Monday, October 30, 2017

WALIMU 10 WASTAAFU SIMANJIRO WAPATIWA MABATI 200

Chama cha walimu Tanzania (CWT) Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, kimewakabidhi walimu 10 wastaafu hundi ya sh3.4 milioni kwa ajili ya ununuzi wa mabati 200. 

Mwenyekiti wa CWT Wilayani Simanjiro mwalimu Abraham Kisimbi aliyasema hayo wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa chama hicho uliofanyika mji mdogo wa Orkesumet. Mwalimu Kisimbi alisema lengo la kuwapa mabati hayo ni kuwawezesha walimu hao wastaafu wajenge nyumba zao baada ya kumaliza utumishi wao serikalini. 

Alisema wamewapa walimu hao wastaafu 10 mabati 200 ambapo kila mmoja atapata mabati 20 yatakayowasaidia kuezeka nyumba zao watakazojenga na kuanza maisha yao ya ustaafu. "Tumeona badala ya kuwapa mabati na kuhangaika kusafirisha kila mmoja tumempa hundi ya sh340,000 ili akanunue mabati 20 kule anapoishi," alisema mwalimu Kisimbi. 

Aliwataka walimu hao kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyopangwa ili wakafanikishe maisha yao kipindi hiki ambacho watakuwa wamestaafu kazi zao za ualimu na kuanza maisha mengine. 

Mwalimu Nazama Tarimo akisoma risala ya CWT alisema wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo walimu kutopandishwa madaraja na kutolipwa madai yao. Mwalimu Tarimo alisema kutembelea umbali mrefu na msongamano wa wanafunzi madarasani kunasababisha walimu kushindwa kufikia asilimia 80 ya ufaulu kwa wanafunzi wa eneo hilo. 

Alisema walimu wa mijini na vijijini wanatakiwa kupatiwa mtaala mmoja ili kuwawezesha kutoa elimu bora kwa wanafunzi wao. Mwalimu mstaafu Peter Toima ambaye pia ni Mwenyekiti Mtendaji wa shirika lisilo la kiserikali la ECLAT alisema kwa kutambua thamani ya elimu ameiunga mkono serikali kwa kukarabati, kukarafati na kujenga madarasa mapya kwenye shule mbalimbali. 

Toima alisema kupitia shirika lake la ECLAT wamewezesha uanzishwaji wa shule ya kwanza yenye kidato cha tano na cha sita, pekee wilayani humo ya Emboreet. Alisema wamekuwa wanaiunga mkono serikali kwenye ujenzi wa miundombinu ya majengo ya madarasa ya shule ili serikali iwezesha walimu na vitabu. 
 Mwalimu mstaafu na Mwenyekiti Mtendaji wa shirika lisilo la kiserikali la ECLAT Peter Toima akizungumza kwenye mkutano mkuu wa walimu wa Simanjiro juu ya mipango na mikakati mbalimbali ya shirika lake ya ujenzi wa baadhi ya shule za wilaya hiyo. 
 Mwenyekiti wa Chama cha walimu Tanzania (CWT) mwalimu Abraham Kisimbi akizungumza juu ya changamoto mbalimbali zinazowakabili walimu wa wilaya hiyo.

Mwenyekiti wa Chama cha walimu Tanzania (CWT) Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara mwalimu Abraham Kisimbi akizungumza juu ya Chama hicho kuwapatia walimu 10 wastaafu hundi ya shilingi milioni 3.4 kwa ajili ya ununuzi wa mabati 200 kwenye mkutano mkuu wa walimu wa wilaya hiyo. 

No comments: