Tuesday, August 14, 2018

Biteko atoa wiki moja kwa muwekezaji kulipa kodi ya madini serikalini

Naibu waziri wa madini, Dotto Biteko akizungumza na wachimbaji wadogo wa eneo la Kilalani, baada ya kutembelea eneo hilo.

Na Zuena Msuya, Tanga

Serikali imempa muda wa wiki moja nwekezaji mmiliki wa kampuni ya Amazon Trading (T)Company Limited Abdi Hozza kuhakikisha anailipa serikali kodi ya pango ya uwekezaji kiasi cha dola za Marekani 70,020 sawa na zaidi ya shilingi milioni 140 za kitanzania anazodaiwa tangu mwaka 2011 katika machimbo ya Kalalani eneo la Umba wilayani Korogwe kutokana na leseni nane za uchimbaji wa madini kuanzialeseni namba (102-109/2001) anazomiliki .

Sambamba na hilo imeiagiza serikali ya wilaya ya Korogwe kuhakikisha inatenga maeneo ya wachimbaji wadogowadogo wa madini ili kuepusha migogoro iliyodumu kwa muda mrefu hali ambayo imeleta hali ya chuki baina ya mwekezaji na wananchi.

Waziri Biteko alitoa agizo hilo alipotembelea katika machimbo hayo juzi Jumamosi katika vijiji vya Kigwasi na Kalalani kata ya Kalalani wilayani humo. Biteko alimtaka ndani ya wiki moja mwekezaji huyo kulipa kodi hiyo ya pango anayodaiwa na serikali na amewataka wananchi kutoa ushirikiano katika kuwabaini wageni na watu wanaonunua madini kwa njia za panya.
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko, akikagua Mabaki ya mgodi wa Amazon,ambao umesitisha uchimbaji kwa miaka mingi kutokana na Matatizo mbalimbali.

“Haiwezekani tangu madini yaanze kuchimbwa katika machimbo haya serikali haijapata kodi kutokana na mgodi huu tunakuta sifuri nimewaambia wailipe haraka nataka nikifika Dodoma kuna commitment statement mnalipa lini” alisema.

Aliongeza “Na yule anayedhani atakuja Kalalani kununua madini kwa njia ya panya muda huo umekwisha,na tumekwenda kwenye mto tumekuta mnachimba madini,sheria inakataza kuchimba madini kwenye vyanzo vya maji naomba kuanzia sasa mkaondoe vifaa vyenu kule mtoni”.

Aidha Waziri Biteko, aliongeza kuwa eneo hilo la Kalalani lina leseni za wachimbaji wadogo wa madini ya vito zipatazo 400 lakini leseni zilizohai na zinaendelea kufanya kazi ya uchimbaji ni 70 tu kati ya hizo. Awali diwani wa kata hiyo Amati Ngerera alimueleza naibu waziri kuwa mwekezaji huyo(Amazon)hana mahusiano mazuri na wa wanakijiji pamoja na wachimbaji wadogowadogo wa hapo kutokana baada ya

kupewa leseni na serikali kwa ajili ya kuendesha shughuli za uchimbaji katika eneo hilo alilitelekeza kwa muda mrefu bila ya kuendeleza shughuli zozote na wananchi wengi ambao shughuli zao kubwa ni uchimbaji waliokuwa wakiingia eneo hilo walifanyiwa vitendo vya visivyokuwa vya kibinadamu ikiwemo kupigwa risasi,kubakwa na askari aliowaweka kulinda eneo hilo.

Diwani huyo alikwenda mbali zaidi kuwa mwekezaji huyo huwa anatumia eneo hilo kama dhamana ya kukopa fedha kutoka kwenye taasisi za fedha na alimpa mwenzake anaitwa Najim kuendesha mgodi huo kinyemela bila ya serikali kuwa na taarifa.

“Huyu mwekezaji leseni yake ilikwisha tangu mwaka 2001,wananchi wakaomba leseni ya uchimbaji na yeye akaomba ,lakini baadae akaingia mkataba na mfanyabiashara anayeitwa Najim halafu yeye akajitoa kabisa na huyo Najim hachimbi bali anafanya shughuli zake za biashara ya utalii na huyu Amazon anatumia eneo hili kukopea fedha kwenye taasisi za fedha ”alisema.

Aliongeza “Serikali ya kijiji ilifanya mapendekezo matatu na kuyapeleka katika baraza la madiwani na baadae tukayandika kuyaleta katika ofisi yako,mapendekezo haoy ni eneo hilo litafutwe mwekezaji mwenye sifa ya uwekezaji,nyumba zilizopo eneo la mgodi zirudishwe serikalini ambazo waasisi wake ni STAMICO na wananchi wakatiwe eneo ili waweze kufanya shughuli za kiuchumi za uchimbaji”.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Kigwasi, Loronyotu Lakaney alimueleza Naibu Waziri kuwa mbali na mgodi huo kutelekezwa na mwekezaji huyo pia madini yanatorosha kwa njia za panya na kuuzwa Voi nchini Kenya.

“Mheshimiwa Naibu waziri mbali na mgogoro huo pia wachimbaji wengi wadogowadogo wakishapata madini wanakwenda kuyauza Voi mpakani mwa Kenya na Tanzania upande wa hapa Tanga kutokana hakuna udhibiti na hakuna minada ya madini inayoendeshwa kama serikali ilivyoagiza”alisema.

Naye mwekezaji huyo alimueleza Naibu waziri kuwa alichelewa kulipa hiyo kodi kutokana Kutokupewa taarifa yoyote ya kuendeleza mgodi wala kudaiwa kodi.

“Mheshimiwa Naibu waziri mimi ni kweli kwa muda mrefu sijapaendeleza hapa baada ya leseni yangu kwisha mwaka 2011 sijapewa leseni nyingine wala sijapata hiyo barua ya kulipa hiyo kodi ya pango”alisema.

Taarifa ya ofisi ya Afisa Madini Mkazi mkoa wa Tanga amabayo gazeti hili inayo nakala yake ilishapendekeza kwa kamishna wa madini leseni hizo nane za mwekezaji ziandikiwe hati ya makosa(default notice) na hatimaye zifutwe kwa mujibu wa sheria ya madini mwaka 2010,lakini kwenye mfumo wa flexicadastre leseni hizo zinaonesha zipo hai(active in default) ingawa zilishaisha muda wake tangu Septemba 30,2011.

No comments: