Wednesday, October 31, 2018

MHANDISI NDIKILO APONGEZA JITIHADA ZA TIC KATIKA KUKUZA,KUVUTIA UWEKEZAJI NCHINI

Na Ripota Wetu,Kibaha

MKUU wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo ametembelea banda la Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC) katika Maonesho ya wiki ya

Viwanda Mkoa wa Pwani ambapo ameipongeza TIC kwa jitihada zake katika kukuza na kuvutia uwekezaji nchini na namna inavyowahudumia wawekezaji kupitia huduma za mahala pamoja zinazotolewa na taasisi mbalimbali zilizopo ndani ya ofis za kituo hicho.

Akizungumza leo akiwa kwenye banda la TIC, Mhandisi Ndikilo amesisitiza ni ukweli kwamba Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa mikoa inayopokea wawekezaji wengi na hivyo nguvu ya

kuwahudumia lazima iimarishwe. Aidha ameshauri TIC kuhakikisha inapata taarifa zote muhimu zinazohusiana na uwekezaji ndani ya mkoa wa Pwani kwa kuwasilian na ofisi za Halmashauri zote za Mkoa wa Pwani kwani kwa kufanya hivyo kutarahisisha uratibu na

huduma kwa wawekezaji nchini.

Baadhi ya tarifa alizosisitiza TIC iwe nazo ni pamoja na maeneo ya uwekezaji yaliyotyengwa, takwimu za miradi ya uwekezaji. Katika kuhakikisha kwamba Mkoa wa Pwani unaendelea kuvutia uwekezaji Mkuu wa Mkoa atawasilisha TIC maeneo ambayo tayari yametengwa kwa ajili ya uwekezaji ili yaweze kutafutiwa wawekezaji.

Akizungumza na Waandishi wa habari katika banda la TIC kwenye maonesho ya Wiki ya Viwanda Mkoa wa Pwani yanayoendelea katika viwanja vya Sabasaba vilivyopo Picha ya Ndege wilayani Kibaha mkoani Pwani, Meneja wa Kanda ya Mashariki Venance Mashiba .Amesema kuwa katika kuharakisha utatuzi wa changamoto zinazowakabili wawekezaji, Kituo cha Uwekezaji Tanzania TIC kimeunda Kamati Maalum ya kiaifa inayojumuisha Wakuu wa Taasisi za Serikali ambazo ni wadau katika kuhudumia uwekezaji.

"Kamati hii hukutana chini ya Mwenyekiti wa muda ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa TIC na kujadili changamoto mbalimbali za uwekezaji na kuzitafutia ufumbuzi. Kamati hii inakaa kila baada ya miezi mitatu inajadili changamoto mbalimbali ikiwa ni sehemu yake ya mpango kazi wa kuhakikisha huduma za wawekezaji zinaboreshwa,"amesema.

Ameongeza kuwa kamati hiyo ilianza kufanya kazi mwishoni mwa mwaka jana ikiwa na wajumbe wanaounda kituo cha huduma za mahala pamoja inayoundwa na taasisi 11 zikijumuisha Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA, Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni BRELA, Uhamiaji, Shirika la Viwango Tanzania TBS, Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania TFDA, Wizara ya Ardhi, Kazi na Ajira, Wakala wa Usalama mahala pa Kazi OSHA, Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa NIDA na Shirika la Umeme Tanzania TANESCO na NEMC.


“TIC tunataka kuhakikisha wawekezaji wanapata urahisi wa kuendesha miradi yao hapa nchini ndio maana tunahakikisha kila mara tunaboresha mazingira ya uwekezaji, hatutaki Mwekezaji akija hapa ahangaike kutafuta vibali au leseni zinazohitajika, au achelewe kutatua changamoto zinazomkabili, kwa hiyo kamati hii lengo lake ni kuhakikisha tunaondoa changamoto zote kwa wakati,"amesema Mashiba.

Aidha Kituo kinawakaribisha watu wote, jumuia ya wafanyabiashara na wawekezaji wote kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kwenye maonesho haya ili wajionee bidhaa zinazozalishwa mko wa Pwani na huduma nyingine zinazotolewa na taasisi mbalimbali zinazoshiriki

maonesho haya. Maonesho hayo yaliyoanza Otoba 29 yanatarajia kumalizika Novemba 4, 2018.
 Baadhi ya wadau wa masuala ya viwanda wakiwa kwenye banda la Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC) wakipata maelezo leo baada ya kutembelea maonesho ya viwanda mkoani Pwani
 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akisaini kitabu cha wageni leo baada ya kufika kwenye banda la Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC). Anayeshuhudia ni Meneja wa TIC Kanda ya Mashariki Venance Mashiba
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Meneja wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC) Kanda ya Pwani Venance Mashiba leo kwenye Maonesho ya viwanda mkoani humo

No comments: