Wednesday, May 30, 2018

RC Wangabo kutumia nguvu ya dola kukomesha Kipindupindu

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amesema atalazimika kuwatumia polisi kusimamia zoezi la usafi na ujenzi wa vyoo salama katika Kijiji cha Namasinzi, kata ya Kapenta, bonde la ziwa Rukwa Wilayani Sumbawanga baada ya wananchi hao kushindwa kujenga vyoo hivyo mbali na elimu ya umuhimu wa vyoo waliyopewa kwa muda mrefu.

Amesema kuwa ikifikia hatua hiyo Kijiji hicho kitafungiwa na hakuna atakayetoka wala kuingia na hatimae kusitisha shughuli za kiuchumi za Kijiji hicho ambacho ni maarufu kwa kilimo cha mpunga hali itakayopelekea maisha magumu kwa wananchi hao jambo ambalo asingependa litokee.

Katika kuhakikisha hali hiyo haitokei Mh. Wangabo alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Dk. Khalfan Haule na timu yake ya usafi ya halmashauri kuhakikisha wanapita kaya kwa kaya ili kuzibaini kaya zisizopenda usafi na zisizokuwa na vyoo na kuzichukulia hatua za kisheria kwani kwa kushindwa kufanya hivyo kipindupindu hakitamalizika katika bonde hilo.

“Sasa tutatumia nguvu ya dola, ili kuhakikisha kwamba kila mtu anaishi katika maisha ya usafi wala sio uchafu, na kila mtu ahakikishe kwamba anakuwa na kiboko Fulani ambacho ni kigumu amuone mtu anachemsha maji, anayaweka maji yake yanapoa akienda shambani anakwenda na maji mbayo yamekwisha poa, lakini mkilea lea hivi, waswahili wanasema ukicheka na nyani unavuna mabua, mabua ambayo tunayavuna ni vifo.” Alisisitiza.

Aliyasema hayo katika Mkutano wa hadhara alioufanya katika  kijiji cha Namasinzi, Kata ya Kapenta, Wilayani Sumbawanga, kijiji ambacho wananchi watatu wamefariki kwa ugonjwa wa kipindupindu na wengine wakiendelea kupatiwa huduma. 

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa hlamshauri ya Wilaya ya Sumbawanga Dkt. Fani Musa aliendelea kuishukuru serikali kwa kuendelea kupeleka misaada katika bonde hilo ili kuhakikisha wanakabiliana na ugonjwa huo na kusisitiza kuwa wataendelea kutoa elimu bila ya kuchoka akiamini kuwa wananchi hao wataelewa wakiendelea kusimamiwa.

“Serikali imekuwa ikifanya kazi tatu kwa wakati mmoja, tumekuwa tukitoa elimu ya ugonjwa huu kwa lengo la kuzuia haya yasitokee, lakini yakitokea tunatumia nguvu kubwa ya kukabiliana na tatizo hili lakini pia serikali inatoa dawa za kutosha ili kuweza kuponya pia, ugonjwa wa kipindupindu ni kitendo cha kula kinyesi ambacho ni kibichi, hivyo watu ni muhimu kujenga vyoo salama,” Alimalizia.

Tangu kulipuka kwa ugonjwa huo tarehe 6 Mei, 2018 watu 14 wameshafariki na wengine 221 wakiendelea na kupatiwa matibabu katika kambi za wagonjwa hao katika bonde la ziwa Rukwa, Wilayani Sumbawanga.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa pili toka kushoto) akiwa Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Dkt. Khalfan Haule (wa kwanza kushoto pamoja na timu ya afya ya wilaya na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa wakikagua vyoo katika Kijiji cha Namasinzi, Kata ya kapenta, Wilayani Sumbawanga.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia) akikabidhi tenki la lita 5000 kwa mwenyekiti wa kitongoji cha Liweliyamvula, Kijiji cha Lumbesa, Kata ya Kapenta, Wilayani Sumbawanga Paulo Maufi, ikiwa ni miongoni mwa juhudi za serikali kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama na kuhifadhiwa sehemu salama, kuepukana na kipindupindu.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia) akikabidhi dawa za “Water guard” kwa mwenyekiti wa kitongoji cha Liweliyamvula, Kijiji cha Lumbesa, Kata ya Kapenta, Wilayani Sumbawanga Paulo Maufi, ikiwa ni miongoni mwa juhudi za serikali kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama, kuepukana na kipindupindu.

No comments: