Tuesday, October 2, 2018

OKTOBA 1 YA KILA MWAKA NI MWEZI WA ROZARI TAKATIFU

Na Mwandishi Wetu Globu ya Jamii

WAUMINI wa Kanisa Katoliki Duniani kote leo wameanza kusali Rozali Takatifu ikiwa kila mara husali lakini kwa mwezi huu inawalazimu kusali zaidi na unajulikana ni Mwezi wa Rozali.

Katika Kalenda ya Kanisa katoliki leo waumini wote wameanza kusali Rozari Takatifu kwa mujibu wa imani ya kanisa katoriki.Hivyo waumini wa Kanisa katoliki wanaalikwa kusali Rozari takatifu kila mara.

Oktoba ni mwezi ambao umewekwa kwaajili ya Bikira Maria na mama wa Kanisa waumini wa kanisa hilo leo wanasali Sala mbalimbali kwa mwombezi Bikira Maria.

HISTORIA YA ROZARI

Ni kwamba sala ya Rozari inasemekana kuanzishwa na Mt. Dominico aliyezaliwa mnamo mwaka 1170 na kufariki mwaka 1221 na hiyo sala Mt. Dominico aliipata kwa njia ya ufunuo ambapo Bikira Maria alimtokea na kumwamuru awe anasali rozari.

 Bikira Maria alimwamuru mtakatifu Dominico kusali rozari kwa kipindi hicho iwe kama silaha yake ili kupambana na uzushi uliokuwa umeibuka ukipingana na mafundisho ya Kanisa, na huo uzushi uliitwa ‘ Albigensia’ hili ni kundi lilokuwa na imani kuwa Duniani kuna nguvu nguvu mbili zenye uwiano sawa lakini hupingana na kupigana moja baada ya nyingine, nazo nguvu hizo ni Mungu na Shetani.

 Hivyo waliamini kabisa kuwa Mungu na Shetani wana nguvu sawa ( Dualistic ).Pia  waliamini kuwa dunia hii imejaa uovu kwa kuwa iliumbwa na mwovu. Ni kwa msingi huu Kanisa liliamua kupambana na hawa wazushi ambao pia walionekana kupotosha mafundisho ya Kanisa.

 Ndipo tunaona Bikira Maria anamtokea Mtakatifu Dominico na kumwambia asali rozari ili kupambana na mafundisho hayo ya kizushi. Ni Papa Pio V ambaye mnamo mwaka 1569 alihidhinisha rasmi kusali rozari kwa kanisa nzima na kuhidhinisha rozari iwe jinsi tunavyoiona sasa. 

Katika zile zama za kati watawa wamonaki walizoea kusali zaburi 150, na kwa upande wa waumini Walei ambao kwa kipindi hicho hawakujua kusoma zaburi iliwabidi wasali sala ya Baba yetu mara 150 badala ya zaburi 150 na hizo baba yetu walizisali kwa kuhesabu punje 150 zilizokuwa zimefungwa kwenye kamba ndefu ambayo kwa lugha ya kitaalamu iliitwa “ Corona” au kwa Kiingereza “ Crown” kadiri ibada kwa Bikira Maria ilivyoendelea kushamiri mnamo Karne ya 12, sala kwa Bikira Maria ilianzishwa na hivyo kuanza kusali salamu maria 150 baadala ya baba yetu 150.

Salamu Maria 150 hapo baadaye zilikuja kugawanywa katika makundi/ mafungu na Mtawa mdominica aliyeitwa Henry Kalkar ( 1328-1408), ambapo kila tendo la rozari lilikuwa na mafungu 50 ya salamu Maria ambapo pia kila fungu liligusia maisha ya Bikira Maria na Yesu katika historia ya wokovu wetu. 

Zaidi ya hapo mtawa mwingine wa mdominican aliyeitwa Alanus de Rupe aliendelea kugawanya hiyo historia ya matendo ya wokovu wetu katika matendo ya furaha,uchungu, nautukufu kama tunavyoyaona sasa. (NB Matendo ya mwanga hayo ni ya majuzi siyo ya wakati ule). 

Na ni kuanzia hapo Bikira Maria amepewa nafasi kubwa katika shirika la watawa wa Dominican. 

Hivyo utamaduni wa kusali rozari umeendelea karne hata karne, mfano Papa Leo XIII (1878-1903) aliweka msisitizo mkubwa juu ya ibada ya rozari kwa Bikira Maria. 

Kuanzia Septemba 1 mwaka 1883 Baba Mtakatifu Leo XIII aliandika jumla ya barua za kichungaji 11 zote zikiwa zinaweka mkazo juu ya rozari.

 Hivyo Rozari ni sala inayotokana na maandiko matakatifu( Biblia).

 Mafumbo ya rozari yote yanapatikana katika agano jipya ambapo ndo tunaona matendo ya Bikira Maria na Yesu Kristo katika wokovu wetu.

Waumini wanakumbushwa uchungu aliopata Bikira Maria Katika maisha yake hasa ule utabiri wa Simeoni kwa Bikira Maria juu ya mateso na kifo cha mwanae Yesu, Matendo saba ya furaha kwa Maria ambapo yaananza na kupashwa habari kwa Bikira Maria na Malaika wa Bwana, kupalizwa mbinguni, na matendo ya huruma ya Bikira Maria kwa wale ambao wanaendelea kuteseka hapa duniani.

No comments: