Tuesday, December 18, 2018

MASHEIKH WA BAKWATA MIKOA YOTE NCHINI WAMPONGEZA MUFTI KWA KUWAUNGANISHA

*Ni kupitia kauli mbiu yake ya Jitambue,mabadilika,acha mazoea...Makonda atoa neno


Na Said Mwishehe,Globu ya jamii

MASHEIKH wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania( BAKWATA) katika mikoa yote ya Tanzania wamempongeza Sheikh Mkuu Aboubakary Zubeiry kutokanana namna ambavyo amejenga umoja na mshikamano ndani ya baraza hilo.

Wametoa kauli hiyo jana mbele ya Rais Dk.John Magufuli aliyekuwa mgeni rasmi kwenye sherehe za kutimiza miaka 50 ya BAKWATA tangu kuanzishwa kwake Desemba 17 mwaka 1968.Akizungumza kwa niaba ya masheikh wa mikoa, Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhad Mussa Salum amesema wanampongeza wanampongeza Muft Zubeiry kwa namna ambavyo amefanya mabadiliko makubwa ya kuwaunganisha Waislamu nchini.

"Wakati leo tunasheherekea miaka 50 tangu kuanzishwa kwa BAKWATA ,salamu za kipekee tunazipeleka kwa Mufti wa Tanzania kwani maadhimisho hayo yanamkuta yakiwa mikononi mwake."Chini ya Mufti wetu Sheikh Zubeiry BAKWATA imekuwa mpya,na walio chini yake tunapendana,tunaheshimiana na tunajitambua .Kupitia kauli mbiu yake ya Jitambue, Mabadilaka,Acha mazoea hakika imetusaidia kutubadilisha na kila mmoja wetu anajua majukumu yake," amesema Sheikh Alhad.

Amesisitiza kupitia Mufti wa Tanzania BAKWATA imeunganishwa na walio chini yake wamekuwa waaminifu na walio tayari kuhakikisha baraza hilo linasonga mbele kimaendeleo.Pia amesema kuwa BAKWATA kwa sasa wamekuwa na uhusiano mzuri na taasisi nyingine na chini ya Mufti Zubeiry kuna maendeleo makubwa yanaendelea kufanyika ukiwamo wa ujenzi wa msikiti mkubwa ambao unajengwa katika makao makuu ya baraza hilo jijini Dar es Salaam.

Wakati huo huo Sheikh Alhad alitumia nafasi hiyo kumkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Dar as Salaam Paul Makonda ambaye hakusita kuelezea mafaniko ambayo BAKWATA wameyapata kwa miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Amesema amefurahishwa na viongozi wa dini zote Mkoa wa Dar as Salaam ambavyo wanaishi kwa ushirikiano mkubwa huku kwa sehemu mkubwa wakijikita kuhimiza umoja,amani na mshikamano miongoni mwa wananchi wote.

"Nitumie fursa hii kulipongeza Baraza Kuu la Waislamu Tanzania kwa kutimiza miaka 50,nikupongeze Mufti kwa uongozi mzuri.Tunafahamu ujenzi wa msikiti mkubwa wa ghorofa tatu pale BAKWATA makao makuu unaendelea .Katika ule msikiti ghorofa ya tatu kutakuwa na ofisi yako,chumba cha kupumzika na chumba kikubwa cha kupokea wageni wako," amesema Makonda.

Ametumia nafasi hiyo pia kumpongeza Raid Magufuli kutokana na uzalendo wake kwaWatanzania ambapo kwa juhudi zake kuna miradi mkubwa ya maendeleo unaendelea nchini kwetu."Tunakushukuru Rais kwa kazi mkubwa na nzuri unayoifanya kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu."

No comments: