Saturday, August 4, 2018

MBUNGE ATOA MILIONI 10 KUSAIDIA VIKUNDI VYA UJASIRIAMALI KATA YA SEPUKA MKOANI SINGIDA



Na Dotto Mwaibale, Singida

MBUNGE wa Singida Magharibi, Mheshimiwa Elibariki Kingu, ametoa sh.milioni 10 kwa vikundi vya ujasiriamali katika Kata ya Sepuka ikiwa kama mtaji ili vijiendesha kwa ufasaha.
Fedha hizo alizitoa katika mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Kata ya Sepuka katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida jana.
Akizungumza wakati akihutubia  mamia ya wananchi wa kata hiyo waliofika kwenye mkutano huo alivitaka vikundi hivyo vya ujasiriamali vilivyopatiwa mtaji huo kwenda kutumia fedha hizo kwa ajili ya uzalishaji na si kwa mambo ya anasa kama kunywa pombe na kuoa.
"Nimetoa fedha hizi kwa ajili ya maendeleo na si kwa ajili ya kufanyia anasa" alisema Kingu huku akishangiliwa.
Alitaja vikundi vya wajasiriamali ambao wamenufaika na mtaji huo kuwa ni vile vinavyo jishughulisha na ufugaji wa kuku, kilimo na biashara mbalimbali ikiwemo migahawa
Katika mkutano huo Kingu alipata fursa ya kuzungumzia miradi mbalimbali ya maendeleo inayofanyika katika jimbo hilo ikiwemo ya ujenzi wa vyumba vya madarasa, zahanati, madaraja, maji, uwekaji wa umeme wa jua pamoja na kuanza ujenzi wa Kituo 
cha Afya cha kisasa katika  Kata ya Sepuka ambacho kitagharimu sh.milioni 400.

"Tunafanya haya yote ikiwa ni utekelezaji wa ilani ya chama changu cha CCM ikiwa ni kumuunga mkono Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa jitihada mbalimbali anazozifanya za kuwaletea maendeleo wananchi na kuziba mianya ya ufisadi" alisema Kingu.

Katika hatua nyingine Kingu amepiga marufuku wanafunzi wa Shule ya Sekondari Sepuka kuchangia ulipaji wa maji shuleni hapo ambapo kila mwanafunzi kwa mwezi alikuwa akilipia sh. 2000 na kuwa sasa fedha hizo atakuwa akizilipa yeye.
Akizungumzia suala la elimu Kingu aliwataka watu wote wanaosimamia elimu katika kata hiyo wakiwemo walimu kuhakikisha wanajipanga kwa kuweka mikakati madhubuti ya  kuinua elimu kutokana na shule za kata hiyo kushindwa kufanya vizuri hivyo kuwa aibu kwake na kwa jamii yote ya hapo.
Katika mkutano huo viongozi wawili wa vyama vya upinzani wilayani humo aliyekuwa Katibu Mwenezi wa Chama cha ACT-Wazalendo na Katibu wa Jimbo la Singida Magharibi, Othman Mkindwa na aliyekuwa Katibu wa Chadema Kata ya Sepuka Omari Saidi Maluja, waliviacha vyama vyao na kujiunga na CCM na kumkabidhi kadi za vyama vyao Mheshimiwa Kingu.

Mkutano huo  ulipambwa na burudani kutoka katika vikundi mbalimbali vya sanaa, ambapo pia kulihudhuriwa  na viongozi na wananchi kutoka vijiji vya jirani na kata hiyo huku Msanii Omari Kiherehere kutoka mjini Singida akitoa burudani safi ya kughani ushairi na kuzikonga nyoyo za wananchi waliokuwepo kwenye mkutano huo.

Mbunge wa Jimbo la Singida Magharibi, Mheshimiwa, Elibariki Kingu, akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Sepuka Halmshauri ya Wilaya ya Ikungi mkoani Singida jana. Mbunge huyo yupo kwenye ziara ya kutembelea kata mbalimbali kuzungumza na wananchi kuhusu maendeleo ya miradi mbalimbali  ikiwa ni utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM)
Wakina mama wa Kata ya Sepuka, wakimfika Mbunge wao Kofia ya Kimila mara baada ya kuwasili Viwanja vya Kata ya Sepuka kwa ajili ya mkutano wa hadhara.
Mheshimiwa Mbunge Kingu, akisalimiana na Wazee wa Kata ya Sepuka baada ya kuwasili kwenye mkutano wa hadhara.
Wanawake wa Kata ya Sepuka wakiwa wamejpanga foleni wakisubiri kusalimiana na mbunge wao.
Mbunge Kingu akisalimiana na wananchi wa Kata ya Sepuka.
Salamu zikiendelea.
Mbunge Kingu, akicheza sanjari na wasanii wa Kikundi cha Umoja cha Kata ya Sepuka.
Wananchi wa Sepuka wakiwa kwenye mkutano huo wa mbunge wao.
Wanafunzi nao walijumuika na wazazi wao kwenye mkutano huo.
Msanii wa Kujitegemea wa mjini Singida, Omari Kiherehere, akighani ushairi mbele ya Mbunge Kingu.

Aliyekuwa Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Kata ya Sepuka, Omari Maluja, akimkabidhi kadi Mbunge Kingu baada ya kukiacha chama hicho na kujiunga CCM.

Wananchi wakila kiapo cha utiifu katika chama cha CCM.
Kiapo kikiendelea.
Kiapo hicho.
Meza kuu ikila kiapo.
Katibu wa CCM Kata ya Sepuka, Juma Mghenyi akiongoza kiapo hicho.
Wanawake wa Kata ya Sepuka wakitoa zawadi ya mbuzi kwa mbunge wao.)

No comments: