Sunday, January 29, 2017

MTANDAO WA WADAU WA ASASI ZA KIRAIA UNAOTETEA MAREKEBISHO YA SHERIA NA SERA IHUSUYO USALAMA BARABARANI WAKUTANA NA WABUNGE

Mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera ihusuyo usalama barabarani Tanzania siku ya tarehe 26 na 27 Januari, 2017 wamefanikiwa kukaa na baadhi ya wabunge kutoka kamati ya mambo ya nje, Ulinzi na usalama, Katiba na sheria pamoja na miundo mbinu katika kikao kilichoongozwa chini ya mwenyekiti wake Mbunge wa Muheza Mheshimiwa Balozi Adadi Rajabu, pamoja walionyesha ushirikiano wao katika kuboresha usalama bararani kwa maendeleo ya Taifa letu.

Wajumbe wa kikao husika walipata nafasi ya kusikiliza mada mbalimbali kuhusiana na masuala ya usalama barabarani na hali ilivyo sasa, ambapo ilielezwa kuwa hali ilivyo kulingana na takwimu zinaonyesha kuwa takribani watu milioni 1.25 hufariki dunia kila mwaka kutokana na ajali za barabarani, aidha, watu milioni 20 hadi 50 hujeruhiwa na wengine hupata ulemavu wa kudumu wengi wao wakiwa ni vijana wenye nguvu kazi ya Taifa. Hii ni kutokana na takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) 2015.
Kwa upande waTanzania Bara, taarifa kutoka jeshi la polisi Kikosi cha Usalama Barabarani inaonyesha kwamba, kwa mwaka 2016 jumla ya watu 3,256 walipoteza maisha kutokana na ajali za barabarani. Katika vifo hivyo wanaume ni 2,580 na wanawake ni 676. Aidha kumekuwa na majeruhi 8,958 kati yao wanaume ni 6,470 na wanawake 2,488. Wakati vyombo vya moto vilivyoongoza katika ajali ni magari binafsi ambayo idadi yake 3,649 ikifuatiwa na pikipiki kwa idadi ya 2,544.

Kutokana na idadi kubwa ya vifo vinavyotokana na ajali za barabarani nchini, Mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera zinazohusu usalama barabarani Tanzania umeona umuhimu na kuchukulia jambo hili kulifanyia kazi kwa kina. Tafiti zinaonyesha kwamba asilimia 76 ya ajali zote zinatokana na vyanzo vya kibinadamu kama vile Ulevi, Mwendokasi, Uzembe, Uchovu, kupuuzia au kutokuwa makini uwapo barabarani na kutokutii sheria za Usalama Barabarani. Tuna amini matendo haya ya kibinaadamu yana dhibitika kisheria, hivyo basi tunaisihi serikali kuboresha sheria.
Kama wadau wa Usalama Barabarani, tunadhani kuna umuhimu wa sheria sasa kuboreshwa, na hivyo utashi wa kisiasa unatakiwa. Ndiyo maana tukaitisha majadiliano ya pamoja na Wabunge pamoja na wadau mbalimbali wa Usalama Barabarani ili kuona ni kwa namna gani tunaweza kuleta mabadiliko ya sheria kwa ufanisi na kwa haraka.

Wabunge waliohudhuri kikao hiki kwa ujumla wao, waliona umuhimu wa kuwa na mikakati ya kitaifa ya kupunguza ajali na walikiri kwa nia moja na kukubali kuunda Mtandao wa Wabunge wanaotetea usalama barabarani.

Maeneo ambayo tunayapa kipaumbele katika maboresho ya sheria ni kama haya yafuatayo: a) Matumizi ya mikanda; Sheria ya sasa ya Usalama barabarani inasema ni kosa kisheria kwa dereva na abiria anayekaa kiti cha mbele kutokufunga mkanda wakati wa safari lakini sheria hiyo hiyo haisemi chochote kwa abiria wanaokaa kiti cha nyuma.
Utafiti uliofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO) unasema kuwa iwapo ajali ikitokea madhara/athari kwa abiria wa kiti cha mbele itapungua kwa 50% na kwa abiria wa nyuma madhara yatapungua kwa 70%. Kanuni zilizotungwa na SUMATRA zinataka abiria wote wafunge mkanda ila kwa vile sheria mama (Road Traffic Act of 1973) ipo kimya katika eneo hili utekelezaji wa kanuni unakuwa mgumu.

Hivyo basi ni rai yetu sheria hiyo ibadilishwe na kuwataka abiria wote wanaokuwa katika chombo cha usafiri wa kibiashara au binafsi kufunga mkanda wakati wote wa safari. b) Matumizi sahihi ya kofia ngumu; Sheria ya sasa ya usalama barabarani inasema kuwa ni kosa kwa muendesha pikipiki kutokuvaa kofia ngumu wakati wa kuendesha chombo hicho. Lakini sheria hiyohiyo haisemi chochote kwa abiria anayepanda katika chombo hicho.

Vilevile pamoja na kuanisha kosa kwa dereva wa pikipiki kutokuvaa kofia ngumu lakini pia sheria haielezi ni jinsi gani kofia inatakiwa kuvaliwa na aina maalum ya kofia inayotakiwa kuvaliwa. Kwa mujibu wa Utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) unaonyesha kuwa iwapo ajali itatokea madhara yanayotokea kwa kutovaa kofia maalum na kwa usahihi ni makubwa sana ukilinganisha na kofia hiyo ikivaliwa kwa usahihi. Hivyo basi ukizingatia kuwa sasa hivi usafiri wa pikipiki umekuwa unatumika kwa kiasi kikubwa (public transport) hivyo ni rai yetu sheria hiyo ifanyiwe maboresho na kuweka kuwa ni sheria kwa mtu yoyote anayepanda pikipiki kuvaa kofia ngumu na kwa usahihi.

c) Ulevi: Sheria ya sasa ya usalama barabarani inasema kuwa itakuwa kosa kwa mtu yoyote kuendesha chombo cha moto akiwa na kiwango cha kilevi katika damu yake kinachozidi asilimia 0.08% katika mfumo wa mwili. Kiwango hiki ni kikubwa sana kikilinganishwa na tafiti zilizofanywa na Shirika la Afya Duniani na kupendekeza kiwango cha asilimia 0.05% kwa dereva aliyebobea (experienced driver) na asilimia 0.02% kwa dereva mchanga (young driver). Hivyo basi ni rai yetu kuwa sheria ifanyiwe marekebisho ili iendane na kiwango cha sasa cha kimataifa kilichofanyiwa utafiti.

d) Mwendo kasi (Speeding): Mwendokasi umeendelea kuwa sababu kubwa ya ajali zinazogharimu uhai wa watu wengi. Sheria yetu inayo mapungufu kadhaa pamoja na juhudi nyingi za Jeshi la Polisi na wadau wengine kutaka kudhibiti jambo hili limeendelea kuwa tatizo. Adhabu zisizokidhi wala kuleta hofu kwa maderava wasiotaka kutii zimeendelea kufifisha juhudi za kudhibiti tatizo hili.

Tunatoa wito kwa watunga sera kushirikiana zaidi na wadau kuuelimisha umma katika eneo la uhusiano wa adhabu zitokanazo na makosa ya usalama barabarani na ongezeko la ajali. Pia sheria kufanyiwa maboresho na kuangalia kwa upya mianya iliyopo.

TAMKO HILI LIMETOLEWA LEO NA MTANDAO WA WADAU KUTOKA ASASI ZA KIRAIA:
1. TAWLA
2. TAMWA
3. WLAC
4. TCRF
5. TLS
6. TMF
7. RSA
8. AMEND TANZANIA
9. SHIVYAWATA
10. TABOA &
11. SAFE SPEED FOUNDATION

No comments: