Tuesday, May 3, 2016

Ada ya Leseni za Madini sasa zaanza kupatikana kupitia SMS

Teresia Mhagama na Asteria Muhozya

Imeelezwa kuwa, Wizara ya Nishati na Madini imeendelea kurahisisha utoaji wa huduma za leseni za madini ambapo sasa  wamiliki wa Leseni hizo wanaweza  kupata taarifa za ada ya leseni kwa njia ya ujumbe wa simu (SMS).

 Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA katika Wizara ya Nishati na Madini, Francis Fungameza alisema kuwa ili mteja aweze kupata huduma hiyo anatakiwa kuandika neno MEM, ache nafasi , kisha aandike  Namba ya Leseni na kutuma kwenda 15341.

Fungameza alisema kuwa hizo ni habari njema kwa wamiliki wa leseni kwani sasa wataweza kupata  taarifa hizo kwa wakati na hivyo  kulipia ada za  leseni hizo kwa wakati.

Aidha Fungameza alisema kuwa Wizara imekuwa ikibuni njia mbalimbali ili kuhakikisha kuwa huduma za utoaji wa leseni za madini pamoja na taarifa mbalimbali kuhusu leseni hizo zinapatikana kwa urahisi na uharaka tofauti na ilivyokuwa hapo awali.

“Kwa mfano kwa sasa tayari kuna mfumo wa kielektroniki ujulikanao kama Online Mining Cadastre Transactional Portal (OMCTP) ambao unawawezesha wateja kufanya masuala mbalimbali ikiwemo kufanya malipo ya leseni na mrabaha, wateja waliosajiliwa kutuma maombi ya leseni, kuhakiki taarifa za leseni wanazomiliki na kutuma taarifa za utendaji kazi . 

Aliongeza kuwa Mfumo wa OMCTP pia unawawezesha wateja kupata taarifa mbalimbali za Sekta ya Madini zikiwamo ramani za kijiolojia na taarifa za migodi mikubwa.

Fungameza alieleza kuwa hapo awali,  mfumo wa utoaji leseni ulifanyika kwa njia ya mkono (manually) na ulitegemea utumaji wa karatasi (paperwork based) na hali hiyo ilichangia kuchelewesha utoaji leseni na kuongeza kuwa utoaji huo wa leseni ulitegemea hali ya mawasiliano kama ya telegram na rejesta.

“ Vilevile upimaji na uchoraji ramani za kijiolojia ulifanyika kwa njia ya mkono na ulitegemea umahiri wa mtu na mara nyingine makosa yalifanyika na kusababisha migogoro au waombaji kukosa leseni kwa sababu zisizo za msingi,” aliongeza Fungameza.

Anasema kuwa mfumo huo wa awali ulileta changamoto kwani Wizara ilikuwa na wakati mgumu kuhakikisha kuwa kumbukumbu za leseni zinatunzwa vizuri bila kupotea, pia kulikuwa na kazi ngumu ya kuchambua nyaraka za leseni kwa njia ya mkono (manually) ili kufuatilia uhai wa leseni, malipo ya ada na utendaji wa wamiliki wa leseni.

Aliongeza kuwa leseni nyingi hazikuweza kuchambuliwa na hali hiyo iliathiri ubora wa utendaji wa Wizara na pia kasi ya kuwahudumia wananchi ilikuwa ndogo.

Alisema kuwa mfumo wa kieletroniki unaotumika sasa katika leseni za madini unakuwa kama kituo kimoja (one-stop-centre) kinakachotumiwa na wadau wa Sekta ya Madini walio nchini na nje ya nchi kuweza kujipatia huduma za leseni bila kulazimika kusafiri kwenda kwenye ofisi ya Madini, pindi wanapokuwa wamesajiliwa ndani ya mfumo huo.

Alisema kuwa OMCTP ina faida mbalimbali ikiwemo,  kuongeza uwazi na kasi ya utoaji wa leseni za madini na Wateja kuingiza maombi ya leseni wao wenyewe hivyo kupunguza tatizo la mlundikano wa maombi kwenye ofisi za madini.

Aliongeza kuwa  Wateja na Serikali watakuwa na uhakika na maombi yote yatakayowasilishwa (yakiwamo maombi ya sihia (transfer), kuhuisha leseni na pia kuwa na uhakika na malipo yote yatakayofanywa kupitia mfumo wa OMCTP.

“ Kupitia mfumo huu, Wateja pia wanapata taarifa za leseni zao kila wakati na kujua wanapotakiwa kufanya malipo ya leseni au watakapotakiwa kutuma taarifa za utendaji kazi na pia kurarahisha mawasiliano  kati ya Wizara na wamimiki wa leseni,” alisema Fungameza.

Aidha alisema kuwa Wateja wataweza kuhuisha taarifa za leseni zao za madini kama vile anuani na namba za simu kupitia mfumo wa OMCTP pindi taarifa hizo zitakapobadilishwa.