Tuesday, September 5, 2017

HomeMCHANGANYIKOBIASHARATECHNOLOJIABURUDANIMICHEZOSIASAMAGAZETITV Latest News KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI,YATEMBELEA HIFADHI YA MAZINGIRA ASILIA ULUGURU NA JUMUIYA YA WANYAMAPORI YA WAMI MBIKI Home / MCHANGANYIKO / WANUFAIKA WA TASAF WAPANDE MIKOROSHO KUTUNZA MAZINGIRA NA KUJIONGEZEA KIPATO; RC NCHIMBI WANUFAIKA WA TASAF WAPANDE MIKOROSHO KUTUNZA MAZINGIRA NA KUJIONGEZEA KIPATO; RC NCHIMBI

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi akizungumza na wasimamizi wa miradi ya kutoa ajira za muda kwa wanufaika wa mpango wa Tasaf kutoka halmashauri na manispaa ya Singida wakati akifungua mafunzo ya uwezeshaji wa kusimamia miradi hiyo.
Wasimamizi wa miradi ya kutoa ajira za muda kwa wanufaika wa mpango wa Tasaf kutoka halmashauri na manispaa ya Singida wakimsikiliza kwa makini Mkuu wa Mkoa wa Singida (hayupo pichani) wakati akifungua mafunzo ya uwezeshaji wa kusimamia miradi hiyo.
Mratibu wa Tasaf Mkoa wa Singida Patrick Girigo Kasango akiwa na Afisa Ufuatiliaji kutoka Tasaf Sinith Haule wakifurahia jambo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uwezeshaji wa kusimamia miradi ya ajira za muda kwa wasimamizi wa kutoka halmashauri na manispaa ya Singida.
Ramadhani Alute kutoka kata ya Minga manispaa ya Singida akiandika baadhi ya mambo katika mafunzo ya uwezeshaji wa kusimamia miradi ya ajira za muda kwa wasimamizi wa kutoka halmashauri na manispaa ya Singida.


…………….

Wanufaika wa mpango wa Kunusuru kaya masikini Tasaf, Mkoa wa Singida wametakiwa kupanda mikorosho ili waweze kutunza mazingira pamoja na kujiongezea kipato kutokana na zao la korosho.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi ametoa rai hiyo wakati akifungua mafunzo ya uwezeshaji kwa wasimamizi 67 wa miradi ya kutoa ajira za muda kwa wanufaika wa mpango wa Tasaf kutoka halmashauri na manispaa ya Singida.

Dkt Nchimbi amesema kutokana na kuwa ajira za muda kwa awamu hii zimelenga katika utunzaji wa mazingira kwa kupanda miti hivyo amewataka Tasaf mkoa wa Singida kuwasiliana na Bodi ya Korosho waweze kupatiwa mbegu ili isipandwe miti mingine bali mikorosho.

Amesema kwa kufanya hivyo mkoa wa Singida utaweza kuwa mzalishaji mkubwa wa Korosho huku ajira hiyo ya muda ya kutunza mazingira kwa kupanda mikorosho, ikiwa imewatengenezea wanufaika hao ajira yao ya kudumu.

“Tukiweza kupanda mikorosho kwa zoezi hili la ajira za muda baada ya muda wanufaika hawa wataweza kuwa na kipato kikubwa kwa kuweza kuuza korosho zao, hii itakuwa ndio maana halisi ya mpango wa kunusuru kaya masikini ambapo zinatakiwa pia zishiriki katika kukuza uchumi”, amesema na kuongeza kuwa,

“Katika kuelekea Tanzania ya uchumi wa kati wa viwanda haimaanishi kila mtu afungue kiwanda bali kila mwananchi asiachwe nyuma katika kufanikisha uwepo wa viwanda, kwa maana hiyo hawa wanufaika watasaidia uwepo wa viwanda kutokana na malighafi ya korosho watakayoilima”, amefafanua.

Dkt Nchimbi ameongeza kuwa miradi ya ajira za muda itafanikiwa endapo itaweza kuwajengea uwezo wanufaika hao wa kutambua fursa za kujiajiri na sio kupokea fedha na kuzitumia kisha kurudi katika umasikini ule ule.

Aidha amewataka watumishi wa umma wasiwafundishe wanufaika hao kulalamika kuwa fedha ni ndogo kama ambavyo wao wamekuwa wakilalamikia mishahara, bali wajifunze kwa wanufaika ambao wameweza kuanzisha miradi kama ufugaji kuku, kilimo cha bustani kutokana na fedha ndogo wanayopata.

Kwa upande wake Mratibu wa Tasaf Mkoa wa Singida Patrick Girigo Kasango amesema mpango wa ajira za muda kupitia Tasaf unafanyika katika halmashauri nne kati ya saba kwa Mkoa wa Singida ambazo ni halmashauri ya Singida, manispaa ya Singida, Malakama na Iramba.

Kasango amesema kwa awamu hii ajira za muda zimelenga katika kutunza mazingira kwa kupanda miti, kutengeneza mabwawa ya maji na kuzuia mmomonyoko wa udongo.

Ameongeza kuwa ajira hizo hufanyika kipindi ambacho si cha kilimo pia wanufaika hao watafanya kazi kwa muda wa masaa manne kwa muda wa siku sitini ambapo watakuwa wanalipwa kiasi cha shilingi 2300 kwa masaa hayo.

Girigo amesema wasimamizi 27 kwa Manispaa ya Singida, 40 halmashauri ya Singida, 41 Mkalama na 42 Iramba watapewa mafunzo kwa siku sita pamoja na mafunzo kwa vitendo yatakayowawezesha kusimamia vema ajira za muda.

Naye mmoja wa washiriki amesema mara baada ya mafunzo hayo wasimamizi hao wakatoe mafunzo kwa wanufaika waweze kutumia fursa ya ajira za muda na fedha watazopata kwa kujiendeleza kiuchumi.

Ramadhani Alute kutoka kata ya Minga manispaa ya Singida amesema watajitahidi kuwaelekeza vizuri wanufaika hao ili wasizitumie vibaya fedha hizo bali wawekeze hicho watakachopata kwa manufaa ya baadaye.

No comments: