Tuesday, November 6, 2018

BARAZA LA KILIMO TANZANIA LAENDELEA NA UJENZI NA UKARABATI WA MAGHALA MKOANI KATAVI.

ZAIDI ya wakulima 57,000 Mkoani Katavi wanatarajiwa kunufaika na mafunzo yatakayowasaidia kuongeza uzalishaji katika mazao yao, namna bora ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ikiwa ni pamoja na kujengewa uwezo wa namna ya upatikanaji wa masoko kwa mazao wanayolima.

Aidha pia imeelezwa kuwa ili kuendelea kuinua kiwango cha uzalishaji kwa wakulima mkoani humo zaidi ya maghala 18 ya kuhifadhia mazao yanatarajiwa kujengwa hasa katika maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao,

Hayo yalielezwa na Afisa Biashara kutoka Baraza la Kilimo Tanzania Bw Alinanuswe Ambalile Mkoani Katavi na kusema kazi kubwa katika Mkoa huo imekwisha kufanyika hasa katika kuwajengea uwezo wakulima wadogo ili kuongeza thamani mazao yao.

Bw Ambalile alisema kwa msimu wa kilimo wa mwaka 2018/19 Baraza la Kilimo Tanzania kwa kushirikiana na Mradi wa TIJA TANZANIA wanatarajia kujenga mashamba darasa zaidi 42 kwa mazao ya Mahindi, Mpunga na Maharage,lengo ikiwa ni kuendelea kumjengea uwezo mkulima.

“Baraza la kilimo Tanzania linafahamu msimu wa kilimo umekaribia na tayari tumekwisha kukarabati maghala 7 ya kuhifadhia mazao pia tumekwisha kuwajengea uwezo wakulima ili mazao wanayozalisha yaendane na mahitaji ya soko na tunaamini kupitia mabadiliko haya tunayoyafanya katika kuweka mashamba darasa hayo 42 wakulima watakuwa na uwezo mzuri zaidi wakulima kilimo chenye tija” alisema Bw Ambalile.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Tija Tanzania Bw. Japhet Laizer alisema chini ya uratibu wa Baraza la Kilimo Tanzania mradi wa Tija umekuwa na manufaa makubwa kwa wakulima mkoani Katavi ambapo tayari wakulima 32,000 wamekwisha kujengewa uwezo wa njia bora za kilimo ambazo zimewasaidia kuanza kulima kilimo chenye manufaa kwao kwa kupata mazao ya kutosha.

“Katika msimu huu wa kilimo tumejipanga sasa kuongeza nguvu katika kuhakikisha mkulima anayelima Mahindi, Maharage na Mpunga anapata soko la uhakika la mazao yake tunaamini kupitia washirika wetu tutapata masoko sahihi ya wakulima ili mkulima anapolima apate bei nzuri na hiyo ndio njia pekee ya kumuinua mkulima wa Katavi ” alisema Bw Lazier. 
Muonekano wa Ghala la kuhifadhia mazao linalojengwa na Baraza la Kilimo Tanzania chini ya udhamini wa AGRA katika Kijiji cha Mnyagala Mkoani Katavi likiwa katika hatua za mwisho za kukamilika kwake ambapo baada ya kukamilika litakuwa na uwezo wa kuhifadhi zaidi ya tani 660. 
Mafundi wakiendelea na hatua za uwekaji Kenki katika ghala hilo ambalo litawasaidia wakulima wa kijiji hiki cha Mnyagala ambao ni wakulima wakubwa wa Mpunga mkaoni Katavi kuwa na uwezo wa kuhifadhi mazao yao, ghala hili linatajwa kuwa la kisasa la kipekee katika kijiji hicho.
Mafundi wakiendelea na hatua za mwisho za ukarabati wa Ghala la kuhifadhia mazao la kampuni ya Nondo Investiment iliyoko Mkoani Katavi, Ukarabati ambao unaratibiwa na Baraza la Kilimo Tanzania chini ya udhamini wa AGRA ambapo baada ya ukarabati huo kukamilika ghala hilo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi tani 10000.
Muonekano wan je wa ghala hilo baada ya kufanyiwa marekebisho kwa kuongeza urefu wa ghala hilo ambapo awali lilikuwa na uwezo wa kubeba tani 7000 pekee lakini baada ya kukamilika kwake litakuwa na uwezo wa kubeba tani 10000, ukarabati wote huo unafanywa na Baraza la Kilimo Tanzania chini ya udhamini wa AGRA.
Mafundi wakiwa katika hatua za mwisho za uwekaji wa kenki katika ghala jipya linalojengwa na Baraza la Kilimo Tanzania katika Kata ya Mishamo Mkoani Katavi ambapo baada ya kukamilika kwa ghala hilo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi zaidi ya tani 660 za mazao.
Muonekano wa ghala la kuhifadhi mazao linalojengwa na Baraza la Kilimo Tanzania chini ya udhamini wa AGRA katika Kata ya Mishano Mkoani Katavi, kukamilika kwa ghala hilo kunatajwa kutawasaidia wakulima wa kata hii yenye vijiji 16 kuweza kuhifadhi mazao yao na kuuza kwa bei yenye tija.
Msiamizi mkuu wa ukarabati wa ghala la kuhifadhia mazao katika kijiji cha Bulamata akitoa ufafanuzi kuhusu hatua zilizokwisha kufikiwa katika ukarabati wa ghala hilo linalokarabatiwa kwa kuongeza urefu kwenda juu na Baraza la Kilimo Tanzania chini ya ufadhili wa AGRA ambapo mara baada ya kukamilika litakuwa na uwezo wa kuhifadhi tani 300 tofauti na tani 250 za awali.
 

No comments: