Wednesday, November 21, 2018

Fanyeni kazi Kwa Bidii Huku Mkimtanguliza Mungu Mbele kwani Huduma Wanayoitoa Inagusa Uhai wa Watu – Prof. Mohamed Janabi

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni moja mfanyakazi bora wa robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2018/2019 Ramadhani Mpili wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu na kumpongeza mfanyakazi bora iliyofanyika leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo uliopo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi cheti cha kutambua utendaji wake wa kazi kwa kipindi chote cha utumishi wa Umma Afisa Muuguzi Mkuu Msaidizi Mstaafu Agnes Mtaki wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu na kumpongeza mfanyakazi bora iliyofanyika leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo uliopo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Huduma ya Uuguzi wa Taasisi hiyo hiyo Robert Mallya.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi ngao ya kutambua utendaji wake wa kazi mhudumu wa Afya Mwandamizi Mstaafu Magdalena Masanno wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu na kumpongeza mfanyakazi bora iliyofanyika leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo uliopo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Huduma ya Uuguzi wa Taasisi hiyo hiyo Robert Mallya.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akiwa katika picha ya pamoja na wastaafu Magdalena Masanno na Agnes Mtaki na baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi hiyo mara baada ya kumalizika kwa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu hao na kumpongeza mfanyakazi bora iliyofanyika leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo uliopo jijini Dar es Salaam.

Afisa Muuguzi Mkuu Msaidizi Mstaafu Agnes Mtaki na mhudumu wa Afya Mwandamizi Mstaafu Magdalena Masanno wakikata keki wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu hao na kumpongeza mfanyakazi bora iliyofanyika leo katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) . Kushoto ni Mkurugenzi wa Utawala na Fedha Agnes Kuhenga na kulia ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Huduma ya Uuguzi Robert Mallya. 



Picha na Genofeva Matemu – JKCI 

……………………… 

Na Mwandishi Maalum 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi amewataka wafanyakazi wa Taasisi hiyo kufanya kazi kwa bidii huku wakimtanguliza Mungu mbele kwani huduma wanayoitoa inagusa uhai wa watu. 

Prof. Janabi ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo ameyasema hayo leo wakati wa hafla fupi ya kuwaaga maafisa uuguzi wawili ambao wamestaafu kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa umma na kumpongeza mfanyakazi bora wa robo ya kwanza ya mwaka wa fedha wa Julai-Septemba 2018. 

Alisema kazi ya kuwahudumia wagonjwa siyo kazi rahisi sana kuna wakati wagonjwa wanakuwa wakali wao na ndugu zao jambo la muhimu ni kuwa wavumilivu na kuwahudumia kwa moyo wa upendo. 

“Leo hii tunawaaga wafanyakazi wenzetu ambao wanastaafu kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa umma, kazi waliyoifanya ni ngumu wanastahili pongezi. Mmoja amefanya kazi miaka 40 na mwingine miaka 35 katika kipindi chao chote walichokuwa kazini hawakuwahi kushtakiwa kwa utovu wa nidhamu”. 

“Jambo la muhimu kwetu sisi tunaobaki tuwaige mfano tujitahidi kuwahi kazini , tuwepo eneo la kazi na kufanya kazi muda wote wa kazi, tushirikiane na tuheshimiane kwa kufanya hivi tutaweza kutoa huduma bora kwa wagonjwa wetu wa moyo”, alisema Prof. Janabi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kurugezi ya Huduma ya Uuguzi Robert Mallya aliwasisitiza wauguzi hao wanaostaafu kwenda kuwahudumia wananchi pale itakapohitajika kufanya hivyo kwani taaluma yao iko palepale na jamii inahitaji kupata huduma yao . 

Akizungumza kwa niaba ya mstaafu mwenzake Afisa Muuguzi Mkuu Msaidizi Mama Agnes Mtaki aliwashukuru wafanyakazi hao kwa moyo wa upendo waliouonyesha katika kipindi chote walichofanya kazi pamoja katika Taasisi hiyo. 

Mama Mtaki alisema, “Jambo la muhimu ninalowahusia ni mfanye kazi kwa bidii huku wakimtanguliza Mungu mbele kwani huduma mnayoitoa ni ya kiroho. Kazi ya kuwahudumia wagonjwa inahitaji uvumilivu, unyenyekevu na ushirikiano”,. 

Alimalizia kwa kuwataka wafayakazi hao kuheshimu kazi wanayoifanya hii ikiwa ni pamoja na kuwahi kazini, kwani kuwa na kazi kumewafanya waheshimike, wasomeshe watoto na ndugu zao na kuweza kujikwamua kiuchumi. 

Wafanyakazi hao wastaafu walipewa zawadi ya mabati 100, mifuko 100 ya smenti, ngao, cheti cha kutambua kazi waliyoifanya kwa kipindi chote walichokuwa kazini pia walikabidhiwa fedha za nauli za kurudi nyumbani kwao waliko zaliwa ambako ndiko watakapokwenda kuishi. 

Mfanyakazi bora alipewa zawadi ya shilingi milioni moja, cheti cha kutambua kazi aliyoifanya na ngao kwa ajili ya kutoa hamasa kwa wafanyakazi wengine ili waendelee kufanya kazi kwa bidii na maarifa.

No comments: