Thursday, June 21, 2018

MSHINDI WA GARI KUTOKA BE FORWARD ATIMIZA NDOTO ZAKE JIJINI MWANZA

Mnamo mwezi Desemba mwaka 2013 Dr. Marko Hingi ambaye alikuwa mwanafunzi wa udaktari katika chuo kikuu cha afya na sayansi alishinda gari kupitia kampuni ya kuagiza magari ya Be Forward ambapo alikabidhiwa mnano mwezi wa pili mwaka 2014.
Katika makabidhio hayo yaliyofanyika katika bustani ya palm residency karibu na hospitali ya Ocean Road Dar es salaam.
Blog ya michuzi imefanikiwa kumtafuta Dr. Marko Hingi na kufanya mahojiano nae miaka minne baada ya kushinda gari aina ya Toyota-Noah ambapo katika mahojiano na vyombo vya habari aliahidi kulitumia gari hilo kubeba wagonjwa hasa kimama wajawazito na watoto wanapopata dharura.
Michuzi Blog:-Habari, tumefurahi kukutana na wewe baada ya miaka minne kupita na tungependa kukufahamu wewe ni nani na unafanya nini kwa sasa?
Dr.Marko Hingi:- Asante sana, Naitwa Dr. Marko Hingi ni daktari wa binadamu na pia ni mkurugenzi wa asasi isiyo ya kiserikali ya Tanzania Rural Health Movement ambayo ipo jijini Mwanza na inajishughulisha na kutoa huduma za afya,kufanya tafiti za afya pamoja na utunzaji wa mazingira endelevu.
Michuzi Blog:-Unaweza kutueleza namna ulivyoshinda gari mwaka 2013/2014
Dr.Marko Hingi:-Nakumbuka nilikuwa mwaka wa tatu katika masomo yangu ya udaktari na pia nilikuwa shirati-Mara kwenye mafunzo kwa njia ya vitendo ambapo niliona ukurusa wa facebook wa be forward na kuanza kuufuatiria na pia niliona tangazo la kushiriki katika shindano la kushinda magari kwa msimu wa sikukuu wa krismas na Be Forward walihitaji washiriki kujibu kwanini unataka gari na niliweza kueleza sababu kwanini nahitaji gari kwa maneno 135 ambapo nililenga kuwasaidia wakimama na watoto waishio vijijini kipindi cha dharura.
Nikiwa katika kuona wagonjwa pamoja na mkufunzi wangu Dr.Nkinda katika idara ya mifupa mnamo  saa nane mchana tarehe 3 desemba 2013 nilipokea ujumbe kweny barua pepe ukinijulisha kuwa nimeshinda gari kama mshindi wa tatu duniani kati ya washindi 25. Kwa kweli sikuamini lakini badae nikaona katika ukurasa wa facebook be forward wakinipongeza pia.
Michuzi Blog:-Katika mahojiano tuliyofanya na wewe mnamo tarehe 25 February 2014 ulisema utalitumia gari hilo kama gari la kubebea wagonjwa. Je mpaka sasa umefikia wapi h uliweka kama ahadi kwa watanzania hasa wakina mama wajawazito na watoto.
Dr.Marko Hingi:- Ni kweli niliahidi kulitumia gari lile kwa ajili ya kutoa huduma za afya hasa za dharura lakini kabla ya kuanzia kutoa huduma za dharura gari si jambo la kwanza, kuna mambo manne ambayo ni muhimu; kwanza ni mfumo wa mawasiliano ambao utatuwezesha kuwasiliana kipindi cha dharura, pili ni usafiri ambao si lazima uwe gari maalumu lakini usafiri wowote wa kufikasha mgonjwa sehemu sahihi kwa ajili ya matibabu zaidi, tatu mafunzo kwa watoa huduma za dharura n.k na mwisho ni uongozi endelevu ambao utaweza kusimamia haya mambo yote na kutoa huduma sahihi na kwa wakati. Kwa kipindi kile nisingeweza sababu ya masomo lakini pia gharama za kuanzisha huduma hiyo.
Mwaka mmoja badae niliweza kuanzisha ushirikiano na Trek Medics International ambayo ni asasi isiyo ya kiserikali ipo New York Marekani na tuliweza kusaidiana kwa pamoja kuanzisha huduma ya dharura jijini Mwanza ambapo tulitumia mifumo/tasisi ambazo zipo kama jeshi la zima moto na uokoaji, waendesha pikipiki (Bodaboda) pamoja na police traffic hawa tuliwapa mafunzo ya kutoa huduma ya kwanza na kuwaunganisha na mfumo wa mawasiliano kwa njia ya meseji unaoitwa “Beacon” ambapo urahisisha kwa watoa huduma kupata taarifa za matukio ya dharura na kutoa msaada kwa haraka zaidi.
Michuzi Blog:- Je huduma hii inapatikanaje na je walengwa wamefikiwa hasa kina mama wajazito na watoto?
Dr.Marko Hingi:- Huduma hii kwa hapa mwanza inaitwa Huduma ya kwanza kwa jamii ambayo inapatika bure bila malipo yoyote na mtu mwenye tatizo/dharura anaweza kupiga simu ya bure namba 114 na atapatiwa usaidizi ndani ya muda mfupi
Kwa sasa tunapokea matukio mengi ya dharura ambayo yanatokana na ajali za barabarani ambapo kwa wastani tunapata matukio 16 kwa mwezi lakini kwa wakinamama wajawazito tangu tumeanza mwishoni mwa mwaka 2015 tumepata matukio matatu tu na hii inaweza kusababishwa na huduma hii kuwepo mjini lakini naamini tukisogea vijijini tutafanikiwa zaidi kusaidia wakinamama wajawazito na watoto wanapopata dharura.
Michuzi Blog:-Je kwa sasa mna mipango gani ya kuendeleza huduma hii katika maeneo megine hasa vijijini na changamoto zipi mnakabliana nazo?
Dr.Marko Hingi:- Kurahisisha kusambaa kwa huduma hii tumeamua kuiweka wazi kwa yeyote anayrtaka kuanzisha katika eneo lake kama ni kijijini au mjini na sisi tutamsaidia kumpa mafunzo na uzoefu pamoja na mfumo wa mawasiliano ili aweze kutumia rasilimali ambazo zipo katika maeneo hayo kwa mfano, sasa Iringa kupitia 1 Call Tz wameanzisha huduma hii mjini Iringa na inapatikana kwa kupiga namba 114 na ni bure bila malipo.
Bahati mbaya gari ambayo nilishinda ilikuwa na shida ya injini ya haikuweza kufaa kutumiaka kama gari ya wagonjwa hapa Mwanza na tunashukuru msaada toka The Desk and Chair Foundation ambapo walitusaidia pikipiki ya kubeba wagonjwa ya matairi matatu na inatusaidia sana katika kubeba wagonjwa japokuwa haina mwendokasi wa kutosha kuwafikia baadhi ya wagonjwa kwa wakati.
Jambo lingine ni jamii kutotoa taarifa kwa wakati pindi tukio la dharura linapotokea na badala yake wanatumia simu zao kupiga picha na kuzituma kwenye mitandano badala ya kupiga namba 114 kwa msaada zaidi.










No comments: