Saturday, September 29, 2018

LUGOLA ATANGAZA OPERESHENI KUWAONDOA WAHAMIAJI HARAMU MKOANI KIGOMA, AWATAKA UHAMIAJI, POLISI WASHIRIKIANE



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kalinzi, Wilaya ya Kigoma Vijijini wakati Waziri huyo alipofanya ziara wilayani humo kwa ajili ya kusikiliza kero mbalimbali za wananchi wilayani humo. Waziri Lugola alitangaza operesheni kuanza kwa operesheni ya kuwaondoa wahamiaji haramu mkoani Kigoma. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Samson Anga. Kulia ni Mwanasheria wa Sekretaireti ya Mkoa wa huo, Said Kamugisha. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akiyaangalia majina ya watuhumiwa waliopo mahabusu katika Kituo cha Polisi Manyovu, wilayani Buhigwe, Mkoa wa Kigoma, alipokua anaonyeshwa na Askari Polisi wa zamu kituoni hapo, Peter Charles. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (katikati) akiwahoji watuhumiwa (hawapo pichani) ndani ya mahabusu ya kituo cha Polisi Manyovu wilayani Buhigwe, Mkoa wa Kigoma, alipofanya ziara katika kituo hicho kujua utendaji kazi wa Polisi wa kituo hicho kilichopo mpakani na nchi ya Burundi. Kulia ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Martin Otieno. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Buhigwe, Luteni Kanali, Michael Ngayalina, na nyuma yake ni Mkuu wa Kituo hicho, Nickobay Mwakajinga. Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Na Felix Mwagara, MOHA-Buhigwe

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, ameitaka Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kigoma ishirikiane na Jeshi la Polisi kufanya operesheni maalum ya kuwaondoa wahamiaji haramu mkoani humo.

Akizungumza na mamia ya wananchi katika uwanja wa Mnanila mjini Manyovu wilayani Buhigwe, leo, Lugola alisema anataarifa za kutosha kuhusu wahamiaji haramu kutoka nchi za jirani wapo mkoani humo, hivyo lazima waondolewe kwa mujibu wa sheria.

Lugola ambaye alikua akishangiliwa na wananchi baada ya kutoa agizo hilo, pia alikemea tabia ya baadhi ya watu wanaohifadhi raia hao wa kigeni ambao wameingia nchini kinyume cha sheria.

“Sasa natoa agizo hili na litekelezwe, Uhamiaji mkoa washirikiane na polisi kuwaondoa raia hawa wa kigeni ambao wameingia nchini kwa njia zisizo halali, nataka operesheni hii ianze mara moja,” alisema Lugola.

Lugola pia aliirudia kauli hiyo ya kuondolewa kwa wahamiaji hao haramu alipokua anazungumza na wananchi wa Kijiji cha Kalinzi, Wilaya ya Kigoma Vijijini, na kuongeza kuwa anashangaa wahamiaji hao wanaendelea kuwepo mitaani huku maafisa uhamiaji wakiwepo mkoani humo.

“Hivi inakuaje, wananchi wanalalamika hapa kuhusu uwepo wa wahamiaji haramu, lakini Uhamiaji mpo, mnakaa kimya tu, mnataka mpaka mimi nije ndio nitoe maelekezo haya? Hii sitaki kusikia tena, nataka operesheni hii ianza mara moja na iwe endelevu,” alisema Lugola.

Hata hivyo, Lugola alisema katika operesheni hiyo lazima maafisa wa uhamiaji wawe makini wakati wanawaondoa wahamiaji haramu pekee na sio kuwasumbua wananchi wa Kigoma ambao ni raia halali wa nchi hiyo.

Lugola alifafanua kuwa operesheni hiyo itasaidia kupunguza matukio ya uhalifu katika maeneo mbalimbali mkoani humo ambapo kwa kiasi kikubwa hutekelezwa na wahamiaji hao haramu.

Aidha, Waziri Lugola akiwa wilayani Buhigwe, pia ametembelea kituo cha Polisi cha Manyovu kilichopo mpakani na nchi ya Burundi na kukagua utendaji kazi wa askari Polisi wa kituo hicho pamoja na kuiwahoji watuhumiwa waliopo mahabusu kujua makosa yaliyowafanya wawepo ndani ya kituo hicho.

No comments: