Tuesday, May 16, 2017

Mkurugenzi wa Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani aendelea kutoa elimu ya mpiga kura

Hussein Makame, NEC-aliyekuwa Dodoma 

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema kuwa kura zilizoharibika zinazopatikana kwenye chaguzi zinasababishwa na wapiga kura wengi kukosa elimu ya mpiga kura.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume hiyo Bw. Kailima Ramadhani wakati akijibu swali la mmoja wa watangazaji wa kituo cha Redio AFM cha mkoani Dodoma katika mfululizo wa kutoa elimu ya mpiga kura kupitia vituo vya redio.

Mtangazaji huyo alihoji kwa nini inajitokeza unapotokea uchaguzi kunakuwa na kura zisizo halili au kura zilizoharibika wakati Tume imekuwa ikitoa elimu ya mpiga kura katika chaguzi zilizopita.

Bw. Kailima alijibu kuwa kinachosababisha hali hiyo ni ukosefu wa elimu ya mpiga kura kwa wananchi, na ndio maana Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi iliona umuhimu wa kutoa elimu hiyo katika kipindi chote cha mwaka.

“Mkurugenzi tusalie hapo kwenye kura halali na zilizoharibika, elimu hii umekuwa ukiitoa maeneo mbalimbali na leo tuko hapa AFM, kwa nini hadi leo tunakuwa na kura zilizoharibika na kura zisizo halali” alihoji.

Akijibu swali hilo, Bw. Kailima alisema ukosefu wa elimu ya mpiga kura ndio unaosababisha hali hiyo na ndio maana Katiba iliona kuna umuhimu wa Tume kutoa elimu hiyo kwa muda wote bada ya kutoa wakati wa kipindi cha uchaguzi.

“Ukiendea kifungu cha 4C cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi kimesema Tume itatoa elimu ya mpiga kura.Lakini tumekuwa na tatizo la kutotoa elimu ya mpiga kura baada ya uchaguzi na imekuwa ikitolewa wakati wa uchaguzi baada ya uteuzi na wagombea wakiteuliwa leo kesho kampeni inaanza” alisema Bw. Kailima na kuongeza:

“Kama Tume na wadau wanaanza kutoa elimu ya mpiga kura katika kipindi hicho, sasa mpiga kura atazingatia kusikiliza kampeni za chama badala ya kusikiliza utaratibu mzima wa namna ya kupiga kura kama”

Alisema kwa kuwa Tume imeanza kutoa elimu ya mpiga kura katika kipindi chote cha mwaka itasaidia sana ifikapo uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 kura zilizoharibika zitakuwa chache sana.

Kuhusu kura kuharibika, Bw. Kailima alisema kura yoyote iliyowekwa alama ya vema kwenye eneo la mgombea itahesabika kuwa kura halali.

“Kwa mujibu wa muongozo na maelekezo yaliyotolewa na Tume kwa wasiamamizi wa uchaguzi, alama yoyote ikiwemo ya X itakayowekwa kwenye chumba cha picha ya mgombea au jina la chama cha mgombea au kwenye chumba cha wazi itakubalika kwamba ni alama halali” alisema.

Alifafanua kuwa karatasi ya kura itakataliwa iwapo haina muhuri wa kituo au itakuwa na kitu au alama inayomtambulisha mpiga kura na iwapo, haijawekwa alama inayotambuliwa kuwa ni halali.

Aliongeza kuwa karatasi ya kura itakayopigwa kwa mgombea aliyejitoa kwa mujibu wa Sheria za Uchaguzi au ikawekwa alama kwa mgombea zaidi ya mmoja na iwapo haina alama yoyote, itakataliwa.

Hata hivyo, Bw. Kailima aliongeza kuwa uamuzi wa uhalali wa kura kituoni utaamuliwa na msimamizi wa kituo iwapo atarijiridhisha kuwa kura imeharibika na haiwezi kuhesabiwa na ataikataa na haitahesabiwa.

Tume imeanza kutekeleza mpango wa kutoa elimu ya mpiga kura kupitia vituo vya redio za kijamii katika mikoa yote ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania ikiwa ni sehemu ya kutekeleza matakwa ya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi ya kutoa elimu ya mpiga kura muda wote.

 Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani (kulia) akisalimiana na Meneja Mkuu wa Redio AFM ya Dodoma Bw. Tatenda J. Nyawo baada ya kutoa elimu ya mpiga kura kupitia redio hiyo hivi karibuni.

No comments: