Tuesday, October 9, 2018

OLE NASHA ATOA AGIZO KALI KWA VIONGOZI NA WAZAZI MKOANI MANYARA


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipokelewa na Watendaji wa Mkoa wa Manyara wakati alipowasili mkoani hapo kwa ajili ya kupata taarifa ya Elimu ya Mkoa huo. Naibu waziri huyo yuko Mkoani Manyara kwa ziara ya siku tatu ikiwa ni muendelezo wa ziara zake ambazo amekuwa akizifanya kukagua miradi ya Elimu inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na kuangalia hali ya Elimu katika mkoa husika.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa maelekezo kwa Viongozi na watendaji wa VETA Manyara wakati wa kukagua karakana inayotumika na wanafunzi wanaosoma kozi ya ufundi wa zana za kilimo (Agro Mechanics).

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua maendeleo ya ujenzi wa karakana itakayotumiwa na wanafunzi wanaosoma kozi ya ufundi uwashi katika Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Manyara.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha amewataka viongozi kuanzia ngazi ya mkoa hadi vijiji nchini kote kuhakikisha wanafunzi wanaomaliza darasa la saba hawaondoki katika maeneo yao kwenda kufanya kazi za ndani wakati wakisubiri matokeo ya kuhitimu darasa la saba, kwani kufanya hivyo kunawaondolea fursa ya kuendelea na masomo pindi wanapofaulu.

Ole Nasha ametoa agizo hilo mkoani Manyara wakati akizungumza na viongozi hao kuhusu hali ya Elimu mkoani humo ambapo amewataka kusimamia kwa ukaribu suala hilo ili kutokatisha ndoto za watoto hao na kwamba wale wanaofanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

“Hakikisheni watoto wanaposubiri matokeo hawasafirishwi kwani wanapofika huko wanarubuniwa na waajiri hivyo hata matokeo yakitoka na kuonesha kuwa wamefaulu hawarejei kuendelea na masomo “alisisitiza Naibu waziri Ole Nasha.

Kiongozi huyo ameendelea kuwasisitiza wazazi kuwa fursa za Elimu katika nchi yetu ni kubwa, ikizingatiwa kuwa Elimu msingi ni bure hivyo hakuna kisingizio tena kuwa mtoto hawezi kusoma.

“wazazi msiwe sehemu ya kuchangia watoto wenu kwenda mjini kwa kuwa tu wanawatumia fedha kwa ajili ya matumizi bali hakikisheni mnawasimamia vyema watoto hao katika kipindi chote cha kusubiri matokeo na kuwapeleka shule pindi matokeo yanapotoka na kuonekana wamefaulu,” alisisitiza Naibu waziri Ole Nasha.Amewataka viongozi hao kutumia sheria kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kuanza shule wanaandikishwa ili kutokuwa na wimbi kubwa la watoto wa mitaani wasiokwenda shule.

Awali Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Arnold Msuya alimweleza Naibu waziri huyo kuwa mkoa kwa sasa una mwamko mdogo wa Elimu hasa katika jamii ya wafugaji hali inayopelekea wazazi kutowaandikisha shule watoto wenye umri wa kuanza shule

Naibu waziri Ole Nasha pia ametembelea Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi stadi cha Mkoa Manyara na kuwataka kuboresha Mitaala yao ili mafunzo wanayoyatoa yaendane na wakati ikiwa ni pamoja na kukidhi mahitaji ya soko la ajira ili kuongeza fursa ya vijana kujiajiri pindi wanapomaliza masomo yao.

Naibu Waziri huyo yuko mkoani Manyara kwa ziara ya kikazi kukagua miradi ya Elimu inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na kuangalia hali ya Elimu mkoani humo.

No comments: