Wednesday, May 24, 2017

PROF. MBARAWA AITAKA BODI YA DMI KUBORESHA MIUNDOMBINU


Serikali imeitaka Bodi ya Chuo Cha Bahari Dar es Salaam (DMI), kuhakikisha inaboresha miundombinu ya chuo na kuzingatia miiko na kanuni za ufundishaji ili wanafunzi wanaohitimu chuoni hapo waweze kukidhi mahitaji ya soko.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, amesema hayo leo jijini Dar es salaam, wakati akizindua bodi hiyo na kusisitiza kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha majengo kwa kutangaza zabuni kwa uwazi ili kuepuka mianya ya rushwa.

“Hakikisheni mnakuwa na mpango madubuti wa kuboresha majengo ya chuo ili chuo kibaki na hadhi yake, lakini pia hakikisheni mntoa elimu bora kwa wanafunzi wanaokuja kusoma hapa ili waweze kupata misingi imara itakayowawezesha kuajiriwa ndani na nje ya nchi mara baada ya kuhitimu masomo yao”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Ameongeza kuwa Serikali ina uhitaji wa wataalam wengi kwenye masuala ya bahari hivyo ni wajibu wa bodi kusimamia chuo na kuhakikisha wataalam hao wanazalishwa kwa wingi chuoni hapo ili kukidhi mahitaji ya soko kitaifa na kimataifa.

Amewataka wakufunzi wa chuo hicho kuhakikisha wanatumia lugha nzuri kwenye ufundishaji ili kuwaweka wanafunzi karibu na kuhakikisha wanapata taaluma inayotakiwa kwani kuwepo kwa waalimu hao kunategemea kuwepo kwa wanafunzi.

“Ni lazima tufungue milango kwa wanafunzi sababu wapo wanaoelewa haraka na wanaoelewa taratibu, hivyo tukae nao muda mrefu ili kubaini changamoto zao lakini pia tuwe waangalifu juu ya matumizi ya lugha tunazotumia kwa wanafunzi wakati tunapofundisha”, amefafanua Prof. Mbarawa.

Kwa upande wake Mwenyekiti Mpya wa Bodi ya DMI, Kapteni Ernest Bupamba, amemuahidi Waziri huyo kuwa watafanya kazi ya kusimamia chuo hicho kwa juhudi zote na kwa maarifa yote ili chuo kizalishe wataalam wenye sifa kwenye sekta ya uchukuzi,

“Naahidi kushirikiana vyema na Wajumbe wezangu wa bodi, Menejimenti ya Chuo na watumishi katika utekelezaji wa majukumu ili kuleta tija’ amesisitiza Kapteni Bupamba.

Aidha, Mkuu wa Chuo hicho Dkt. Erick Massami amemuomba Waziri Mbarawa kukisaidia chuo hicho kuanza kutumia fedha za mfuko wa Usafirishaji ambazo zimekusanywa tangu mwaka 2013 bila kutumika ili fedha hizo zitumike kuzalisha wataalam wengi katika sekta ya usafiri wa majini.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amezindua bodi ya chuo ambayo iko chini ya uenyekiti wa Kapteni Ernest Bupamba na wajumbe wanne ambao ni Kapteni Andrew Matilya, Dkt. Mwamini Tulli, Bi Tumaini Silaa na Eng. Alfred Waryana.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

No comments: