Thursday, October 25, 2018

KAIMU SHEIKHE WA MKOA WA MWANZA AELEZA MIKAKATI YA KUBORESHA UCHUMI WA VIONGOZI, WALIMU NA MASHEIKHE


Kaimu Sheikh wa Mkoa wa Mwanza Hassan Musa Kabeke akizungumza na wajumbe wa halmashauri ya BAKWATA mkoani Mwanza, masheikhe wa wilaya, Kata na Misikiti ya wilaya zote za Mwanza jana, kwenye ukumbi wa mikutano wa baraza hilo Mbugani katika Wilaya ya Nyamagana jana. Picha na Baltazar Mashaka


Kiamu sheikh wa Mkoa wa Mwanza Hassan Musa Kabeke akiweka saini kwenye kitabu cha wageni kwenye ofisi za Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Mwanza jana tangu ateuliwe kushika wadhifa huo. Wanaoshudia wa kwanza ni Mwenekiti wa Halmashauri ya baraza hilo Amran Batenga, aliyekuwa akikaumu nafasi hiyo Hamis Almas na Kaimu Katibu wa baraza hilo mkoani humu Sina Mwagalazi.

Kaimu Katibu Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Mkoa wa Mwanza, sina Mwagalazi akizungumza na wajumbe wa Halmashauri kuu ya baraza hilo, masheikhe wa wilaya na kata wa wilaya za mkoani humu.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya BAKWATA Mkoa wa Mwanza Amran Batenga akizungumza na wajumbe wa halmashauri hiyo, masheikhe wa wilaya na kata za mkoani humu jana kwenye ukumbi wa baraza hilo Mbugani katika Wilaya ya Nyamagana.

Kaimu Sheikhe wa Mkoa wa Mwanza Hassan Musa Kabeke akiteta jambo na mtangulizi wake Sheikh Hamis Almas muda mfupi baada ya kumvisha joho.


NA BALTAZAR MASHAKA, MWANZA

KAIMU Sheikhe wa Mkoa wa Mwanza Hassan Musa Kabeke amesema moja ya vipaumbele vyake ni kuimarisha uchumi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na elimu ya dini.

Sheikhe Kabeke alitoa kauli hiyo jana kwenye ukumbi wa ofisi za BAKWATA zilizopo Mbugani katika Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza, wakati akizungumza na wajumbe wa halmashauri ya mkoa, masheikh wa wilaya na kata mkoani humu.

Alisema miongoni mwa mambo yanayomkera ni hali duni ya maisha na udhalili (unyonge) hivyo ameweka mikakati na mipango ya kuimarisha uchumi wa BAKWATA ili kubadilisha maisha ya walimu wa madrasa, masheikhe na maimamu wa misikiti ambao ni zao la uislamu (kiwanda) na misingi ya dini hiyo ya Kiislamu.

Kaimu Sheikhe huyo wa mkoa alisema madrasa na msikiti ndio eneo dhaifu kutokana na walimu na masheikhe kushindwa kufundisha elimu ya dini na hata ujira wao ni mdogo wanazidiwa na watumishi wa ndani jambo ambalo linamkera na hivyo ameamua kulitafutia tiba.

Sheikhe Kabeke alieleza kuwa ili kuboresha hali za walimu wa madrasa,masheikhe na maimu na waumini wa kiislamu lazima kuwe na vyanzo vya mapato yatakayosaidia Waislamu na haiwezekani kuendelea kuwa na BAKWATA ombaomba.

“Niwaondoe hofu maana wapo watu wanaosema mimi ni mkali la hasha, mimi nina msimamo kwenye haki.Sote tunachukia ufisadi, wizi na umaskini na hata Mufti wa Tanzania kilio chake ni kutaka kuwatoa waislamu kwenye udhalili (unyonge).Katika hili la kuimarisha uchumi hata mkinilaumu niko radhi na Mwenyezi Mungu atanihukumu,”alisema Sheikhe Kabeke.

Alisema waislamu hawana sababu ya kuwa wanyonge na wasimuone mkali bali atautumia na kuendelea na ukali huo kuwaondoa kwenye unyonge wao kuwataka viongozi dini ya kiislamu na waumini kutumia neema waliyopewa na Mungu kutafuta pepo na nyumba ya ahera.

Aliongeza kuwa BAKWATA ina hali mbaya kiuchumi na ni taasisi pekee isiyo na wanachama wanaolipa ada wakati chombo hicho kinawapa heshima hivyo kwa Mkoa wa Mwanza dira na mipango yake ya kuleta maendeleo viongozi wa ngazi ya mkoa watachangia sh.8,000 mwezi sawa na sh. 2,000 kwa wiki fedha ambazo zitawekwa kwenye akaunti maalumu.

“Tunataka kujenga uchumi kwa kuangalia rasilimali watu na kuanzia Oktoba viongozi watachanga sh. 8,000 kwa ngazi ya mkoa, wilaya sh. 4,000 , kata sh. 500 na tayari akaunti imefunguliwa kwa usalama wa fedha hizo ili ndani ya miaka tujenge jengo la kitega uchumi, kulipa mishahara ya walimu wa madrasa na masheikhe na kutatua kero zao,” alifafanua Sheikhe Kabeke.

Aidha,kuhusu elimu ambayo imegawanyika sehemu tatu, aliwawataka waislamu kuacha kulalamika kuwa taasisi yao inahujumiwa na kuchafuliwa pamoja na kupoteza akidi yao ilhali wenye dhamana ya kufundisha elimu ya dini shuleni hawatimizi wajibu wao na kusababisha vijana waliolelewa kwa misingi ya dini kiislamu wakosekane.

Alisistiza kuwa kama huo ni ukali basi hana budi kuacha hali iendelee ili uislamu ufe na kutoweka kwa sababu masheikhe na walimu hawaoni umuhimu wa kufundisha elimu ya dini shuleni licha ya kutengwa kwa vipindi vya dini.

Kaimu Sheikh huyo wa mkoa alimshukuru Mufti wa Tanzania Abubakar Zuberi bin Ali kwa na Baraza la Ulamaa kwa kumteua, kumuona na kumuamini kuwa anafaa kumsaidia kwenye nafasi hiyo kubwa ambayo si ya kukimbiliwa na kuahidi kuwa kwenye uongozi wake hatabadilika na atakubali kushauriwa.

No comments: