Tuesday, November 1, 2016

Dkt. Bilal aipongeza Serikali kwa kuridhia Makubaliano ya Paris2015

Na: Frank Shija, MAELEZO.

Serikali ya pongezwa kwa hatua ya kuridhia makubaliano ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, Paris 2015 UN Climate Change Conference COP21.CMP11.

Pongezi hizo zimetolewa na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhadhiri wa Heshima wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere 2016, Mhe. Mohamed Gharib Bilal alipokuwa akitoa muhadhara katika Tamasha la Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Hali ya Hewa leo Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Bilal amesema kuwa kitendo cha Tanzania kuridhia makubaliano haya ya Paris kina maana kubwa sana katika suala zima la kukabiliana na athari za Mabadiliko ya Tabia nchi na utunzaji wa mazingira kwa ujumla.

“Niipongeze Serikali yetu kwa kuridhia kuingia katika makubaliano ya Paris ya mwaka 2015 hii itakuwa hatua muhimu sana katika jitihada za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi”. Alisema Dkt. Bilal. 

Aidha Dkt. Bilal aliongeza kuwa athari za mabadiliko ya hali ya hewa ni makubwa sana hivyo ni vyema tukachukua tahadhari kubwa katikakuhakikisha tunakabiliana nayo.Tuweke utamaduni wa kuhifadhi na kuyatunza mazingira yetu ili vizazi vijavyo visije kupata taabu itokanayo na uharibifu wa mazingira unaoweza kuepukika.

Hakikisheni mnatunza mazingira kwani kufanya uharibifu kunapoteza uhakika wa maisha kwa viumbe hai, pamoja na kupoteza vyanzo vya mapato,hivyo ni vyema tukajiepusha na matumizi ya baruti, uvuvi haramu, ukataji miti na mikoko.

Kwa upande wake Balozi wa Norway nchini Balozi Hanne – Marie Kaarstad, amesema kuwa Tamasha la Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi limekuja wakati muafaka ambapo dunia imeathiriwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya hali ya hewa.

Amesema kuwa Tanzania inaeneo kubwa la mwambao ambalo lina ulinzi wa asili hivyo ni vyema kuvilinda kwa kufanya usafi ilikuendeleza uhai wa viumbe hai vilivyopo majini na nchi kavu.

Naye Mwenyekiti wa Kigoda cha Mwalimu Julius Nyerere cha Mazingira na Mabadiliko ya Tabia nchi Profesa. Pius S. Yanda alisema kuwa Tamasha hilo limewakutanisha wadau kutoka nchi za Afrika Mashariki kwa lengo la kushirikiana katika kukabiliana na changamoto za Mabadiliko ya Tabia nchi.

Profesa Yanda aliongeza kuwa wataendelea kushirikiana baina ya nchi za Afrika kama na huu ndiyo mwanzo mzuri tulioanza nao, pia alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Norway kwa shirikiano wao katika Nyanja ya mazingira ambapo alisema Norway inafadhili takribani PhD 11 katika eneo la mazingira.

No comments: