Tuesday, September 5, 2017

China na Tanzania kuongeza Nguvu katika kupunguza Umaskini Nchini


Na Adili Mhina.


Taasisi ya Kimataifa ya Kupunguza Umaskini China (IPRCC) imeahidi kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano baina yake na Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Tume ya Mipango kwa lengo la kuongeza kasi ya maendeleo na kupunguza umaskini nchini.

Uamuzi huo umefikiwa katika kikao cha wataalamu kutoka Wiraza ya Fedha na Mipango kupitia Tume ya Mipango wakiongozwa na Kaimu Katibu Mtendaji Bw. Maduka Kessy na ujumbe kutoka taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika kikao hicho kiongozi wa ujumbe kutoka China Bw. Xia Gengsheng alieleza kuwa maeneo mapya yanayotarajiwa ni pamoja na kuanzisha vituo vingingine vya mfano vya kilimo katika vijiji mbalimbali hapa nchini.

Bw. Xia alieleza kuwa wameamua kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano kutokana na mafanikio yaliyojitokeza katika juhudi za kupambana na umaskini nchini hususan katika kutoa elimu ya kilimo kwa wakulima kupitia kuanzishwa kwa Kijiji cha mfano cha Peapea Wilayani Kilosa Mkoani Morogoro.

“Ndugu Kaimu Katibu Mtendaji naomba nikuhakikishie kwamba tutaanzisha vijiji vingine vya mfano kama kile cha Peapea na kutoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kujifunza mbinu bora za kilimo ili waweze kuendesha kilimo chenye tija na waondokane na umaskini,” alieleza Bw. Xia.

Eneo jingine la ushirikiano litakalo anzishwa ni masuala ya utafiti ambapo IPRCC kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Tume ya Mipango na taasisi zingine itawezesha kufanyika kwa tafifi katika kuchochea maendeleo na kutafuta mbinu mbalimbali za kupunguza kasi ya umaskini.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Bw. Maduka Kessy alieleza kuwa ushirikiano kati ya Tume ya Mipango na Taasisi ya IPRCC ambao umedumu kwa zaidi ya miaka sita umekuwa na faida kubwa katika kukabiliana na umaskini kwa watanzania.

Alielezea kuwa kwa kipindi hicho Tume ya Mipango na IPRCC wamefanikiwa kuendesha programu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuratibu mazungumzo ya kisera juu ya mageuzi ya kilimo vijijini na kupunguza umaskini, kuanzishwa kwa kituo cha mfano katika kupunguza umaskini kwa wakulima wadogo Kilosa Mkoani morogoro.

Aliongeza kuwa ushirikiano kati ya Tume ya Mipango na IPRCC umefanikisha uratibu wa programu za kuwajengea uwezo watanzania kwa kutoa udhamini wa masomo katika ngazi za uzamili na uzamivu katika fani za maendeleo vijijini pamoja na kuandaa mafunzo mbalimbali yanayohusu mageuzi ya kilimo kwa maafisa kilimo pamoja na wakulima wenyewe.

Pamoja na mambo mengine, Taasisi ya Kimataifa ya Kupunguza Umaskini ya China imekuwa ikisaidia kutoa msaada wa kitaaalamu ambapo wataalamu wa kilimo kutoka China wamekuwa wakitoa mafuzo kwa wakulima mkoani Morogoro.
Kaimu Katibu Mtendaji, Wizara ya Fedha na Mipango – Tume ya Mipango Bw. Maduka Kessy (wa tatu kutoka kushoto, mwenye tai nyekundu) na kiongozi wa ujumbe kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kupunguza Umaskini China, Bw. Xia Gengsheng (wanne kutoka kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na wataalamu kutoka China na viongozi wa Tume ya Mipango.
Wataalamu kutoa Tume ya Mipango wakiwa katika kikao na Ujumbe kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kupunguza Umaskini China (hawapo pichani).
Ujumbe kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kupunguza Umaskini China wakiwa katika kikao na wataalamu wa Wizara ya Fedha na Mipango – Tume ya Mipango (hawapo pichani) katika ofisi za Tume ya Mipango, jijini Dar es Salaam.
Kaimu Katibu Mtendaji, Wizara ya Fedha na Mipango – Tume ya Mipango Bw. Maduka Kessy (katikati), Naibu Katibu Mtendaji, Klasta ya Biashara za Kimataifa na Mahusiano ya Uchumi Bw. Paul Sangawe (kulia) na Kaimu Naibu Katibu Mtendaji anayesimamia Klasta ya Huduma za Jamii na Idai ya Watu, Tume ya Mipango, Bw. Ibrahim Kalengo (kushoto) wakimsikiliza mjumbe (hayupo pichani) kutoka China wakatika wa kikao.

No comments: