Wednesday, November 14, 2012

MUCCoBS wauaga mwili wa mwanafunzi mwenzao aliyejinyonga

MWANAFUNZI wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Ushirika na Biashara cha Moshi (Muccobs),aliyejinyonga amesafishwa jana kuelekea Njombe mkoani Iringa kwa ajili ya maziko.

 Mwanafunzi huyo, Samson Mbena (24), alijinyonga usiku wa kuamkia jumapili ambapo Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz, alithibitishia kuhusu tukio hilo. 

 Kwa mujibu wa Kamanda Boaz,alisema uchunguzi wa kifo hicho bado unaendelea ili kubaini kiini cha kijana huyo kujinyonga. 

 Wakati wa uhai wake, kijana huyo alikuwa anasomea shahada ya sanaa katika Menejimenti ya Taasisi ndogo za fedha. Habari zilisema wananchi wa eneo la mwisho wa lami katika Kijiji cha Uru Timbirini, ndio waliougundua mwili wa mwanafunzi huyo ukining’inia juu ya mti. 

 Baadaye walitoa taarifa polisi na kufuatiwa na hatua ya askari kwenda katika eneo la tukio na kuushusha mwili na kisha kuupeleka chuoni ambako wanafunzi walimtambua mwanafunzi mwenzao. Habari zilisema baadaye, mwili wa marehemu ulipelekwa katika Hospitali ya Mawenzi, ambako umehifadhiwa ukisubiri kufanyiwa uchunguzi. 

 Hili ni tukio la pili kwa mwanafunzi wa Muccobs, kukutwa akiwa amekufa katika mazingira ya kutatanisha. 

 Oktoba mwaka juzi, mwanafunzi Lucy Genge (20) aliuawa kikatili baada ya kubakwa na kundi la watu wasiojulikana. 

 Maiti yake ilitupwa kwenye kichaka kidogo kilichokuwa umbali wa meta 100 kutoka katika Ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa Kilimanjaro na kugunduliwa na wapita njia saa 6:00 mchana. Marehemu ndio kwanza alikuwa amemaliza kozi ya cheti katika fani ya Utawala na Uhasibu.
 Mwanafunzi Samson Mbena (24), aliyejinyonga usiku wa kuamkia jumapili .
 Wanafunzi wa mwaka wa tatu katika chuo kikuu kishiriki cha ushirika na biashara(MUCCoBS)waliokuwa wakisoma na marehemu Sam,wakiwa katika mavazi ya maombolezo.wakati wa kuuga mwili wa mwenzao katika ukumbi wa Nyerere chuoni hapo.
 Wanafunzi wakijiandaa kuaga mwili wa marehemu Samson.
 Msaidizi wa makamu mkuu wa chuo,MUCCoBS ,Bw Ndainzera Manta akitoa heshima zake za mwisho
 Wanafunzi wakipita mbele ya jeneza kutoa heshima zao za mwisho.
 Baadhi ya wahadhiri wa chuo kikuu kishiriki cha ushirika na biashara,MUCCoBS wakifuatilia zoezi la kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa marehemu Samson.
 Baadhi ya wananfunzi walishindwa kujizuia.
 Safari ya kutoka ukumbini kupeleka jeneza kwenye gari ilianza.

Mwili ukiwa umeingizwa katika gari la Chuo cha MUCCoBS tayari kwa safari ya kuelekea Njombe mkoani Iringa. Habari na picha na Dixon Busagaga wa Globu yaJamii Moshi.

No comments: