tagora (wa kwanza kulia), akijadiliana jambo na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), Eng. Patrick Mfugale (wa kwanza kushoto), wakati ujumbe huo ulipokagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la tatu la Abiria (Terminal III) katika Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Mwl. Julius Nyerere (JNIA). 
Mkurugenzi wa Mradi wa ujenzi wa Jengo la Tatu la Abiria (TB III), Eng. Mohamedi Milanga akifafanua jambo kwa ujumbe maalum wa wadau wa ujenzi walipokagua hatua za ujenzi wa jengo hilo. 
Mkurugenzi wa Mradi wa ujenzi wa Jengo la Tatu la Abiria (TB III), Eng. Mohamedi Milanga akionesha wajumbe maalum wa wadau wa ujenzi eneo la kupumzikia abiria katika Jengo la Tatu la Abiria (TB III) waliokagua hatua za ujenzi wa jengo hilo. 
Muendelezo wa jengo la tatu la abiria sehemu ya pili katika hatua za ujenzi. Jengo hilo litakapokamilika litakuwa na uwezo wa kuhudumia abiria 2,800 kwa wakati mmoja. 
Muonekano wa eneo zitakapokuwepo huduma za kibenki na Idara ya Uhamiaji katika Jengo la tatu la Abiria (TB III). 
Muonekano wa sehemu ya mbele ya wa Jengo la Tatu la Abiria (TB III) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Julius Nyerere (JNIA). Jengo hilo linatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka ujao. 
Muonekano wa juu wa Jengo la Tatu la Abiria (TB III) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Julius Nyerere (JNIA).

MAGAZETI YA LEO JUMATANO,NOV 02


Tuesday, November 1, 2016

KUTOKA BUNGENI MJINI DODOMA LEO

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, Jenista Mhagama akizungumza bungeni mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Mbunge wa Tarime, Ester Matiko bungeni mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Naibu Spika, Dkt. Tulia Ackson akizungumza na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, bungeni mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa Kawe, Halima Mdee kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa Singida Kaskazini , Lazaro Nyalandu kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma Novemba 1, 2016.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na wabunge wanawake kutoka bunge la Zimbabwe kwenye jengo la utawala la Bunge mjini Dodoma Novemba 1, 2016.Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu

Sababu tano za kuunga mkono Muswada wa Huduma za Habari 2016


Fatma Salum- MAELEZO

Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari wa mwaka 2016 ambao unatazamiwa kuwasilishwa kwa mara ya kwanza bungeni katika kikao kilichoanza Novemba 1 mwaka huu umezua mjadala mkubwa na mpana miongoni mwa wadau wa sekta ya habari.

Mjadala wa muswada huu umekuwa ni mkubwa ukilinganisha na miswada mingine kwa sababu ukweli ni kwamba kila mtanzania ni mdau wa sekta hii ambayo wote tunaitegemea kwa kupata taarifa zinazoaminika ili kutusaidia kufanya maamuzi mbalimbali katika maisha yetu ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Usahihi wa maamuzi yote makubwa tunayoyafanya mmoja mmoja au kwa pamoja kama jamii – iwe kuchagua vongozi, kuchagua kozi ya kusoma na mengineyo yanategemea sana taarifa tulizonazo.

Ili tuweze kupata taarifa sahihi ni muhimu vyombo vya habari na waandishi watengenezewe mazingira mazuri ya kufanyia kazi, jambo ambalo ndiyo malengo ya sheria hii tarajiwa.

Licha ya ukosoaji mkubwa unaofanyika, ukweli ni kwamba Muswada wa Vyombo vya Habari 2016, kama utapitishwa, utajenga mazingira mazuri ya tasnia hii na kuirudishia heshima inayostahili.

Katika kupitia muswada huu nimeona faida nyingi za muswada, lakini kwenye makala hii nitataja faida tano kubwa.

Heshima ya tasnia

Kwanza, muswada huu unairejeshea tasnia hii heshima yake iliyoipoteza siku nyingi kwa kuifanya fani hii iwe miongoni mwa fani za uweledi, kama zilivyo nyingine zikiwemo udaktari na uanasheria.

Heshima ya tasnia hii inastahili kuwa juu na ndiyo maana vyombo vya habari vimeitwa mhimili wa nne, ukifanya kazi sambamba na mihimili mingine yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

Tasnia hii ilianza kupoteza heshima kuanzia miaka ya 1990 kufuatia mabadiliko ya kiuchumi, kijamii na baadae kisiasa (vyama vingi 1992) yaliyochochea kuibuka kwa vyombo vingi vya binafsi, hususan magazeti.

Tangu enzi hizo, changamoto kubwa ya fani hii imekuwa ni ukosefu wa udhibiti kiasi kwamba kila anayejisikia, bila kujali kasoma au la, anaingia. Matokeo yake waandishi wasiosoma (makanjanja) wamekuwa wakifanya madudu na lawama zimeelekezwa kwa wanahabari wote. Akioza samaki mmoja ndiyo wote.

Kwa sasa waandishi wanatazamwa kwa kejeli, wanatukanwa, wanabezwa na yote haya ni kwa sababu ya kundi la waandishi wasio na maadili na ambao hawana ukomo wala miiko katika kutafuta habari na wanachokiandika ni tofauti na walivyopokea kutoka katika chanzo chao cha habari.

Mara nyingi tunasikia mwandishi anavamia stara za watu katika majumba yao au katika maeneo yao ya starehe kwa jina la kutafuta habari. Kwa hali hii, ni vigumu kulaumu vyanzo (source) wanapokataa kuzungumza na vyombo vya habari. Yote haya ni kwa sababu ya waandishi waliokosa taaluma na weledi (makanjanja).

Uholela wa kuingia katika fani hii ulitokana na sababu mbili kubwa, kwanza kisingizio cha kipengele cha katiba kinachomhakikishia kila mtu haki ya kukusanya na kusambaza habari (Ibara ya 18.1) kwani baadhi ya watu wametafsiri kipengele hiki kuwa kila mtu anaweza kuwa mwandishi wa habari!

Sababu ya pili ni maendeleo makubwa ya teknolojia ambapo kila aliyeweza kujitengenezea blogu yake alifanya hivyo na kuanza kutafuta na kuchapisha habari.

Lakini ukweli ni kwamba tasnia hii si ya mchezo mchezo na kufanyia majaribio. Zipo nchi zilizosambaratika au kuingia katika vurugu kutokana na vyombo vya habari ambavyo havikuwajibika, vikashindwa kutanguliza uzalendo, weledi na kuzingatia maadili.

Muswada huu katika sehemu ya tatu, Ibara ya 10, unaondoa shida hiyo kwa kuweka Bodi ya Ithibati ya Wanahabari itakayowajibika kutoa vitambulisho (press card) kwa wanahabari kwa kuzingatia sifa na viwango vya elimu vinavyotakiwa. Bodi pia itasimamia kanuni za maadili ya wanahabari zilizoidhinishwa na kutunza orodha ya waandishi waliothibitishwa.

Ibara ya 18.1–2 inapiga marufuku wasio na vitambulisho (press card) kufanya kazi ya uandishi wa habari na ibara ya 47.2 inaweka adhabu ya faini isiyopungua Milioni 5 au kifungo cha hadi miaka mitano kwa wanaovamia tasnia ya habari na kutumia huduma ya habari kueneza habari za uongo kwa lengo la kuhatarisha ulinzi, amani na usalama wa nchi. Bila ya shaka sheria hii ikitekelezwa, heshima ya tasnia ya habari itarejea.

Msisitizo wa elimu

Ukiangalia hali halisi ya uandishi wa sasa, utagundua kuwa kiini cha tatizo ni watu kupita njia za mkato kuingia katika fani hii, yaani kutokuwa tayari kwenda shule kusoma.

Lakini hata wale waliosoma bado wanahitaji kuendelea kupigwa msasa juu ya namna bora ya kufanya kazi zao maana tasnia ya habari inabadilika kila uchao hususan upande wa teknolojia.

Miaka 20 iliyopita hatukuwa na blogu wala hakukuwa na Twitter, Facebook, Instagram na Whatsapp kama ilivyo sasa, lakini hizi ni silaha za mwandishi na anaweza kuzitumia kuboresha kazi zake.

Ukiangalia muswada huu utaona kuwa umeweka msisitizo mkubwa katika elimu ya waandishi wa habari kiasi kwamba bodi itakayoundwa ina jukumu la kuishauri serikali kuhusiana na mafunzo ya waandishi, kushauriana na taasisi za elimu ya mambo ya habari juu ya viwango vya elimu vinavyotakiwa kwa waandishi na muhimu zaidi bodi hii ina jukumu la kuandaa mafunzo ya waandishi wa habari.

Katika Ibara ya 21, muswada huu unazungumzia mfuko wa mafunzo ya habari wenye malengo matatu ikiwemo kuwezesha mafunzo kwa wanataaluma ya habari, kukuza program za uendelezaji wa maudhui ya ndani ya nchi na pia kuchochea na kuchangia utafiti na maendeleo katika nyanja za habari na mawasiliano ya umma.

Kwa mujibu wa Ibara ya 22, mfuko huo utapata fedha kutoka bungeni, misaada na zawadi na michango ya vyombo vya habari. Kwa hiyo ukisoma vifungu hivi unaona kuna faida nyingi ambazo iwapo muswada huu utapita na kutekelezwa ipasavyo, utasaidia kuhuisha tasnia ya habari.


Umuhimu wa Baraza Huru la Habari
Pia muswada huu umeainisha kuwa kutakuwa na Baraza Huru la Habari ambalo kazi na mamlaka yake yatatambulika kisheria. Kila mwanahabari aliyethibitishwa atakuwa mwanachama wa baraza hili.

Ibara ya 25 (1) inaeleza kazi za baraza hili kwa kushirikiana na Bodi ya Ithibati zitakuwa ni kuandaa na kuidhinisha kanuni za maadili ya taaluma ya habari pamoja na kukuza maadili na viwango vya taaluma baina ya wanahabari na kampuni za habari.

Uwepo wa baraza hili utapelekea tasnia ya habari kuwa taaluma rasmi inayotambulika kisheria kama taaluma nyingine, tofauti na baraza lililopo sasa ambalo halitambuliki kisheria hivyo mamlaka yake hayana nguvu.

Kulinda Maslahi ya Waandishi wa Habari
Sababu nyingine ya kuunga mkono muswada huu ni maslahi ya moja kwa moja kwa wanahabari. Sheria hii itasaidia sana kulinda maslahi ya waandishi wa habari pale wanapopata majanga wakiwa kazini, maradhi, kustaafu au kuachishwa kazi. 

Kila mwajiri atatakiwa kuweka bima na hifadhi ya jamii kwa kila mtu aliyeajiriwa katika chombo cha habari husika na wanahabari wa kujitegemea watapaswa kujiwekea kinga kwa mujibu wa sheria hii.
Jambo hili ni la kupongeza sana kwani sheria hii itasaidia kuboresha maslahi ya wafanyakazi kwenye tasnia ya habari.

Wengi wetu ni mashahidi kwamba kuna baadhi ya waandishi wa habari wamewahi kupata matatizo wakiwa kazini lakini wameishia kusubiri kuchangiwa na wasamaria wema ili wapate matibabu kwa vile hakuna kinga ya kuwabana waajiri au vyombo vya habari viweze kuwasaidia.
Mwelekeo kwa Vyombo vya Habari.


Sababu ya tano ya kuafiki muswada huu ni kwamba, pamoja na mambo yote sheria hii inatoa mwelekeo wa vyombo vya habari kuhusu jinsi ya kufanya kazi kwa ufanisi, kuzingatia maadili na weledi. Katika hili, sheria imeeleza majukumu ya vyombo vya habari vya umma na binafsi ili kuhakikisha majukumu hayo yanaleta tija kwa taifa.

Kwa kuzingatia hayo muswada huu una manufaa makubwa sio tu kwa wanahabari bali watu wote watanufaika kwa kupata taarifa sahihi zenye maudhui ya kuelimisha, kukosoa, kuonya na kuboresha bila ya kuudhi, kukiuka haki za wengine au kuharibu amani na usalama wa taifa letu.

RAIS DKT. MAGUFULI AFUNGUA BARABARA YA NAIROBI SOUTHERN BYPASS KATIKA ENEO LA KAREN NCHINI KENYA



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na mwenyeji wake Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta mara baada ya kuwasili katika eneo ka Karen jijini Nairobi kwa ajili ya kufungua rasmi barabara ya kupunguza msongamano ya Nairobi Southern Bypass nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na mwenyeji wake Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta wakati wa nyimbo za Taifa zikipigwa mara baada ya kuwasili katika eneo la Karen jijini Nairobi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na mwenyeji wake Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, Naibu Rais wa Kenya William Rutto pamoja na viongozi wengine, wakikata utepe kuashiria ufunguzi wa barabara ya kupunguza msongamano ya Nairobi Southern Bypass nchini Kenya.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa Karen nchini Kenya mara baada ya kufungua barabara ya Nairobi Southern Bypass nchini Kenya.




Sehemu ya barabara hiyo ya Nairobi Southern Bypass nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na mwenyeji wake Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta wakicheza wimbo pamoja na kikundi cha kwaya katika eneo la Karen mara baada ya kufungua barabara hiyo ya Nairobi Southern Bypass nchini Kenya.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akipata maelezo kutoka kwa Bi. Lucy Karuga kuhusu usindikaji wa mazao ya chakula katika kiwanda cha Maziwa cha Eldoville katika eneo la Karen nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia usindikaji wa Samli katika kiwanda hicho cha maziwa cha Eldoville nchini Kenya.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Mama Ngina Kenyatta mama mzazi wa Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta wakati alipomtembelea nyumbani kwake Nairobi nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akijadiliana jambo na Mama Ngina Kenyatta mama mzazi wa Rais Uhuru Kenyatta pamoja na Rais Uhuru Kenyatta wakati alipomtembelea mama huyo nyumbani kwake Nairobi nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimshukuru Mama Ngina Kenyatta mama mzazi wa Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta wakati alipomtembelea nyumbani kwake Nairobi nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimshukuru Mama Ngina Kenyatta mama mzazi wa Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta wakati alipomtembelea nyumbani kwake Nairobi nchini Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta pamoja na Mama yake Rais Uhuru Kenyatta Mama Ngina Kenyatta jijini Nairobi nchini Kenya. PICHA NA IKULU

RC PWANI AWATAKA WAJASIRIAMALI NCHINI KUWA WABUNIFU ILI KUWEZA KUSHINDANA KATIKA SOKA AFRIKA MASHARIKI

Mkuu wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo akiwahutubia wajasiriamali hawapo pichani wakati wa sherehe za ufungaji wa maonyesho ya tisa kanda ya mashariki yaliyofanyika katika viwanja vya mwanakalenge Wilayani Bagamoyo.(PICHA NA VICTOR MASANGU)
mmoja wa wajasiriamali walioshiriki katika maonyesho ya tisa ya kanda ya mashariki yaliyofanyika katika viwanja vya mwanakalenge Wilayani Bgamoyo Jacob Luis akiwa katika gari yake ambayo ameitengeneza yeye mwenyewe ambapo mpaka kukamilika kwake ametumia gharama ya kiasi cha shilingi milioni tisa(PICHA ZOTE NA VICTOR MASANGU)

NA VICTOR MASANGU, BAGAMOYO 

WAJASIRIAMALI nchini wametakiwa kuhakikisha wanakuwa wabunifu na kutengeneza bidhaa zenye ubora wa kiwango cha juu ili kuweza kuleta ushindani na kuzipeleka katika soko la afrika mashariki ambalo lina idadi kubwa ya watu ili ziweze kuuzika na kukuza pato la Taifa.

Kauli hiyo imetolewa na MKUU wa Mkoa wa Pwani Injnia Evarist Ndikilo wakati wa sherehe za ufungaji wa maonyesho ya 9 ya wajasiriamali wadogo wadogo kutoka kanda ya mashariki yaliyofanyika katika viwanja vya Mwanakalenge Wilayani Bagamoyo.

Ndikilo alisema kwamba ili bidhaa zinazotengenezwa na wajasiriamali wa Tannzania ziweze kuuzika katika soka la afrika mashariki kunahitajika juhudi za makusudi kutoka kw amamalaka ya chakula na dawa (TFDA) pamoja na Shirika la viwango Tanzania (TBS) kuzingatia maagizo waliyopatiwa na serikali wakati wa ufunguzi wa maonyesho hayo ili kuweza kukuza uchumi wa nchi.

Ndikilo akizungumzia kuhusina na changamoto inayowakabili wajasiriamali hao katika suala la upatikanaji wa vifungashio katika kuhifadhi bidhaa zao amesema kwamba serikali ya awamu ya tano kupitia Wizara ya viwanda na biashara ipo tayari kutoa fungu la fedha kwa ajili ya kuweza kuwa na vifungashio hapa nchini kuliko kuviagizia kutoka nje ya nchi kwani ni gharama kubwa.

“Kwa upande wangu mimi napenda kuchukua fursa hii ya kuwaomba wajasiiamali kuwa wabunifu katika bidhaa ili kuweza kuleta ushindani mkubwa katika soka la afrika mashariki kwani kule ndio kuna idadi ya watu wengi zaidi kwa hivyo mkilizingatia hilo kutaweza kuleta mabadiliko chanya ya kuleta maendeleo,”alisema Ndikilo.

Aidha Ndikilo aliwataka wakuu wa Wilaya na wakurugenzi wote nchini kuhakikisha wanatenga maeneo maaalumu kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vidogo vidogo na vikubwa ambayo vitaweza kusaidia kwa kisi kikubwa kuwapatia ajira vijana ambao wengi wao hawana kazi za kufanya.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la viwanda vidogovidogo (SIDO) Tanzania Profesa Syvester Mpanduji alibanisha kwamba maonyesho hayo yameweza kuwapa fursa wajasiriamali kubadilishana ujuzi kupata mafunzo ikiwemo pamoja na kukuza uchumi wao kutokana na kuuza bidhaa zao .

Nao baadhi ya washiriki katika maonyesho hayo akiwemo Jacob Luis, Jania Omary pamoja na Rehema John walisema kwa sasa wanakabiliwa na chngamoto kubwa ya kutokuwa na vifungashio maalumu kwa ajii ya bidhaa zao hivyo wameimba serikali kupitia wizara ya viwanda na biashara kuwasaidia ili kuweza kufikia malengo yao.

MAONYESHO hayo ya kanda ya mashariki ambayo yamefungwa rasmi na mKuu wa Mkoa wa Pwani yameandaliwa na shirika la viwanda vidodovidogo (SIDO) Tanzania na yamewashirikisha wajasiriamali wadogo wadogo na wale wa kati zaidi ya 200 kutoka mikoa mitano ya Dar es Salaam, morogoro, Lindi, Mtwara , pamoja na wenyeji Mkoa wa Pwani .

Dkt. Bilal aipongeza Serikali kwa kuridhia Makubaliano ya Paris2015

Na: Frank Shija, MAELEZO.

Serikali ya pongezwa kwa hatua ya kuridhia makubaliano ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, Paris 2015 UN Climate Change Conference COP21.CMP11.

Pongezi hizo zimetolewa na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhadhiri wa Heshima wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere 2016, Mhe. Mohamed Gharib Bilal alipokuwa akitoa muhadhara katika Tamasha la Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Hali ya Hewa leo Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Bilal amesema kuwa kitendo cha Tanzania kuridhia makubaliano haya ya Paris kina maana kubwa sana katika suala zima la kukabiliana na athari za Mabadiliko ya Tabia nchi na utunzaji wa mazingira kwa ujumla.

“Niipongeze Serikali yetu kwa kuridhia kuingia katika makubaliano ya Paris ya mwaka 2015 hii itakuwa hatua muhimu sana katika jitihada za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi”. Alisema Dkt. Bilal. 

Aidha Dkt. Bilal aliongeza kuwa athari za mabadiliko ya hali ya hewa ni makubwa sana hivyo ni vyema tukachukua tahadhari kubwa katikakuhakikisha tunakabiliana nayo.Tuweke utamaduni wa kuhifadhi na kuyatunza mazingira yetu ili vizazi vijavyo visije kupata taabu itokanayo na uharibifu wa mazingira unaoweza kuepukika.

Hakikisheni mnatunza mazingira kwani kufanya uharibifu kunapoteza uhakika wa maisha kwa viumbe hai, pamoja na kupoteza vyanzo vya mapato,hivyo ni vyema tukajiepusha na matumizi ya baruti, uvuvi haramu, ukataji miti na mikoko.

Kwa upande wake Balozi wa Norway nchini Balozi Hanne – Marie Kaarstad, amesema kuwa Tamasha la Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi limekuja wakati muafaka ambapo dunia imeathiriwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya hali ya hewa.

Amesema kuwa Tanzania inaeneo kubwa la mwambao ambalo lina ulinzi wa asili hivyo ni vyema kuvilinda kwa kufanya usafi ilikuendeleza uhai wa viumbe hai vilivyopo majini na nchi kavu.

Naye Mwenyekiti wa Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi Profesa. Pius S. Yanda alisema kuwa Tamasha hilo limewakutanisha wadau kutoka nchi za Afrika Mashariki kwa lengo la kushirikiana katika kukabiliana na changamoto za Mabadiliko ya Tabia nchi.

Profesa Yanda aliongeza kuwa wataendelea kushirikiana baina ya nchi za Afrika kama na huu ndiyo mwanzo mzuri tulioanza nao, pia alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Norway kwa shirikiano wao katika Nyanja ya mazingira ambapo alisema Norway inafadhili takribani PhD 11 katika eneo la mazingira.

NI MUHIMU ICC NA AFRIKA KUZUNGUMZA –TANZANIA

Na Mwandishi Maalum, New York 

Jamhuri ya Muugano wa Tanzania imeishauri Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ( ICC) kukaa meza moja na nchi wanachama wa Mkataba wa Roma hususani zile za Afrika ili kutafuta suluhu ya changamoto na tofauti zilizopo kati ya mahakama hiyo na wanachama wake. 

Tanzania imetoa wito huo siku ya jumatatu kupitia Mwakilishi wake wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi, wakati Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, lilipopokea na kujadili Taarifa ya Utendaji ya Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai. 

Taarifa ICC imewasilishwa na Rais wa mahakama hiyo Jaji Slivia Fernandez de Gumendi katika kupindi ambacho Jumuiya ya Kimataifa imekumbwa na taharuki baada ya wanachama wawili wa Mkataba wa Roma, Afrika ya Kusini na Burundi kuwasilisha rasmi katika Umoja wa Mataifa kusudio la kujiondoa huku Gambia nayo ikitangaza kutaka kujitoa ingawa bado haijawasilisha rasmi nia yake hiyo. 

Mwakilishi huyo wa Tanzania katika mchango wake amesema, uwepo au kuanzishwa kwa ICC kulitokana kwa kiasi kikubwa na uungwaji mkono kutoka Afrika. Akasema uungwaji mkono huo ulitokana hasa baada ya nchi hizo za Afrika kukatishwa tamaa na kuvunjika moyo baada ya kutokea kwa mauaji ya kimbari nchini Rwanda. 

“Baada ya kukatishwa tamaa na kuvunjwa moyo, Mahakama hii, ilikuja kuwa chombo cha kutenda haki dhidi ya watu waliojihusisha na vitendo vya kikatili vikiwamo vya ukatili dhidi ya binadamu, uhalifu kivita na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu. Madhira yasiyoelezeka yaliyotokea Barani Afrika yakaifanya mahakama hii kuwa chombo cha matumaini dhidi ya wale ambao hawakuweza kuguswa au walikuwa juu ya sheria”. Akasema Balozi Manongi 

Na kuongeza. “ Kama nchi mwanachama wa Mkataba wa Roma wa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai na Mwanachama wa Umoja wa Afrika. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua kwamba, uhusiano kati ya mahakama na Afrika ni ule wa misuguano, na ni uhusiano ambao umeleta hofu ya Afrika kujitoa”. 

Balozi Tuvako Manongi akaeleza zaidi kwamba, hofu hiyo ya kujitoa kwa Afrika katika mahakama hiyo, haipaswi kuwepo kutokana na mambo kadhaa ambayo Afrika imejipanga kuyatekeleza kwa manufaa ya bara hilo na watu wake. Baadhi ya mipango hiyo ni utekelezaji wa ajenda ya Maendeleo ya Umoja wa Afrika maarufu kama agenda 2063 ambayo pamoja na mambo mengine inachagiza katika utawala bora, demokrasia, usawa wa jinsia, kuheshimu haki za binadamu, haki na utawala wa sheria.. 

“Viongozi wa wakuu wa nchi na serikali wa Afrika wameutangaza mwaka 2016 kuwa mwaka wa haki za binadamu huku mkazo ukielekezwa katika haki za wanawake. Na katika kutambua kuwa Amani na Haki ni vitu ambavyo haviwezi kutenganishwa, kwa sababu hizo, tunachotakiwa kuhimiza leo sana sana ni majadiliano”.Akasisitiza Balozi. Tanzania pia ikaeleza kwamba ni vema Mahakama hiyo katika utekelezaji wa majukumu yake ikajenga mazingira ya kuaminiana kati yake na wanawachama wake. 

Tanzania pia kupitia Mwakilishi wake, imezitaka nchi hususani zile za mataifa yaliyoendelea kuacha kuzihubiria nchi zinazondelea kama vile zenyewe ni adilifu sana. Na kusisitiza kwamba, kinachotakiwa wakati huu si kunyosheana vidole au kulaumiana bali kufanya kazi kwa pamoja ili kuifanya mahakama hiyo iendelee kutekeleza majukumu yake kwa uwazi , haki na kuaminiwa. 

Akasisitiza pia kuwa hata kama matatizo yaliyopo baina ya ICC na Africa yatapatiwa ufumbuzi. Bado kuna haja na umuhimu kwa nchi za Afrika kuziimarisha na kuzijengea uwezo Taasisi zake na vyombo vinavosimamia utoaji wa haki na utawala wa sheria ili viweze kushughulikia makosa ya jinai yakiwamo ya ukatili dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita badala ya kusubiri au kutegemea mahakama za kimataifa kama ICC. 

Akabinisha kuwa nchi zinatakiwa kuwajibika kikamilifu siyo kwa kuhofia kuingiliwa mambo yao ya ndani na ICC bali kwa sababu zinaowajibu wa kwanza wa kuwalinda raia wao. “Kwa Afrika matukio kama yale ya Jamhuri ya Afrika ya Kati, Cote d’ Ivore, Rwanda na Sierra-Leone ni kielelezo cha hatari ambayo tunatakiwa kujikinga nayo. 

Vile vile Tanzania imelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, kutopeleka ICC rufaa zenye malengo wa kisiasa kwani kwa kufanya hivyo kunachangia kuharibu sifa ya ICC na kuifanya isiaminiwe na kuonekana inatumiwa na wakubwa kutimiza malengo yao. Pamoja na kulitaka Baraza la Usalama kutoingiza siasa katika rufaa zake, Tanzania pia imewashangaa baadhi ya wajumbe wa Baraza hilo na ambao si wanachama wa Mkataba wa Roma kuwa mstari wa mbele katika kupeleka rufaa kwenye Mahakama hiyo dhidi ya mataifa mengine. 

Wazungumzaji wote zaidi ya 50 walioomba kuchangia Taarifa hiyo ya ICC pamoja na kuzungumzia utendaji kazi na changamoto zinazoikabili Mahakama hiyo, walijielekeza zaidi katika kuelezea masikitiko yao juu ya uamuzi wa Afrika ya Kusini na Burundi kujitoa. Wasemaji hao kama ilivyokuwa kwa Tanzania walisisitiza sana umuhimu wapande zinazopingana kukaa mezani na kuzungumza huku baadhi yao wakizitaka Afrika ya Kusini na Burundi kufikiria upya uamuzi huo. 
Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,Balozi Tuvako Manongi akizungumza wakati Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipopokea na kujadili Ripoti ya Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ( ICC) hapo jumatatu. Katika kuchangia Ripoti hiyo, Tanzania imesisitiza haja na umuhimu kwa ICC kukaa na kuzungumza na Nchi za Afrika ili kutafuta suluhu ya misuguano baina ya pande hizo mbili.