Sunday, June 24, 2018

WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI YAZUNGUMZIA MIKAKATI YA SERIKALI KUANDAA MAZINGIRA MAZURI YA UFUGAJI KUKU


Na Emmanuel Masaka,Globu ya jamii


NAIBU Waziri wa Mfugo na Uvuvi atembelea shamba la AKM Glitters Company Ltd lililopo Dar es salaam eneo la Mbopo na Mbezi Beach, ambapo lengo la ziara yake ni kuangalia fursa walizonazo Watanzania katika ufugaji.

Akiwa katika ziara yake katika kampuni hiyo Naibu Waziri ulega ameona kazi mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo ikiwemo ya shamba la kuku wazazi, sehemu ya kutotoleshea vifaranga na chakula cha kuku wazazi.Ulega amesema ufugaji wa kuku ni fursa kubwa  ambayo ikiitumia vizuri, mhusika anaweza kuongeza kipato kwa mtu mmoja mmoja, na taifa zima kwa ujumla wake.

" Serikali lengo letu ni kuhakikisha nyama ya kuku isiwe kitoweo kwa watu wa juu tu, bali kiwe kwa hali zote kuanzia ngazi ya watu wa kipato cha chini na kati."Tunataka watu wote wajiingize kwenye ufugaji wa kuku, ili tuweze kujitosheleza wenyewe na tutoe ajira nyingi kwa watu ili kuendeleza tasnia hii ya kuku na kuuza kuku kwa bei ya chini kuliko kutegemea kuku kutoka nje,"amesema.

Amefafanua katika bajeti  ya serikali kwa mwaka huu wamependekeza pendekezo ambalo limeletwa Wizara ya Fedha na Mipango, kwamba riba imeondolewa kwa asilimia 5 kutoka kwa wakina mama na vijana."Sasa haitakuwa ni hiari kwa Halmashauri bali ni sheria kuwa Halmashauri zote kadri ya mapato yao ya ndani yanavyopatikana yatakwenda moja kwa moja kwa vijana na akina mama kwa asilima 5 kila mmoja," ameongeza.Amesema Serikali imeona hivyo, ili kusaidia hasa wakina mama walio wengi na kufuta riba hiyo.

Kwa upande wake Mkurugezi Mtendaji wa kampuni hiyo Elizabeth Swai alizungumzia suala la usafirishaji vifaranga ikiwa ni changamoto kuwafikia wakazi wa vijijini ambapo Naibu Waziri alisema, Serikali imejiweka katika mazingira mazuri katika hili kuhakikisha usafirishwaji unawafikia pia watu waliopo vijijini.

"Tunaomba tumuunge mkono Rais wetu Dk. John Magufuli katika kazi hii kubwa wanayoifanya ya kuzindua shirika letu la ndege ATC,ambapo haitakuwa na sababu ya kusafirisha kwa gari, ndio maana tunatakiwa kuleta mafanikio ya kuendeleza miundo mbinu ili liwezekane hili."Pamoja na mifugo iweze kukua inabidi kuimarisha ndege zetu pamoja na reli, ambapo reli yetu ya mwendokasi ikifanikiwa ina maana itawezesha usafiri kwa urahisi zaidi na ksafirisha bidhaa katika maeneo mengi kwa haraka zaidi,"amesema.

Ulega amesema hiyo ni fursa kubwa  lazima kampuni ya AKM waungwe na kuona jinsi gani watashirikiana  kuendeleza tasnia hiyo na pia kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa wafugaji wengine ili waweze kufanikiwa kama walivyofanikiwa kwenye kampuni hiyo. Hata hivyo kampuni ya AKM imetoa nafasi kwa walio na uwezo mdogo wakalipa nusu na robo ya Sh.milion 1.9 kwa ajili ya kupata vifaranga na huduma nyinginezo kama dawa na vyakula vya kuanzia.

Naibu Waziri ametoa mwito kwa Watanzania kwamba, hawatakiwi kuagiza nyama kutoka nje bali wanatakiwa kuzalisha hapahapa nyumbani na kujitosheleza wenyewe.Ameongeza hiyo inasaidia kuwa na uhakika wa chakula ambacho kina protein ya kutosha ili ukuaji wa watoto wetu na jamii uwe ni mzuri.

Ulega amesema  " haya mambo yanawezekana tukiungana wote kwa pamoja na sisi kama serikali tupo mstari wa mbele kuhakikisha tunafanikisha hili hasa katika suala la kupunguza zaidi kodi katika vyakula vya mifugo kwa bei ya chini zaidi".
 Naibu Waziri wa Mifungo na Uvuvi,Abdallah Ulega akiangalia kuku wa wazazi katika shamba la (AKM) lililopo Mbopo jijini Dar as Salaam.(picha na Emmanuel Massaka wa Globu ya jamii)
 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi,Abdallah Ulega akizungumza na wafanyakazi wa shamba la kuku wazazi,kituo cha kutotolea vifaranga mbopo jijini Dar as Salaam.
 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi,Abdallah Ulega akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa shamba hilo.

No comments: