Thursday, February 9, 2017

WAJUMBE KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI, MBUNGE WA SIMANJIRO NA MKUU WA MKOA WA ARUSHA WATEMBELEA MNADA WA PILI WA KIMATAIFA WA MADINI YA TANZANITE.

Teresia Mhagama na Zuena Msuya, Arusha
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo na Mbunge wa Simanjiro, James Millya wametembelea Kituo cha Jimolojia Arusha, unapofanyika Mnada wa Pili wa Kimataifa kwa madini ya Tanzanite ili kujionea jinsi mnada husika unavyoendeshwa.
Mnada huo wa kimataifa unaofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 9 hadi 12, Februari, 2017 unahudhuriwa na wanunuzi mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi na wauzaji kutoka ndani ya nchi.
Akitoa maelezo kuhusu  mnada huo, Mkurugenzi wa Kitengo cha Uthaminishaji Madini katika Wizara ya Nishati na Madini (TANSORT), Archard Kalugendo, alisema kuwa lengo la mnada huo ni kuhakikisha kuwa madini ya Tanzanite yanapata soko rasmi na Serikali kupata mapato yake stahiki.
Alisema kuwa minada ya madini inayofanyika ndani ya nchi inasaidia pia kudhibiti utoroshaji wa madini hayo nje ya nchi kwani wauzaji wa madini hayo wanakuwa na uhakika wa kupata wanunuzi wa Tanzanite wanaohudhuria minada hiyo.
“Hapa tumekaribisha  wanunuzi kutoka sehemu mbalimbali duniani na sisi kama Serikali tunasaidia kutathmini madini yaliyoletwa na wauzaji wa ndani ya nchi kwa kuangalia bei katika masoko mengine nje ya nchi na kutoa muongozo wa bei za madini husika ambayo itamsaidia mchimbaji katika kufanya mauzo,” alisema Kalugendo.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Arusha, baada ya kukagua mnada huo, aliishukuru Wizara ya Nishati na Madini kwa kuendesha mnada husika jijini Arusha na kusema kuwa hii itasaidia kuitangazia dunia kuwa madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania pekee na Serikali itaongeza mapato kupitia madini hayo.
Alitoa wito kwa wafanyabiasharawa madini ya Tanzanite kuweza kupeleka madini mengi zaidi katika mnada huo ili kuweza kuwa na wadau wengi zaidi na madini  hayo yatanunuliwa kwa uwazi ambao utaleta faida kwa Serikali na wananchi kwa ujumla.
Wajumbe wa Kamati, Mkuu wa Mkoa na Mbunge wa Simanjiro pia walipata fursa ya kuona shughuli mbalimbali zinazofanyika katika Kituo cha Jimolojia ikiwemo za kuchonga vinyago vinavyotokana na miamba mbalimbali na kuweka katika maumbo mbalimbali na pia kukata madini ya vito na kuyaweka katika maumbo ya kuvutia.
Mnada wa kwanza wa madini ya Tanzanite ulifanyika mwezi Agosti mwaka 2016 ambapo jumla ya gramu 318,033.17 na karati 3,274.70 za Tanzanite ziliuzwa na jumla ya kampuni 43 kutoka mataifa mbalimbali duniani zilihudhuria.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini waliotembelea mnada huo ni pamoja na Mhe. John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini (CHADEMA), Mhe. Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Mhe. Mwantakaje Juma Mbunge wa Bububu (CCM) na Mhe. Dunstan  Kitandula Mbunge wa Mkinga (CCM).




No comments: