Sunday, December 9, 2018

NITAENDELEA KUFANYA ZIARA ZA KUSTUKIZA KATIKA HOSPITALI NA VITUO VYA AFYA NYAKATI ZA USIKU MPAKA HUDUMA ZIIMARIKE - DC MURO

Na.Imma Msumba Arumeru

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe. Jerry Muro amefanya ziara ya kustukiza usiku wa manane katika Hospitali mbili za Wilaya na kujionea hali ya utoaji wa huduma za Afya nyakati za Usiku , ziara ambayo alianza saa Saba na nusu Usiku mpaka saa kumi na moja alfajiri.

Hatua ya Mhe Muro kufanya ziara ya kushtukiza nyakati za Usiku katika hospitali imekuja Kutokana na kuwepo Kwa malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi ambao wameonyeshwa kukerwa na huduma duni za Afya zinazotolewa nyakati za Usiku ikiwemo kutokuwepo Kwa wataalamu katika maeneo yao ya kazi kama inavyotakiwa Kwa mujibu wa sheria, Kanuni na taratibu.

Akiwa katika Hospitali ya Halmashauri ya wilaya (ARUSHA DC) Hospitali ya Oltrumet Mhe. Muro Alifika katika Eneo la mapokezi ambalo mbali na milango kuwa wazi pamoja na nyaraka na baadhi ya Madawa na vifaa tiba lakini hapakuwa na mtu yoyote katika eneo hilo na badala yake kazi ya mapokezi aliachiwa Askari mgambo anaelinda hospitali hiyo ambapo huwapokea wagonjwa na kisha kwenda KUWAAMSHA WAHUSIKA AMBAO MUDA MWINGI WANAKUWA Wamelala tukio ambalo limeshuhudiwa na Mhe Muro ambae alilazimika kwenda katika Hospitali hiyo akiwa na Usafiri Binafsi wa pikipiki na gari lingine la kawaida moja.

Pia Dc Muro alitembelea katika jengo la upasuaji na kukuta tukio la kukera ambapo wauguzi na wahusika wa chumba hicho walikuwa wamelala uku wamejifunika mablanketi hatua iliyomlazimu Mhe Muro kuwaamsha jambo ambalo liliwafanya wakimbie wakihisi wamevamiwa na Mzimu.

Pamoja na kuwepo Kwa changamoto hizo, Mhe Jerry Muro alioonyeshwa kufurahishwa na kitendo Cha muuguzi wa zamu katika jengo la kujifungulia kina mama ambae mbali na kuwa mwenyewe lakini alikuwa akitimiza wajibu wake wa kuendelea kuwahudumia kina mama ambao baadhi walikuwa katika hatua za kujifungua.

Baada ya kumaliza ziara katika Hospital ya Halmashauri ya Arusha ya Oltrumet Mhe Muro alitembelea hospital ya Halmashauri ya Meru ya Tengeru kujionea pia huduma za matibabu nyakati Za Usiku ambapo akiwa katika hospital hiyo aliwakuta baadhi ya wataalamu wakiwajibika ikiwemo muuguzi wa zamu katika eneo la mapokezi , pamoja na wauguzi wa wodi za kina mama , kina baba, watoto na pamoja na eneo la jengo la wazazi ambapo alikuta huduma zikiendelea kama kawaida uku Mganga wa zamu akiwa amelala, ambapo hata hivyo alikerwa na kitendo Cha kutokuwepo katika eneo la kazi kwa Dereva wa gari la wagonjwa ( Ambulance ) ambapo walitumia zaidi ya nusu saa kumtafuta pasipo kupatikana.

Wakizungumzia ziara hiyo ya aina yake , baadhi ya wagonjwa na ndugu waliokuwa wakipatiwa huduma katika Hospital hizo mbali na kupongeza hatua ya Mhe Muro kuzunguka usiku kujionea hali ya utoaji wa huduma wamesema kitendo hicho kitaisaidia kuwazindua wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi Kwa mazoea.

Mhe Muro amemaliza ziara yake kwa kutoa maelekezo kwa wakurugenzi wa Halmashauri za Meru na Arusha kuchukua hatua stahiki kwa watendaji wa sekta ya Afya ambao wamekuwa wakidumaza mfumo wa utoaji wa huduma za afya nyakati za Usiku na kuagiza kila mtu anaepaswa kuingia zamu ya Usiku anatakiwa kuwa katika eneo lake la kazi hata kama hakuna wananchi wanaofika kupata huduma kwa wakati huo.

Dc Muro amefafanua kuwa nyakati za Usiku matukio mengi ya dharura hutokea japo sio mara kwa mara lakini akawatahadharisha kuwa lazima watu wawe katika maeneo yao ya kazi ili kukabiliana na dharura hizo kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi .

Imetolewa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Arumeru
 Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe Jerry Muro Akizungumza na Waaguzi walikuwa zamu katika hospital ya Halmashauri ya Meru ( Tengeru) baada ya kufanya ziara yake ya kushtukiza usiku wa manane katika hospital hiyo.
 Dc Muro Akizungumza na moja ya wagonjwa walikuwa wamelazwa katika hospital ya Halmashauri ya Arusha Dc ( Oltrument) usiku wa kuamkia leo

 Dc Muro akipakua moja ya Nyaraka za Hospital ya Halmashauri ya Arusha Dc ( Oltrument ) alipozikuta katika chumba cha mapokezi kilichokuwa wazi na hapakuwa na mhudumu kwa muda huo.