Tuesday, March 28, 2017

MAAFISA MAENDELEO YA JAMII WA MIKOA WAJENGEWA WELEDI KUTOKOMEZA UKATILI DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO NCHINI

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jinsia Julius Mbilinyi akifungua Kikao Kazi cha Maafisa wa Maendeleo ya Jamii wa Mikoa (hawapo pichani) katika cha siku mbili kinachoanza leo katika Hotel ya Edema Mkoani Morogoro.
Katikati ni Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jinsia Julius Mbilinyi akiwa katika picha ya pamoja na Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Mikoa wanaohudhuria kikao kazi kuhusu utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika mkutano unaofanyika Hotel ya Edema Mkoani Morogoro.
Baadhi ya washiriki wa kikao kazi cha Maafisa Maendelo ya Jamaii wa Mikoa wakifuatilia maelezo ya wawezeshaji kuhusu utekelezaji wa Mpango Kazi wa taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika Hotel ya Edema, mkoani Morogoro.

………………….

Na erasto ching’oro- Msemaji: Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto leo imefungua kikao cha siku mbili cha Maafisa Maendeleo ya Jamii wa Mikoa kwa ajili ya kuwajengea uwezo kuhusu utekelezaji wa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Kuzuia na Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (2017-2022).

Akifungua kikao hicho, Mwakilishi wa Katibu Mkuu Bw. Julius Mbilinyi ambaye ni Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jinsia aliwashukuru Washirika wa Maendeleo katika kuhakikisha kuwa tatizo la ukatili dhidi ya wanawake na watoto linatokomezwa hapa nchini. Aliyataja mashirika haya kuwa ni pamoja na UN-WOMEN, Shirika la Idadi ya Watu Duniani (UNFPA), na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Haki na Ustawi wa Watoto (UNICEF).

Mgeni Rasimi Kaimu Mkurugenzi wa Jinsia, aliwapongeza Maafisa Maendeleo ya Jamii kwa shughuli mbalimbali ambazo wamekuwa wakizitekeleza katika maeneo yao ya kazi, juhudi ambazo zimekuwa na mchango katika kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto nchini. Alifafanua kwamba, baada ya mafunzo haya, maafisa hao wataendelea kutekeleza majukumu yao kikamilifu ili kupunguza ukatili kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2021/20122.

Wanawake na watoto wamekuwa wakifanyiwa ukatili kwa kisingizio cha mila na desturi. Aidha, mfumo dume umesababisha wanawake kutoshiriki kikamilifu katika maamuzi yanayohusu maendeleo yao, katika ngazi ya kitaifa, katika ngazi ya jamii na hata katika familia zao. Mara nyingi tumesikia wanawake na watoto wakipigwa, kubakwa na wakati mwingine kuuwawa na watu wa karibu. Vitendo hivi ni ukatili wa hali ya juu na vinaleta simanzi na madhara makubwa katika jamii yetu.

Akiongea na Maafisa Maendeleo wa Mikoa, Bw. Mbilinyi alieleza kuwa madhara ya vitendo vya ubaguzi, unyanyasaji na ukatili dhidi ya wanawake na watoto huwaathiri kiafya na kisaikolojia na kijamii ambapo uthoofisha ushiriki wa wanawake katika shughuli za maendeleo na hivyo kurudisha nyuma jitihada za kuiwezesha nchi yetu kuwa ya viwanda na uchumi wa kati. Wizara kwa kuzingatia changamoto hizo, imekuwa ikifanya juhudi za kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto, ikiwemo uandaaji wa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto.

Katika kuhakikisha kuwa Mpango Kazi huu unaeleweka na kutekelezwa ipasavyo Wizara imetoa mafunzo kuhusu Mpango huu kwa wadau mbalimbali. Mafunzo yaliyotolewa ni mwendelezo wa mafunzo yaliyotolewa kwa waratibu wa Madawati ya Jinsia kutoka katika Wizara, Idara zinazojitegemea na Wakala wa Serikali kuhusu Mpango kazi huo ili kuwezesha utekelezaji wake.

Kaimu Mkurugenzi wa maendeleo ya Jinsia amefafanua kuwa, Tafiti mbalimbali ikiwemo Taarifa ya Idadi ya Watu na Afya ya mwaka 2015-2016 inaonesha kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia bado vipo. Taarifa hii inaonyesha kuwa wanawake 4 kati ya 10 wamewahi kukumbana na ukatili wa kimwili tangu wakiwa na umri wa miaka 15. Taarifa hiyo inaonesha kuwa wanawake 2 kati ya 10 walikumbana na ukatili wa kimwili wakati utafiti huo ukifanyika. Ukatili wa kimwili unaongezeka kadri umri unavyoongezeka; asilimia 22 ya wanawake wenye umri wa miaka 15-19 wamewahi kukumbana na ukatili wa kimwili, ukilinganisha na asilimia 48% ya wanawake wenye umri wa miaka 40-49.

Akitoa nasaha zake Afisa Mendeleo ya Jamii wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Paul Shayo alieleza kuwa mafunzo haya yatawajengea umahiri, kuweza kutekeleza Mpango Kazi kwa ufanisi. Mbinu watakazopata zitakuwa mwongozo wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika jamii. Vile vile, amekiri kwamba, uzoefu na weledi utakaoupata kupitia mafunzo haya utawasaidia wahanga wa vitendo vya ukatili kupata huduma stahiki kwa kuwaunganisha na watoa huduma katika maeneo mbalimbali.

Mikoa ambayo itajumuishwa katika awamu ya pili ya mafunzo hayo ni Kagera, Mara, Kigoma na Katavi.

No comments: