Monday, October 30, 2017

Ni Wakenya Rock City Marathon 2017

 Abrahamu Too kutoka Kenya ameibuka mshindi wa kwanza kwenye mbio za km 42 Rock City Marathon zilizofanyika jijini Mwanza jana baada ya kumaliza kwa muda wa saa 02:22:45, akifuatiwa kwa karibu na mshiriki mwenzake kutoka nchini humo Moris Motima aliyetumia muda wa saa 02:23:19

Kivutio katika mbio hizo ilikuwa ni Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza ambae mbali na kuzindua mbio hizo pia alishiriki katika mbio za km 3 akiambatana na viongozi wengine wa serikali.

Nafasi ya tatu katika mbio hizo pia ilichukuliwa Mkenya George Onyacha aliyetumia muda wa saa 02:23:27, ikiwa sekunde chache nyuma ya mpinzani wake.

Katika mbio hizo zilizoanzia na kuhitimishwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini humo ilishuhudiwa nafasi ya kwanza hadi ya saba zikishikwa na wakimbiaji kutoka nchini Kenya huku nafasi ya nane ikienda kwa Mtanzania Paschal Mombo alietumia muda wa saa 02:30:43.

Akizungumzia siri ya ushindi wake, mbali na kusifia uratibu mzuri wa mbio hizo uliomuwezesha kukimbia bila changamoto yoyote Too alisema ni kujituma kufanya zaidi mazoezi na kukaa kambini muda mrefu ili kufanya vizuri katika michuano ya mwaka huu.

“Maandalizi ya mwaka huu ni mazuri na washiriki wameendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka jambo linalotufanya wanariadha kujiwekea mikakati mizuri ili kuweza kukabiliana na ushindani mkali uliopo katika mbio hizi na ninashukuru Mungu nimefanikiwa,” alisema.

Upande wa wanawake mshindi wa kwanza ni Mkenya Alice Gradys Otero aliyetumia muda wa saa 02:48:18 akifuatiwa na Mkenya mwenzie Tecla Chebet  aliyetumia saa 02:54:28 huku nafasi ya tatu ikishikwa na Mkenya Flavious Kwamboka alietumia muda wa saa 02:57:32.
Mtanzania Brabuelia Bryton kutoka mkoani Moshi alishika nafasi ya sita kwa upande wa wanawake katika mbio hizo akitumia saa 03:14:41

Washindi wa kwanza katika mbio hizo zilizofanyika kwa mara ya nane jijini humo  waliibuka na kitita cha Sh 4 milioni kila mmoja, washindi wa pili Sh 2 mil na washindi watatu Sh Mil 1.

Kwa upande wa mbio za km 21 Peter Limo kutoka Kenya aliibuka mshindi wa kwanza baada ya kumaliza kwa muda wa saa 01:05:24, akifuatiwa kwa karibu na mshiriki mwenzake kutoka nchini humo George Wayaki aliyetumia muda wa saa 01:05:50

Nafasi ya tatu katika mbio hizo pia ilichukuliwa Mtanzania Chacha Boy aliyetumia muda wa saa 01:05:59, ikiwa sekunde tisa tu nyuma ya mpinzani wake.

Upande wa wanawake mshindi wa kwanza ni Mkenya Dorifin Omare aliyetumia muda wa saa 01:17:12 akifuatiwa na Mkenya mwenzie Alice Mogiare aliyetumia saa 01:18:30 huku nafasi ya tatu ikishikwa na Mkenya Maiselina Issa alietumia muda wa saa 01:19:55.

Mtanzania Siatha Romanus kutoka mkoani Arusha alishika nafasi ya sita kwa upande wa wanawake katika mbio hizo akitumia saa 01:25:58
Katika mashindano hayo ilishuhudiwa washiriki ambao pia ni wadhamini wa mbio hizo kutoka  makampuni ya PUMA, Tiper, NSSF, RedBull,  Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), New Mwanza Hotel, EF Out door, CF Hospital, KK Security, na kampuni ya uchapishaji ya SDS wakishiriki kikamilifu katika mbio za KM 5 sambamba na watu wenye ulemavu wa ngozi yaani Albino.

Akizungumza kabla ya kukabidhi zawadi kwa washindi, Naibu Waziri Shonza alisema aliwapongeza washiriki na waandaaji wa mbio hizo na kutoa wito kwa wadau mbalimbali kushirikiana kwa pamoja ili kurejesha hadhi ya mchezo wa riadha nchini.

“Tanzania inaweza kurejea katika ramani ya dunia kwenye michezo kama tukijikita katika maandalizi mazuri ya kuibua na kuviendeleza vipaji vya vijana wetu nchini hasa kuanzia ngazi ya shule za msingi.” Alisema.

Naye Rais wa Shirikisho la riadha nchini (RT) ambae pia ni Mkuu wa mkoa wa Simiyu Bw Anthony Mtaka mbali  mbali na kuwapongeza waandaaji wa mbio hizo alisema licha ya wingi wa washiriki kutoka ndani ya nchi bado taifa linakabiliwa na uhaba wa wanaridha wa mbio ndefu yaani km 42 na wachache wanaofanya vizuri kwenye mbio hizo wamekuwa wakishindwa kushiriki mbio kama hizo zinazofanyika ndani ya nchini.

Abrahamu Too kutoka Kenya akimaliza katika nafasi ya kwanza kwenye mbio za km 42 Rock City Marathon zilizofanyika jijini Mwanza jana baada ya kumaliza kwa muda wa saa 02:22:45, akifuatiwa kwa karibu na mshiriki mwenzake kutoka nchini humo Moris Motima aliyetumia muda wa saa 02:23:19.

 Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kuzindua mbio za Rock City Marathon zilizofanyika jijini Mwanza jana  ambapo alikimbia mbio za km 3 akiambatana na viongozi wengine wa serikali.
 Baada ya uzinduzi kazi ikaanza!
 Mbali na kuzindua mbio hizo pia Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza (wa pili kulia)alishiriki kikamilifu katika mbio mbio za km 3 akiambatana na viongozi wengine wa serikali.

 Mbali na washiriki kutoka ndani ya nchin pia pia washiriki kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo China na Marekani nao hawakuwa nyuma.

Rais wa Shirikisho la riadha nchini (RT) ambae pia ni Mkuu wa mkoa wa Simiyu Bw Anthony Mtaka akizungumza kwenye warsha ya kukabidhi zawadi kwa washindi ambapo pamoja na mambo mengine aliwapongeza waandaaji wa mbio hizo kampuni ya Capital Plus Internantional (CPI).


Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza ( katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washindi wa kwanza hadi wa tatu wa mbio za Km 42 (waliosimama nyuma) mara baada ya kuwakabidhi zawadi pamoja na medali. Wengine ni pamoja na Rais wa Shirikisho la riadha nchini (RT) ambae pia ni Mkuu wa mkoa wa Simiyu Bw Anthony Mtaka(wa tatu kushoto), waandaaji pamoja na viongozi wa mchezo huo.

 Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza (Kushoto) akikabidhi zawadi kwa washindi wa mbio za Km 42 kwa upande wa wanawake ambapo washindi wa kwanza hadi watano wote walitoka nchini Kenya.
 Naibu Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Bi Juliana Shonza (Kushoto) akikabidhi zawadi kwa washindi wa mbio za Km 5 ambazo zilikuwa mahususi kwa washiriki wenye ulemavu wa ngozi pamoja na washiriki kutoka kwenye mashirika mbalimbali (corporate race)
Meneja Mahusiano Mkuu wa Kampuni ya kuhifadhi mafuta nchini Tiper, Bw Emanuel Kondi (kulia) akikabidhi zawadi kwa mmoja wa washindi wa mbio hizo. Kampuni ya Tiper ni moja ya wadhamini wakubwa wa mbio hizo ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo kuisaidia Serikali kutangaza utalii kupitia michezo pamoja na kuinua ya michezo kupitia riadha.

 Baadhi ya washindi wa mbio hizo, waandaaji na viongozi wa mchezo wa Riadha wakiwa kwenye picha ya pamoja na Meneja Huduma kwa wateja Kanda ya Ziwa kutoka  kampuni ya ndege ya Precision Air, Bi Isabella Mwalwiba mara baada ya kukabidhiwa zawadi zao. Kampuni ya Precision ni miongoni mwa wadhamini wakubwa wa mbio hizo.
 Baadhi ya washindi wa mbio hizo wakipokea zawadi zao kutoka kwa muwakilishi wa kampuni ya CF Hospital ya jijini Mwanza.zawadi zao. CF Hospital ni miongoni mwa wadhamini  wa mbio hizo.
 Baadhi ya washindi wa mbio hizo, waandaaji na viongozi wa mchezo wa Riadha wakiwa kwenye picha ya pamoja na Meneja Kanda  wa  kampuni ya Ulinzi ya KK Security, Bi Levina Vedasto  mara baada ya kukabidhiwa zawadi zao. Kampuni ya KK Security ni miongoni mwa wadhamini wakubwa wa mbio hizo ambapo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi waliwahakikishia washiriki uwepo wa ulinzi na Usalama.
 Baadhi ya washiriki kutoka ndani na nje ya nchi wakifurahia medali zao!

Baada ya ushindi ilikuwa ni furaha tupu!  

No comments: