Thursday, December 6, 2018

NAIBU WAZIRI MHE. CONSTANTINE KANYASU AMPA MKANDARASI SIKU 30 KUKAMILISHA JENGO LA MALIASILI NA UTALII DODOMA

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe .Constantine Kanyasu ametoa siku 30 kwa mkandarasi wa SUMA JKT, aliyepewa kazi ya kujenga jengo la ofisi ya wizara hiyo katika mji wa serikali eneo la Ihumwa, Jijini Dodoma, kuhakikisha jengo hilo linakamilika ndani ya siku hizo alizopewa
Amemshauri Mkandarasi huyo kufanya kazi usiku na mchana ili aweze kukamilisha ujenzi wa jengo hilo ndani ya siku hizo 30. 

Ametoa rai hiyo mara baada ya kutembelea eneo hilo la ujenzi wa jengo la ofisi za Wizara hiyo linalotarajiwa kugharimu shilingi bilioni moja za kitanzania katika eneo la Ihumwa jijini Dodoma. 

Aidha, Mhe.Kanyasu ameitaka kandarasi ya SUMA JKT ihakikishe inajenga jengo hilo kwa umakini, umahiri na viwango vya ubora wa hali ya juu vinavyokwenda sambamba na hadhi ya Wizara yenye mchango mkubwa kwenye pato la Taifa. Pia, Mhe.Kanyasu ameielekeza SUMA JKT wakati ikiendelea na maandalizi ya ujenzi wa jengo iwe inatoa taarifa kila siku kwa kila hatua inayofikia katika Ujenzi wa jengo hilo kwa Uongozi wa Wizara. 

Awali, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw.Lusius Mwenda amemueleza Naibu Waziri huyo kuwa eneo hilo patakapojengwa Ofisi za Wizara hiyo lina ukubwa wa Hekta 2.27 .Ameongeza kuwa hata hivyo kuna eneo ambalo Wizara ilipewa mwanzo ambapo hatua kubwa zimeshafanyika ikiwa pamoja na kulifanyia usafi eneo hilo lakini baadaye wamepewa eneo jipya ambalo tayari hatua za maandalizi tayari zinaendelea. 


Eneo la Ihumwa katika Mji wa Dodoma ni eneo rasmi ambalo limetengwa na serikali kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya serikali yakiwemo ya wizara ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ofisi za serikali kuhamia rasmi Mjini Dodoma, kutokana na agizo lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli wakati akiingia madarakani mwezi Novemba 2015.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akizungumza na baadhi ya Wakurugenzi wa Wizara hiyo mara baada ya kutembelea eneo ambalo jengo la ofisi ya Wizara ya Maliasili na Utalii litakapojengwa ndani ya siku 30 katika mji wa kiserikali wa Ihumwa jijini Dodoma kwa kandarasi ya SUMA JKT litakalogharimu bilioni moja.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akipewa maelezo na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali watu wa Wizara hiyo, Bw. Lusius Mwenda mara baada ya kutembelea eneo ambalo jengo la ofisi ya Wizara ya Maliasili na Utalii litakapojengwa ndani ya siku 30 katika mji wa kiserikali wa Ihumwa jijini Dodoma kwa kandarasi ya SUMA JKT litakalogharimu bilioni moja.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akioneshwa eneo na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali watu wa Wizara hiyo, Bw. Lusius Mwenda mara baada ya kutembelea eneo ambalo jengo la ofisi ya Wizara ya Maliasili na Utalii litakapojengwa ndani ya siku 30 katika mji wa kiserikali wa Ihumwa jijini Dodoma kwa kandarasi ya SUMA JKT litakalogharimu bilioni moja. (Picha zote na Lusungu Helel 

No comments: