Tuesday, November 1, 2016

Sababu tano za kuunga mkono Muswada wa Huduma za Habari 2016


Fatma Salum- MAELEZO

Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari wa mwaka 2016 ambao unatazamiwa kuwasilishwa kwa mara ya kwanza bungeni katika kikao kilichoanza Novemba 1 mwaka huu umezua mjadala mkubwa na mpana miongoni mwa wadau wa sekta ya habari.

Mjadala wa muswada huu umekuwa ni mkubwa ukilinganisha na miswada mingine kwa sababu ukweli ni kwamba kila mtanzania ni mdau wa sekta hii ambayo wote tunaitegemea kwa kupata taarifa zinazoaminika ili kutusaidia kufanya maamuzi mbalimbali katika maisha yetu ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Usahihi wa maamuzi yote makubwa tunayoyafanya mmoja mmoja au kwa pamoja kama jamii – iwe kuchagua vongozi, kuchagua kozi ya kusoma na mengineyo yanategemea sana taarifa tulizonazo.

Ili tuweze kupata taarifa sahihi ni muhimu vyombo vya habari na waandishi watengenezewe mazingira mazuri ya kufanyia kazi, jambo ambalo ndiyo malengo ya sheria hii tarajiwa.

Licha ya ukosoaji mkubwa unaofanyika, ukweli ni kwamba Muswada wa Vyombo vya Habari 2016, kama utapitishwa, utajenga mazingira mazuri ya tasnia hii na kuirudishia heshima inayostahili.

Katika kupitia muswada huu nimeona faida nyingi za muswada, lakini kwenye makala hii nitataja faida tano kubwa.

Heshima ya tasnia

Kwanza, muswada huu unairejeshea tasnia hii heshima yake iliyoipoteza siku nyingi kwa kuifanya fani hii iwe miongoni mwa fani za uweledi, kama zilivyo nyingine zikiwemo udaktari na uanasheria.

Heshima ya tasnia hii inastahili kuwa juu na ndiyo maana vyombo vya habari vimeitwa mhimili wa nne, ukifanya kazi sambamba na mihimili mingine yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

Tasnia hii ilianza kupoteza heshima kuanzia miaka ya 1990 kufuatia mabadiliko ya kiuchumi, kijamii na baadae kisiasa (vyama vingi 1992) yaliyochochea kuibuka kwa vyombo vingi vya binafsi, hususan magazeti.

Tangu enzi hizo, changamoto kubwa ya fani hii imekuwa ni ukosefu wa udhibiti kiasi kwamba kila anayejisikia, bila kujali kasoma au la, anaingia. Matokeo yake waandishi wasiosoma (makanjanja) wamekuwa wakifanya madudu na lawama zimeelekezwa kwa wanahabari wote. Akioza samaki mmoja ndiyo wote.

Kwa sasa waandishi wanatazamwa kwa kejeli, wanatukanwa, wanabezwa na yote haya ni kwa sababu ya kundi la waandishi wasio na maadili na ambao hawana ukomo wala miiko katika kutafuta habari na wanachokiandika ni tofauti na walivyopokea kutoka katika chanzo chao cha habari.

Mara nyingi tunasikia mwandishi anavamia stara za watu katika majumba yao au katika maeneo yao ya starehe kwa jina la kutafuta habari. Kwa hali hii, ni vigumu kulaumu vyanzo (source) wanapokataa kuzungumza na vyombo vya habari. Yote haya ni kwa sababu ya waandishi waliokosa taaluma na weledi (makanjanja).

Uholela wa kuingia katika fani hii ulitokana na sababu mbili kubwa, kwanza kisingizio cha kipengele cha katiba kinachomhakikishia kila mtu haki ya kukusanya na kusambaza habari (Ibara ya 18.1) kwani baadhi ya watu wametafsiri kipengele hiki kuwa kila mtu anaweza kuwa mwandishi wa habari!

Sababu ya pili ni maendeleo makubwa ya teknolojia ambapo kila aliyeweza kujitengenezea blogu yake alifanya hivyo na kuanza kutafuta na kuchapisha habari.

Lakini ukweli ni kwamba tasnia hii si ya mchezo mchezo na kufanyia majaribio. Zipo nchi zilizosambaratika au kuingia katika vurugu kutokana na vyombo vya habari ambavyo havikuwajibika, vikashindwa kutanguliza uzalendo, weledi na kuzingatia maadili.

Muswada huu katika sehemu ya tatu, Ibara ya 10, unaondoa shida hiyo kwa kuweka Bodi ya Ithibati ya Wanahabari itakayowajibika kutoa vitambulisho (press card) kwa wanahabari kwa kuzingatia sifa na viwango vya elimu vinavyotakiwa. Bodi pia itasimamia kanuni za maadili ya wanahabari zilizoidhinishwa na kutunza orodha ya waandishi waliothibitishwa.

Ibara ya 18.1–2 inapiga marufuku wasio na vitambulisho (press card) kufanya kazi ya uandishi wa habari na ibara ya 47.2 inaweka adhabu ya faini isiyopungua Milioni 5 au kifungo cha hadi miaka mitano kwa wanaovamia tasnia ya habari na kutumia huduma ya habari kueneza habari za uongo kwa lengo la kuhatarisha ulinzi, amani na usalama wa nchi. Bila ya shaka sheria hii ikitekelezwa, heshima ya tasnia ya habari itarejea.

Msisitizo wa elimu

Ukiangalia hali halisi ya uandishi wa sasa, utagundua kuwa kiini cha tatizo ni watu kupita njia za mkato kuingia katika fani hii, yaani kutokuwa tayari kwenda shule kusoma.

Lakini hata wale waliosoma bado wanahitaji kuendelea kupigwa msasa juu ya namna bora ya kufanya kazi zao maana tasnia ya habari inabadilika kila uchao hususan upande wa teknolojia.

Miaka 20 iliyopita hatukuwa na blogu wala hakukuwa na Twitter, Facebook, Instagram na Whatsapp kama ilivyo sasa, lakini hizi ni silaha za mwandishi na anaweza kuzitumia kuboresha kazi zake.

Ukiangalia muswada huu utaona kuwa umeweka msisitizo mkubwa katika elimu ya waandishi wa habari kiasi kwamba bodi itakayoundwa ina jukumu la kuishauri serikali kuhusiana na mafunzo ya waandishi, kushauriana na taasisi za elimu ya mambo ya habari juu ya viwango vya elimu vinavyotakiwa kwa waandishi na muhimu zaidi bodi hii ina jukumu la kuandaa mafunzo ya waandishi wa habari.

Katika Ibara ya 21, muswada huu unazungumzia mfuko wa mafunzo ya habari wenye malengo matatu ikiwemo kuwezesha mafunzo kwa wanataaluma ya habari, kukuza program za uendelezaji wa maudhui ya ndani ya nchi na pia kuchochea na kuchangia utafiti na maendeleo katika nyanja za habari na mawasiliano ya umma.

Kwa mujibu wa Ibara ya 22, mfuko huo utapata fedha kutoka bungeni, misaada na zawadi na michango ya vyombo vya habari. Kwa hiyo ukisoma vifungu hivi unaona kuna faida nyingi ambazo iwapo muswada huu utapita na kutekelezwa ipasavyo, utasaidia kuhuisha tasnia ya habari.


Umuhimu wa Baraza Huru la Habari
Pia muswada huu umeainisha kuwa kutakuwa na Baraza Huru la Habari ambalo kazi na mamlaka yake yatatambulika kisheria. Kila mwanahabari aliyethibitishwa atakuwa mwanachama wa baraza hili.

Ibara ya 25 (1) inaeleza kazi za baraza hili kwa kushirikiana na Bodi ya Ithibati zitakuwa ni kuandaa na kuidhinisha kanuni za maadili ya taaluma ya habari pamoja na kukuza maadili na viwango vya taaluma baina ya wanahabari na kampuni za habari.

Uwepo wa baraza hili utapelekea tasnia ya habari kuwa taaluma rasmi inayotambulika kisheria kama taaluma nyingine, tofauti na baraza lililopo sasa ambalo halitambuliki kisheria hivyo mamlaka yake hayana nguvu.

Kulinda Maslahi ya Waandishi wa Habari
Sababu nyingine ya kuunga mkono muswada huu ni maslahi ya moja kwa moja kwa wanahabari. Sheria hii itasaidia sana kulinda maslahi ya waandishi wa habari pale wanapopata majanga wakiwa kazini, maradhi, kustaafu au kuachishwa kazi. 

Kila mwajiri atatakiwa kuweka bima na hifadhi ya jamii kwa kila mtu aliyeajiriwa katika chombo cha habari husika na wanahabari wa kujitegemea watapaswa kujiwekea kinga kwa mujibu wa sheria hii.
Jambo hili ni la kupongeza sana kwani sheria hii itasaidia kuboresha maslahi ya wafanyakazi kwenye tasnia ya habari.

Wengi wetu ni mashahidi kwamba kuna baadhi ya waandishi wa habari wamewahi kupata matatizo wakiwa kazini lakini wameishia kusubiri kuchangiwa na wasamaria wema ili wapate matibabu kwa vile hakuna kinga ya kuwabana waajiri au vyombo vya habari viweze kuwasaidia.
Mwelekeo kwa Vyombo vya Habari.


Sababu ya tano ya kuafiki muswada huu ni kwamba, pamoja na mambo yote sheria hii inatoa mwelekeo wa vyombo vya habari kuhusu jinsi ya kufanya kazi kwa ufanisi, kuzingatia maadili na weledi. Katika hili, sheria imeeleza majukumu ya vyombo vya habari vya umma na binafsi ili kuhakikisha majukumu hayo yanaleta tija kwa taifa.

Kwa kuzingatia hayo muswada huu una manufaa makubwa sio tu kwa wanahabari bali watu wote watanufaika kwa kupata taarifa sahihi zenye maudhui ya kuelimisha, kukosoa, kuonya na kuboresha bila ya kuudhi, kukiuka haki za wengine au kuharibu amani na usalama wa taifa letu.

No comments: