Saturday, October 20, 2018

SERIKALI, ACACIA WASAINI HATI ZA MAKUBALIANO KUTEKELEZA MRADI WA MAJI SHINYANGA NA GEITA


Halmashauri za Wilaya ya Msalala, Shinyanga (Shinyanga)  Nyang'hwale (Geita), Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji) na Wadau wa Maendeleo ambao ni ACACIA Mining PLC (kupitia Mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu) wamesaini hati za makubaliano ya kisheria kutekeleza  Mradi wa Pamoja wa Maji ujulikanao kama JOINT WATER PARTNERSHIP PROJECT (JWPP). 
Akizungumza jana wakati wa kutia saini makubaliano hayo (Legal Agreement) kijiji cha Ilogi halmashauri ya Msalala, Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo amesema katika mradi huo sehemu kubwa ya fedha za mradi zimetolewa na Serikali kupitia wizara ya maji na ACACIA Bulyanhulu Gold Mine Ltd ambapo pia halmashauri hizo tatu zinachangia kiasi cha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za mradi huo kutoka katika makusanyo yake ya ndani. 
Mradi huu utanufaisha jumla ya vijiji kumi na nne (14) kutoka katika Halmashauri za Wilaya tatu ambapo kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga  vijiji viwili ambavyo ni Mwenge na Mahando vitanufaika na mradi huo.
Kwa upande wa Halmashauri ya wilaya ya Nyang'hwale vijiji 6 ambapo ni Nyugwa, Mwamakiliga, Izunya, Kharumwa, Kafita na Lushimba vitanufaika kupitia mradi huo na kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Msalala  pia ni Vijiji 6 ambavyo ni Kakola Na. 9, Lwabakanga, Bushing'we, Kakola, Bugarama na Ilogi.
Profesa Mkumbo amesema Utekelezaji wa Mradi huu umegawanyika katika Awamu mbili. 
Awamu ya kwanza ambayo inahusisha utandazaji wa bomba kuu la kusafirisha maji kutoka bomba kuu la KASHWASA katika Kijiji cha Mhangu (Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga) hadi Tanki la kuhifadhia maji katika kijiji cha Ilogi (Halmashauri ya Wilaya ya Msalala) Bomba hili kuu la kusafirisha maji yaani Mhangu - Ilogi. 
Amesema Transmission Main ni la chuma na lina urefu wa kilimita 58.5 na vipenyo kati ya milimita 110 hadi milimita 400; zikiwemo bomba za matoleo kuwezesha usafirishaji wa maji kwenda kwenye vijiji 14 vitakavyonufaika na mradi huo. Utekelezaji wa shughuli za Mradi katika Awamu ya Kwanza umekwishaanza.
Amesema Awamu ya pili ya Mradi itahusisha ujenzi wa matanki mapya 11 ya maji yenye ujazo kati ya lita 45,000 hadi lita 900,000 pamoja na utandazaji wa bomba za mfumo wa usambazaji maji katika vijiji vyote 14 vilivyotajwa hapo juu. Utekelezaji wa shughuli za Mradi Awamu ya pili bado haujaanza.
Kuhusu Mkandarasi wa Utekelezaji wa Shughuli za Mradi Awamu ya Kwanza,amesema, utekelezaji wa shughuli za mradi kwa Awamu ya Kwanza unafanywa na Mkandarasi, Kampuni ya Kichina inayoitwa M/s. Beijing Construction Engineering Group (BCEG) Co. Ltd ambapo muda wa mkataba ni miezi kumi na mbili (12). 
Mkumbo pia amebainisha kwamba Msimamizi wa Shughuli za Ujenzi wa Mradi Awamu ya Kwanza ni Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jijini Mwanza (MWAUWASA), na kwamba awamu ya Kwanza ya Utekelezaji wa Shughuli za Mradi huu inatarajiwa kugharimu jumla ya Shilingi za Kitanzania Bilioni 13,860,873,200.
Mchanganuo wa uchangiaji wa Serikali pamoja na Wadau wa ACACIA Bulyanhulu Gold Mine Ltd katika gharama za mradi kwa upande wa serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji imechangia TSH 4,000,000,000/=, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala TSH 600,000,000/=,Halmashauri ya Wilaya ya Nyang'hwale TSH 600,000,000/= na Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga TSH 40,000,000 na  ACACIA Bulyanhulu Gold Mine Ltd USD 2,000,000.
Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akitia saini hati za makubaliano hayo (Legal Agreement) kutekeleza  Mradi wa Pamoja wa Maji ujulikanao kama JOINT WATER PARTNERSHIP PROJECT (JWPP).  Wa kwanza kulia ni Meneja Mkuu wa Migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi,Benedict Busunzu. 
 Viongozi wa ACACIA na Serikali wakitia saini hati za makubaliano hayo (Legal Agreement).
Viongozi wa ACACIA na Serikali wakielekea katika kijiji cha Ilogi halmashauri ya Msalala ambapo bomba la maji litapita.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akishiriki kuchimba mtaro katika eneo la Kijiji cha Bushing'we halmashauri ya Msalala ambapo bomba la maji litapita.
Meneja Mkuu wa Migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi,Benedict Busunzu akishiriki kuchimba mtaro katika eneo la Kijiji cha Bushing'we halmashauri ya Msalala ambapo bomba la maji litapita.
Katibu Mkuu Wizara ya Maji Profesa Kitila Mkumbo akizungumza baada ya kusaini hati za makubaliano ya kisheria kutekeleza  Mradi wa Pamoja wa Maji ujulikanao kama JOINT WATER PARTNERSHIP PROJECT (JWPP). 
Meneja Mkuu wa Migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi,Benedict Busunzu akizungumza baada ya kusaini hati za makubaliano ya kisheria kutekeleza  Mradi wa Pamoja wa Maji ujulikanao kama JOINT WATER PARTNERSHIP PROJECT (JWPP). 
Mkuu wa wilaya ya Kahama,Anamringi Macha akizungumza.
PICHA NA MPIGA PICHA WETU

No comments: