Tuesday, October 2, 2018

KESI UTAKATISHAJI FEDHA DHIDI YA ALIYEKUWA MHASIBU TAKUKURU YAKWAMA

Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii

KESI  ya utakatishaji fedha na kumiliki mali zisizolingana na kipato chake halali, inayomkabili aliyekuwa Mhasibu Mkuu wa Takukuru, Godfrey Gugai na wenzake wanne, imeshindwa kuendelea kusikilizwa  sababu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu haina hela ya kuwaleta mashahidi.

Wakili wa Serikali, Pius Hila akisaidiana na wakili kutoka Takukuru, Vitalis Peter ameeleza hayo, leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba,  kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa.

Wakili Hilla amedai walishaita mashihidi  kutoka nje ya Mkoa wa Dar es Salaam lakini wameshindwa kufika kwa kuwa Mtendaji wa Mahakama hakuwa na fungu la  fedha, kwa  ajili ya kuwalipa.Ameendela kueleza kwa sasa wamepata  kibali kutoka kwa  Mtendaji wa Mahakama ambacho kinawaelezea kuwa malipo yatasubiri fedha zitakapoingia lakini mashahidi wameshindwa kuja kwa  gharama zao wenyewe.

"Mheshimiwa hakimu kutokana na hali hiyo, tunaomba terehe fupi kwa ajili ya kuendelea na usikilizwaji wa kesi hii," ameeleza Hilla.Kutokana na maelezo hayo, Wakili wa Utetezi Alex Mgongolwa aliwasilisha maombi mawili mahakamani hapo.

,"Mheshimwa, tunaomba jitihada za kuwapata mashahidi hao waliopo nje ya mkoa wa Dar rs Salaam ziendelee na pia  ni rai yetu kwa  mahakama upande wa mashtaka walete mashahidi ambao hawahitaji kuombewa kibali na hawatoki nje ya mkoa wa Dar es salaam ili Kesi hii iweze kuendelea," amedai Wakili Mgongolwa.

Kutokana na hayo, Hakimu Simba amesema, mahakama itazungumza na Mtendaji wa Mahakama ili kutafuta fedha sehemu yoyote ili mashahidi hao waweze kuja mahakamani na kutoa ushahidi kwa sababu kesi hiyo ni ya muda mrefu.Kesi imeahirishwa hadi  Oktoba 15 na 16, mwaka huu kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa.

Mpaka sasa ni shahidi  mmoja wa upande wa mashtaka, Ayoub Akida(52) ambaye ni Ofisa Utumishi Mkuu kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ameshatoa ushahidi wake dhidi ya Gugai.Mbali na Gugai, washtakiwa wengine, ni George Makaranga, Leonard Aloys na Yasin Katera.

Katika kesi ya msingi, Gugai na mwenzake, wanakabiliwa na makosa 43, kati ya hayo 19 ni ya kughushi, 23 ni utakatishaji fedha na moja ni kumiliki mali zisizoendana na kughushi mikataba ya mauziano ya viwanja katika maeneo mbali mbali.Gugai anakabiliwa na kosa la kumiliki mali zisozoendana na kipato chake, analodaiwa kutenda kati ya January 2005 na Decemba 2015.

 Akiwa ofisa wa umma ameajiriwa na TAKUKURU alikutwa akimiliki mali za zaidi ya Sh. bilioni 3.6 ambazo hazilingani na kipato chake cha awali na cha sasa

No comments: