Wednesday, September 10, 2014

IPTL, wengine wawili wamburuza Zitto mahakamani

 ·        Wadai fidia ya shilingi bilioni 500

Kampuni ya ufuaji umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na wadai wengine wawili wamefungua kesi ya madai katika Mahakama Kuu dhidi ya Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini, Bw. Zitto Kabwe na wengine wawili wakitaka kulipwa fidia ya Shilingi bilioni 500 kwa kashfa alizotoa kimaandishi dhidi yao.

Mbali na IPTL,  wengine waliofungua kesi hiyo mnamo tarehe 4, Septemba kupitia wakili Melchisedeck Lutema wa Asyla Attorneys na  Kay Felician Mwesiga wa Bulwark Associates Advocates, ni kampuni ya Pan Africa Power Solutions Tanzania Limited (PAP) na Mwenyekiti Mtendaji wa makampuni hayo mawili, Bw. Harbinder Sing Seth.

Wadai hao watatu, miongoni mwa mambo mengine wanahitaji malipo ya fedha kutoka kwa Bw. Kabwe na washtakiwa wengine watatu ambao ni mhariri wa gazeti la Raia Mwema, Kampuni ya Raia Mwema na kampuni ya Flint Graphics, kuwa kama fidia itokanayo na makala ya kuwachafua iliyochapishwa kwenye gazeti hilo, iliyosababishwa na washitakiwa hao.

Pamoja na hayo, pia wanahitaji tamko rasmi toka mahakamani kwamba makala iliyokuwa na kichwa cha habari "Fedha za IPTL ni Mali Ya Umma" iliyochapishwa katika kurasa wa 7 na 14 za gazeti la tarehe 13 Agosti, 2014 ilikuwa ni ya kupotosha na kuchafua kwa kudhamiria na kuhitaji washitakiwa kuomba radhi kwa kuandika na kuchapisha katika kurasa za mbele kichwa cha habari ya kuomba msamaha katika matoleo mawili mfululizo ya gazeti hilo.


Zaidi ya hayo, wadai waliiomba mahakama kuweka vizuizi vya kudumu kwa washitakiwa, watumishi wao, wafanyakazi, washirika, wawakilishi au watu wengine wowote wanaofanya kazi chini ya washitakiwa kwa uchapishaji, kuchapisha au kusababisha kuandika na kuchapishwa kwa makala yoyote ya kuwachafua.

Wadai walisema kuwa, IPTL waliingia mkataba na Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (Tanesco) kuwa umeme unaozalishwa na mdai utakuwa ukinunuliwa na kusambazwa na TANESCO kwa bei waliyokubaliana.

Inadaiwa kwamba, katika kurasa namba 7 na 14 za gazeti la Raia Mwema la mwezi Agosti 13, 2014, Mbunge wa Kigoma Kaskazini aliandika, wakati mshtakiwa wa pili,  wa tatu na wa nne walihariri, kuchapa na kusambaza makala ambayo ilikuwa ni ya uongo na yakuwachafua wadai.

Katika hati ya mashtaka, wadai walisema kuwa makala hiyo ilikuwa na maneno yafuatayo yaliyokuwa si ya ukweli na ya kuwachafua wanaodai; “Kwa mara nyingine, serikali kupitia viongozi wake akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wamedai kwamba kiasi cha Dola za Marekani milioni 250 zilizopaswa kuendelea kuwapo katika “Tegeta Escrow Account’ si mali ya serikali na hivyo si mali ya umma. Akaunti hiyo ilifunguliwa na serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) pamoja na kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).”
  
Ilidaiwa kuwa pasingekuwa na nia ya dhati ya kumchafua  mdai, mdaiwa hasingechapisha, na kusambaza maneno yaliyonukuliwa kama angefanya juhudi za kuthibitisha ukweli kutoka upande wa pili (kwa mdai) au kutoka kwa maafisa husika wa serikali ambao wangethibitisha kwamba:

“kiasi cha fedha kilichowekwa kwenye akaunti ya Escrow ilikuwa ni dola za kimarekani 122,000,000.00 na siyo dola za kimarekani 250,000,000.00 kama ilivyodaiwa na mshtakiwa,” ilisomeka sehemu ya hati ya madai.

Kwa mujibu wa wadai, Tanesco kamwe haikuwa sehemu ya makubaliano ya Escrow kama  ilivyodaiwa na washtakiwa.  “Fedha ziliwekwa katika makubaliano ya Escrow na siyo kama fedha za umma lakini ni kwa kutokana na mgogoro wa malipo yaliyotakiwa kufanywa na Tanesco kwa IPTL.

“Madai kuwa fedha hizo ziliwekwa kama fedha za umma ni za uongo za kuupotosha umma na kuwachafua wadai kuwa ni wabadhilifu wa fedha za umma”, sehemu ya hati ya madai ilisomeka. 

No comments: