Saturday, April 28, 2018

AfDB YAAHIDI KULING'ARISHA JIJI LA DODOMA NA KUONGEZA MABILIONI YA DOLA KUCHOCHEA MAENDELEO YA TANZANIA

Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma 

Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB, Dkt. Akinumwi Adesina, amemaliza ziara yake ya siku tatu nchini na kuahidi kuwa atahakikisha Tanzania inaendelea kunufaika na misaada na mikopo yenye masharti nafuu kutoka Benki hiyo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kisasa katika Jiji la Dodoma na mradi wa kuzalisha umeme wa Stieglers Gorge. 

Akiwa katika uwanja wa ndege Jijini Dodoma, Dkt. Adesina amemmwagia sifa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna anavyosimamia ukuaji wa uchumi uliofikia wastani wa asilimia 7 kwa mwaka pamoja na kupambana na vitendo vya ufisadi, rushwa, kuimarisha uwajibikaji wa viongozi kwa wananchi, kupiga vita matumizi mabaya ya rasilimali za umma ili kuwaondoa wananchi wake katika umasikini. 

Dkt. Adesina amesema kwa kutambua mchango huo pamoja na umahili wa Waziri wa Fedfha na mipango Dkt. Philip Mpango, wa kusimamia uchumi na sera ya bajeti na fedha, benki yake itaendelea kuwekeza kiasi kikubwa cha fedha ili nchi iweze kupiga hatua kubwa kupitia miundombinu mbalimbali inayotekelezwa kupitia benki yake na washirika wengine wa maendeleo. 

Miongoni mwa miradi ambayo Benki hiyo imepanga kusaidia ni ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa utakaojengwa katika eneo la Msalato, nje kidogo ya Jiji la Dodoma ambapo kwa kuanzia benki hiyo itatoa zaidi ya shilingi bilioni 200. 

“Tumekuwa na majadiliano ya kina na Mhe. Rais Dkt. John Magufuli kuhusu mradi wa kuzalisha umeme wa Stieglers Gorge ambao utazalisha Kw 2100, Benki yetu itaangalia namna ya kutoa fedha kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa mradi huo mkubwa” alisema Dkt. Adesina. 

Alisema kuwa suala la mapinduzi ya viwanda haliwezi kufanikiwa bila kuwa na nishati ya umeme ya uhakika na kwamba benki yake itawekeza dola za Marekani bilioni 1.5 kwa ajili ya sekta ya nishati na itaongeza kiasi kingine cha dola milioni 950 kwa ajili ya kazi hiyo. 

“Mwaka huu tutatoa fedha kwa ajili ya kuboresha nishati ya umeme katika ukanda wa Kaskazini Magharibi mwa Tanzania na tuna mpango pia wa kuboresha Shirika la Ugavi wa Umeme hapa nchini-TANESCO, ili liweze kuzalisha umeme wa uhakika na wenye gharama nafuu kwa ajili ya kuendeleza mpango wa Serikali wa kuwa na uchumi wa viwanda” aliongeza Dkt. Adesina 

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameelezea kufurahishwa na ujio wa Rais huyo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB, Dkt. Akinumwi Adesina, na kwamba ujio huo umeleta neema kwa nchi baada ya benki hiyo kuahidi kutoa shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kujenga Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato pamoja na kuahidi kutoa fedha kwa ajili ya kujenga barabara za mchepuko (mzunguko) Jijini Dodoma. 

Dkt. Mpango amewataka watanzania kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuwaletea maendeleo na watembee kifua mbele kwa kuwa hivi sasa Tanzania imeshika nafasi ya pili katika Bara la Afrika kwa ukuaji wa uchumi kwa kasi ikitanguliwa na nchi ya Ethiopia, na Rais Adesina amelisemea vizuri jambo hilo. 

Ushirikiano wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB na Tanzania ulianza tangu mwaka 1971, ambapo mpaka sasa benki hiyo imewekeza kiasi cha dola bilioni 3.6, sawa na zaidi ya shilingi trilion 8, katika miradi mbalimbali ya kiuchumi ikiwemo umeme, barabara, maji na usafi wa mazingira, uboreshaji rasilimali watu pamoja na masuala ya utawala bora.

No comments: