Wednesday, May 16, 2018

UPANDE WA UTETEZI KESI YA 'UCHOCHEZI' INAYOWAKABILI VIONGOZI CHADEMA WATOA MAOMBI YAO ,WAWASILISHA MAPINGAMIZI NANE

Na Karama Kenyynko,Blogu ya jamii

UPANDE wa utetezi katika kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa Chadema akiwemo Mwenyekiti wa Chama hicho Freeman Mbowe, wameomba Mahakama kutupilia mbali mashtaka dhidi ya washtakiwa kwa kuwa yanamapungufu, kisheria.

Maombi hayo yamewasilishwa leo mahakamani hapo  mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Wilabard Mashauri wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Wakili Peter Kibatala.Hivyo amewasilisha mapingamizi nane ya kisheria yanayoshambulia uhalali wa hati ya mashtaka na mashtaka dhidi ya washtakiwa.

Katika mapingamizi hayo, Kibatala amedai, kibali cha DPP kina mapungufu ya kisheria kwa sababu haioneshi imetolewa kwa mashtaka yapi  na pia hati ya mashtaka imewataja majina washtakiwa wote bila ya kufafanua na pia imetaja tu kifungu cha sheria ambacho washtakiwa wameshtakiwa nacho 
Amedai, hakuna kibali kilichowasilishwa mahakamani hapo kwa maana hiyo mashtaka dhidi ya washtakiwa yamepelekwa mahakamani hapo bila ridhaa ya DPP.

Amedai Aidha Kibatala ametoa ombi mbadala na kuomba, iwapo Mahakama itashindwa kuifuta hati nzima ya mashtaka yanayowakabili washtakiwa hao basi iyafutilie mbali mashtaka ambayo yanamapungufu kisheria. Ikiwamo shtaka la nne, latano, la sita na la saba.

Alidai, maelezo ya mashtaka hayo yanawachanganya washtakiwa na hawawezi kujitetea ipasavyo. Pia mashtaka hayo kufunguliwa kwake kunahitaji ridhaa ya (DPP) ambayo haipo kutokana na mapungufu hayo, inaonesha hakuna ridhaa yake.

Amebainisha kwa kuwa mashtaka hayo tajwa kufunguliwa kwake kunahitaji ridhaa ya DPP, lakini kuwa haipo tunaomba yafutiliwe mbali. Alidai Kibatala.Pia alidai hati ya mashtaka inamapungufu kwa sababu shtaka la pili na la Tatu hayana maelezo ya kutosheleza ya kuwapa washtakiwa msingi na uwezo wa kuweza kujitetea kikamilifu katika kesi hiyo ya jinai.

Alidai, katika shtaka la kufanya mkusanyiko bila kibali hati haijataja watu waliotishiwa na wametajwa kwa wingi hivyo haijulikani ni washtakiwa ama ni watu wengine.

Akiendelea kuwasilisha maoungamizi hayo, kibatala amedai, mashtaka yanayowakabili washtakiwa hao yamejichanganya na hayaonyeshi walipelekeaje kifo cha Akwilina na hao majeruhi walijeruhiwa na nani na kwa kutumia nini.

Amedai, maelezo katika hati ya mashtaka yamerundikana  kiasi kwamba ni vigumu mtu kujitetea na kwamba unapomshtaki mtu  kwa kisababisha kifo ni lazima utoe Maelezo ya kutosha kuonesha unamaanisha kitu Fulani ili mtu  aweze kujitetea.

Pia amedai mapungufu mengine yaliyomo kwenye hati hiyo ni kuwa hayaoneshi dhumuni la pamoja ambalo washtakiwa walikutana kulitenda hivyo linawanyang'anya washtakiwa haki ya kujitetea.

Kibatala alidai kuwa hati ya mashtaka inamapungufu kwa sababu  vifungu vilivyotajwa katika shtaka la Tatu, tano na saba siyo sahihi.

Alidai katika shtaka la 10,11 na 12 yanamapungufu kisheria kwa sababu hayaonyeshi watu waliochochewa kufanya makosa ni wakina nani waliohudhuria mkutano, wakazi wa kinondoni ama wapiga kura bila kujali itikadi zao.

AJIBU MAPIGO 

Wakili wa Serikali Mkuu,Paul Kadushi ameiomba Mahakama kuyatupilia mbali mapingamizi yote hayo ya upande kwa kuwa hayana mashiko kisheria. Kuhusu kibali cha DPP kinachoipa Mahakama ridhaa ya kusikiliza kesi,Kadushi amedai hakuna uamuzi wowote ulioweka msingi kwamba ni lazima kiwepo na nini ama hakipaswi kuwepo na nini.

Mbali na  Mbowe wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo Namba 112 ya 2018 ni  mbunge wa Iringa Mjini Peter Msigwa, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar Salum Mwalimu na Naibu katibu Mkuu bara na Mbunge wa kibamba John Mnyika.

Mbunge wa Tarime mjini Esterher Matiko, Katibu wa chama hicho Dk  Vicenti  Mashinji na mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche, Mbunge wa Kawe Halima Mdee na  mbunge wa bunda, Esther Bulaya.

Washtakiwa hao wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 12 katika kesi ya jinai namba 112 ya mwaka 2018 ikiwamo kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali kinyume cha sheria na kuendelea kufanya mkusanyiko usio halali ama maandamano yaliyosababisha kifo cha Akwilina.

No comments: