Thursday, June 28, 2018

NHIF YAWAHAMAISHA WANAUSHIRIKA KUJIUNGA NA MPANGO WA BIMA YA AFYA

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya mkoani Tanga(NHIF) umewahamasisha wanaushirika mkoani Tanga kujiunga na mpango wa Ushirika Afya ili waweze kupata kadi za matibabu ambazo wanaweza kunufaika na huduma ya matibabu nchini nzima kwani bila afya imara mipango wanayopanga inaweza kushindwa kufanyika kwa ufanisi mkubwa. 

Uhamaishaji huo ulifanywa na Afisa Matekelezo wa Mfuko huo mkoani Tanga Sophia Kaku wakati wa mkutano wa Jukwaa la wadau wa maendeleo ya ushirika mkoani Tanga uliofanyika kwenye ukumbi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Tanga na kufunguliwa na Katibu Tawala wa Mkoa huo Mhandisi Zena Saidi. 

Alisema bila wana ushirika hao kuwa na afya imara mipango yao wanayopanga itashindwa kufanikiwa kwa sababu wanapokuwa wakiungua wanaweza kutumia kiasi kikubwa cha fedha nyingi kuweza kujitibu lakini wanapokuwa kwenye mpango huo wataweza kupata matibabu kwa gharama nafuu. 

“Lakini niwaambie kuwa mkijiunga na mpango wa ushirika mnaweza kunufaika na huduma za matibabu nchi nzima lakini pia utawawezesha kuweza kuwa na uhakika wa matibabu wakato wote bila kujali kama utakuwa na fedha wakati unapougua “Alisema. 

Alisema mpango wa ushirika afya ni mpango maalumu unaomuwezesha wana ushirika kwa umoja wao kuchangia huduma za matibabu kabla ya mwanachama kupata majanga yakiwemo maradhi,kuunguliwa au magonjwa mbalimbali wakati wakiendelea na shughuli zao. 

Hata hivyo aliwataka wanaushirika hao kuona umuhimu wa kuwekeza kwenye mpango huo ili kuweza kupata huduma za matibabu wakati wanapokuwa wakikumbana na maradhi mbalimbali ambayo yanaweza kuwapelekea kushindwa kutekeleza wajibu wao kama ilivyokuwa awali. 

“Ndugu zangu niwaambieni bima ya afya ndio mambo yote bila kuwa na afya imara mipango tunayopanga haiwezi kukamilika hivyo niwaase tujiunge na mpango huo wa Ushirika Afya ambao ni mpango maalumu unaowawezesha kuchangia huduma za matibabu kabla ya kupata majanga”Alisema.
Afisa Matekelezo wa Mfuko huo mkoani Tanga Sophia Kaku akizungumza wakati wa mkutano wa Jukwaa la wadau wa maendeleo ya ushirika mkoani Tanga uliofanyika kwenye ukumbi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Tanga na kufunguliwa na Katibu Tawala wa Mkoa huo Mhandisi Zena Saidi. 

No comments: