Wednesday, November 28, 2018

UJENZI WA RELI KIPANDE CHA PILI MOROGORO HADI MAKUTUPORA SINGIDA WASHIKA KASI

Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii Kilosa

ujenzi wa reli ya kisasa kwa kipande cha pili kuanzia eneo la Morogoro hadi Makutupora Singida, unazidi kushika kasi baada ya wakandarasi wa ujenzi wa reli hiyo kumaliza kazi muhimu.

Kazi hizo ni pamoja na uchukuaji wa sampuli za udongo, miamba kwenye milima itakayapasuliwa, kuchonga, kupasua na kujaza udongo kwenye njia za reli ya mwendokasi pamoja na kumalizia ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza mataluma ya reli.

Hayo yalibainika kwenye ziara ya maalumu iliyoandaliwa na kampuni ya Ador Tanzania kwa waandishi mbalimbali nchini, ili kujionea ufanyaji kazi wa ujenzi wa reli hiyo kuanzia Morogoro hadi Makutupora.

Ujenzi wa reli hiyo kwa kipande hicho, unajengwa na Kampuni ya Yepi Merkezi kwa gharama ya dola bilioni 2, ambapo Meneja Mradi huo katika Lot 2 inayotoka Morogoro Mpaka Makutupola, Dk. Husnis Uysa amesema wamekamimilisha mambo ya Msingi katika ujenzi huo.

Amesema tayari wameshaleta vifaa ambavyo zaidi ya magari 3,085, ambayo ipo katika eneo la mradi, huku pia kambi za mafundi na wafanyakazi kujengwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo Mkata, Kilosa na Makutupora.

"Malengo yetu ifikapo Januari mwakani au mwishoni mwa mwezi Desemba, kazi rasmi itaanza ya kuanza kuweka vifusi vya zege ili shughuli zingine za utandazaji wa reli uanze" amesema.

Dk. Husnis amesema reli hiyo yenye kilometa zaidi 422, itakuwa na vituo vya kisasa nane huku kati ya hizo vituo vikubwa vikiwa viwili, ambazo ni Kilosa, na Dodoma Mjini.Amesema licha ya kuwepo kwa vituo hivyo, ambavyo vitajengwa kulingana na tamaduni za kila eneo na uasili wake, pia maandalizi ya njia ya kupita reli hiyo chini ya milima tayari imeanza kufanya kazi."Tuna milima kama minne ambayo tutaichonga hasa katika eneo la Kilosa kwenye mto mkoandoa, ambapo kwa muda mrefu lilikuwa eneo korofi, ambapo sasa tutaipitisha reli hiyo chini ya mlima," amesema.

Vituo hivyo ni Mkata, Kilosa(itakuwa stesheni kubwa),Kidete, Igandu, Dodoma Mjini(ambapo kitakuwa stesheni kubwa), Bahi, Makutupora, ambazo zote zitajengwa kulingana na maeneo yao ya asili jinsi yalivyo.
Kwa mujibu wa Dk. Husnis, milima ya Kilosa, reli hiyo itajengwa kwenda chini kwa mita 30 hadi mita 90, huku ikitarajia kutembea chini ya ardhi kwa zaidi ya kilometa 2.7.

"Maandalizi yote ya mlima utakaopita treni tayari unajulikana na sasa tunaanza kupima miamba ya hapo ili tuweze kujua aina ya udongo uliopo kabla ya kuanza kuuchoronga," amesema.Kwa upande wake, Meneja mradi wa Stardand Gauge kipande cha Morogoro hadi Makutupora kwa upande wa Shirika la reli nchini(TRC), Injinia Faustin Kataraia alisema wanaendelea na usimamizi madhubuti.

Amesema mradi huo ni mkubwa na ndio maana kama TRC imejipanga kikamilifu kuwa pamoja na mkandarasi, ambapo sasa katika hatua zote za awali walikuwepo pamoja na wadau wengine."Tupo na mamlaka ya maji Morogoro, shirika la umeme nchini(TANESCO) na wadau wengine muhimu ambao kwa namna moja au nyingine hii stardand gauge ina wahusu kwa ukaribu zaidi,' amesema.

Aidha, amesema katika mradi wa pili wa ujenzi wa reli hiyo zaidi ya watanzania asilimia 79 wanashiriki kwenye ujenzi huo kwenye kazi mbalimbali sawa na wafanyakazi 1533 kati ya 1924 waliopo kwenye mradi huo.
Meneja mradi wa Standard Gauge kipande cha Morogoro hadi Makutupora kwa upande wa Shirika la reli nchini(TRC), Injinia Faustin Kataraia akiwaeleza Waandishi wa Habari namna mradi huo utakavyoungana na ule wa kutoka Dar mpaka Ngerengere.
Meneja Mradi wa SGR katika Lot 2 inayotoka Morogoro Mpaka Makutupola, Dk. Husnis Uysa akizungumza na Waandishi w ahabari juu ya hatua zilizochukuliwa katika kutekeleza Mradi huo. 
Sehemu ya Waandishi wa Habari waliotembelea mradi wa SGR Kutoka Morogoro mpaka Makutupora wakiangalia mashine ya kusagia kokoto
Sehemu ya Makandarasi wakiendelea na ujenzi wa tuta kutoka Morogoro mpaka Makutupora Singida.
Mtambo wa kusagia Kokoto ukiwa umefungw akatika moja ya vituo vya kazi katika tuta la Morogoro kama unavyoonekana.
Mashine ya kuchimba Miamba kwa ajili ya kukagua ubora wa Ardhi katika eneo ambalo Reli ya SGR itapita katika eneo la Mpwapwa. 

No comments: