Wednesday, February 7, 2018

UTUNZAJI FEDHA BADO NI CHANGAMOTO KWA WATANZANIA

Na Said Mwishehe,Blogu ya jamii

BENKI Kuu ya Tanzania(BoT) imesema bado ni changamoto kwa watanzania walio wengi katika kutunza fedha za noti na noti ya sh.500 na noti ya Sh.1000.

Hayo yamesemwa leo mkoani Mtwara na Meneja Msaidizi Idara ya Sarafu kutoka Benki Kuu Tanzania(BoT) Dolla Abdull wakati akitoa mada kwa waandishi wa habari waliokuwa kwenye semina iliyoandaliwa na benki hiyo kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuandika taarifa sahihi za uchumi.

Akifafanua kuhusu fedha chakavu, amesema noti ya Sh.500 ndio inayochakaa zaidi ukilinganisha na noti nyingine inayofuata kwa kuchakaa ni ya Sh.1000.Amesema sababu ya fedha hizo kuchakaa haraka inatokana na kutumika zaidi kwenye mzunguko wa fedha hasa kwa kuzingatia kundi kubwa la wananchi ndio watumiaji wakubwa.

"Hii noti ya Sh.500 na ya Sh.1000 zinatumika zaidi ukilinganisha na noti ya sh 10,000. Ni fedha ambazo zipo kwenye mzunguko zaidi." Pia utunzaji wa fedha bado changamoto kubwa katika jamii na ndio maana zinachakaa mapema.Ukifuatilia zaidi utabaini hizi noti za Sh.500 wengi ambao wanazitumia hawazitunzi vizuri na wala haziwapeleki benki,"amesema Dolla.

Amefafanua sababu nyingine ya fedha hizo kuchakaa haraka inatokana na ukweli uliopo watanzania ambao wwnatunza fedha zao benki hawazidi asilimia 14.Hivyo amesema sehemu kubwa ya fedha inabaki mtaani na matokeo yake zinachakaa. "Ujue fedha nayo ina umri wake wa kuishi ambapo kwa fedha za noti ni zinaishi kati ya miezi sita hadi saba.

" Kazi yetu idara ya sarafu ni kuhakikisha tunapeleka fedha safi katika mzunguko na zile ambazo zimechakaa tunazisaga katika mashine maalumu,"amesema Dolla.

Ametoa ombi kwa Watanzania kuhakikisha wanatunza fedha hizo kwani Serikali inatumia gharama kubwa kuchapa fedha hizo huku akifafanua fedha ni moja ya alama ya nchi yetu,hivyo lazima zitunzwe vizuri.Amesititiza wananchi kutunza fedha zao benki kwani ni njia moja wapo ya kuzifanya fedha kuwa safi huku akiwakumbusha wenye fedha zilizochaa kuzipeleka benki ili zibadilishwe.

Dolla amesema wao wamekuwa na utaratibu wa kuchukua fedha ambazo zimechaa ambazo zinapelekwa BoT na kisha kuzichambua kwa vifaa maluum."Zile ambazo zitaonekana kuchakaa sana zitasagwa na zile ambazo zitakuwa bado kulingana na vigezo vyetu basi zitarudi kwenye mzunguko," amefafanua Dolla.

Alipoulizwa iwapo wamefanya utafiti kubaini mikoa ambayo inaongoza kwa wananchi kutumia fedha zilizochakaa,Dolla amejibu mkoa wa Kigoma in moja ya mkoa ambao fedha zinaokana kuchakaa.Amesema sababu mojawapo inaonesha bado wananchi walio wengi hawana muako katika kutunza fedha na pia miundombinu ya usafiri ndani ya mkoa huo inachangia fedha zinazochakaa huchelewa kusafirishwa ili zibadilishwe.

Wakati huohuo,waandishi walioko kwenye semina hiyo walitaka kufahamu kwanini Tanzania kuna noti ya Sh.10,000 wakati katika nchi nyingi ikiwamo Marekani noti waliyonayo ni dola 100 tu na hata Kenya hawana noti ya 10,000.

Wajibu awali hillo BoT imesema moja ya sababu ya kuwa na noti ya Sh.10000 ilisababishwa na mfumko wa bei uliotokea miaka ya 1980 na mwanzoni kwa mwaka 1980.Inaelezwa katika miaka hiyo mfumko wa bei ulikuwa asilimia 30,hivyo ili kukabiliana na hali hiyo ndipo ilipotengenezwa noti hiyo.

Hata hivyo kikubwa ni kudhibiti mfumko wa bei ili kuhakikisha tunabaki tulipo.Kuhusu sarafu ya senti kurudishwa kwenye mzunguko,Dolla amesema siku za karibuni awali hilo lilijibiwa vizuri bungeni,ila kwa kuongezea ni kwamba sarafu za senti bado zipo na ndio maana kwenye vitabu vya benki zipo.

Amesema hata BoT haijatangaza kutozitambua senti .ila kinachotokea nguvu ya soko katika kununua huduma na bidhaa imefanya sarafu hiyo kutokuwa na sifa.

No comments: