Tuesday, May 16, 2017

Mahakama yaamuru Halotel kulipa faini ya milioni 700.

Na Karama Kenyunko, blogu ya Jamii.

MKURUGENZI Mtendaji wa Kampuni ya Mawasiliano ya Viettel Tanzania ‘Halotel’, Do Manh Hong na wenzake nane wamehukumiwa kulipa faini ya zaidi ya milioni 700 baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka saba likiwemo la uhujumu uchumi.

Hukumu hiyo, imetolewa baada upande wa mashtaka kuomba kufanyia marekebisho hati ya mashtaka kwa kuondoa mashtaka matatu Kati ya kumi yaliyokuwa yakiwakabili.

Mashtaka mapya ni pamoja na kusimika mitambo ya mawasiliano bila kibali cha TCRA, kutumia mitambo ambayo haijathibitishwa na kuitia hasara Serikali na TCRA ya milioni 459.

Akisoma Hukumu hiyo, Hakimu Wilbard Mashauri amesema amewatia hatiani washtakiwa mwenyewe baada ya kukiri kutenda makosa yao

Kabla ya kuwasomea hukumu, Hakimu aliwauliza upande wa mashtaka kama walikuwa na lolote ambapo wakili, Johavenes Zacharias ameiomba mahakama kutoka adhabu stahiki kwa washtakiwa.

Naye Wakili wa utetezi, aliiomba mahakama kuwapa adhabu ndogo washtakiwa kwa kuwa hilo ni kosa lao la kwanza na wanafamilia zinazowategemea.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mashauri amewahukumu washtakiwa kulipa faini ya jumla ya faini ya milioni 700. 

Akifafanua adhabu hiyo, hakimu Mashauri amesema kila mshtakiwa anatakiwa kulipa faini ya milioni tano kwa kila shtaka linalomkabili na pia walipe milioni 459 kwa TCRA kwa hasara waliyoisababisha.

Ameongeza kuwa, ametoa adhabu hiyo ili iwe fundisho kwao na kwa wafanyabiashara wengine wanaohujumu uchumi.Ameongeza kuwa, watuhumiwa wamekuja nchini kuwekeza kwenye biashara na siyo kuhujumu mitambo ya nchini.

"Washtakiwa hawa ni wafanyabiashara na wamekuja kwa ajili ya kuwekeza, hivyo ili kuonyesha Tanzania ipo makini kwenye masuala ya uwekezaji lazima wafate sheria" amesema Mashauri.

Mbali ya Hong, watuhumiwa wengine ni Dilshad Ahmed (36), Rohail Yaqoob(47), Khalid Mahmood (59), Ashfaq Ahmad (38), Muhamad Aneess(48), Imtiaz Ammar (33) wote raia wa Pakistan na Ramesh Kandasamy (36) raia wa Sri-Lanka na Viettel Tanzania Limited.

Katika mashtaka yao wamedaiwa, kuwa kati ya Novemba 2016 na Februari 2017 Dar es Salaam walitengeneza mfumo wa kutumia huduma za mtandao kwa lengo la kukwepa kodi ya kupokea na kusambaza simu za kimataifa bila kibali cha TCRA.

Wanadaiwa kuwa katika kipindi hicho waliendesha hiyo mifumo ya kupokea na kusambaza simu za kimataifa bila ya kuwa na leseni.Pia inadaiwa kuwa Novemba 20, 2016 waliingiza vifaa vya kielektroniki bila ya kuwa na leseni. Pia katika tarehe isiyofahamika Novemba 2016 walisimika vifaa hivyo ikiwamo sim box yenye namba ya siri 1152000.8.n.t.n na Laptop mbili aina ya Dell bila ya kuwa na kibali cha TCRA.

Katika kipindi hicho, washtakiwa hao wanadaiwa kuunganisha vifaa hivyo na huduma za mitandao kwa lengo la kupokea na kusambaza mawasiliano bila ya kuthibitishwa na TCRA.

Kwa upande wa Kampuni ya Viettel Tanzania Limited na Do Hong wanadaiwa kati ya Novemba 2016 na Februari 2017 maeneo ya ofisi za Halotel Victoria Kinondoni walishindwa kuthibitisha taarifa iliyotolewa na Unex Company Ltd kwa lengo la kusajili lakini za simu 1000.

Washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuisababisha hasara TCRA na serikali ya Tanzania ya milioni 459.

Mpaka Michuzi blogu inaondoka katika viunga vya Mahakama, ni mkurugenzi pekee ndiye aliyelipa faini, huku watuhumiwa wengine wakiendelea kusota lupango.Mkurugenzi huyo amelipa jumla ya milioni 479 ambazo ni faini yake ya milioni 20 ambapo ni kwake yeye na kampuni na Viettel Tanzania Ltd. 
 Mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya simu ya Halotel, Do Manh Hong, kwenye tisheti ya kijani na wenzake ambao ni raia wa Pakistan na Sri Lanka wakirudishwa mahabusu baada ya kuhukumiwa kulipa faini zaidi ya milioni 700 baada ya kupatikana n hatia ya mashtaka saba likiwemo la uhujumu uchumi

No comments: