Tuesday, March 27, 2018

Mbowe, vigogo Chadema wafikishwa Mahakama ya kisutu,wanakabiliwa na mashtaka nane likiwemo la uchochezi na uasi.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA, Freeman Mbowe na vingozi wenzake watano, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashitaka nane yakiwemo ya uchochezi na uasi.

Mbali na Mbowe wahtakiwa wengine ni wengine ni Peter Msigwa, Salum Salum, John Mnyika, Ester Matiko na Dk Mashinji.

Katika mashtaka hayo nane, shtaka la kwanza na la pili linawakabili watuhumiwa wote sita, huku Mbowe peke yake anakabiliwa na mashtaka matano, yaani shtaka la tatu hadi la saba na Msigwa akikabiliwa na shtaka moja la peke yake la nane.

Akisoma hati ya mashitaka wakili wa Serikali Mwandamizi, Faraja Nchimbi amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, kuwa Februari 16, mwaka huu washtakiwa kwa pamoja, wakiwa katika barabara ya Kawawa wilayani Kinondoni, walifanya mkusanyiko na maandamano isivyo halali kinyume na sheria,

Imedaiwa walikusanyika kutekeleza lengo la pamoja kufanya mkusanyiko usio wa halali wenye vurugu na kufanya watu waogope kwamba watakwenda kusababisha uvunjifu wa amani.

Aidha Nchimbi ameongeza kudai kuwa, Februari 16, mwaka huu katika barabara ya Kawawa eneo la Mkwajuni wilayani Kinondoni, washtakiwa wakiwa wamekusanyika wao na wenzao 12 ambao bado hawajafikishwa mahakamani, wakiwa kwenye maandamano hayo,licha ya kutolewa tamko la kuwataka kutawanyika...waligoma kutii amri hiyo na kuendelea na maandamano na kusababisha kifo cha Aquilina Akwkilina kusababisha askari wawili kujeruhiwa kutokana na mkusanyiko huo.

Katika shtaka la tatu imedaiwa Februari 16, mwaka huu katika viwanja vya Buibui wilayani Kinondoni, jijini mshtakiwa Mbowe peke yake wakati akihutubia wananchi wa jimbo hilo alihamasisha chuki isivyohalali kwa kutoa matamshi ya kuhamasisha chuki maneno ambayo yalipelekea chuki mioyoni mwa wana jamii wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pia Mbowe anadaiwa kufanya uchochezi na kusababisha chuki miongoni mwa wanajamii ya watanzania kinyume na sheria.Aidha Nchimbi amedai
Katika mashitaka ya uchochezi wa uasi yanayomkabili Mbowe, inadaiwa katika maeneo hayo akiwa katika mkutano wa hadhara, akiwa na nia ya kupandikiza chuki na dharau kwa watanzania dhidi ya uongozi wa kiserikali uliopo madarakani kisheria, alitamka maneno yenye kupandikiza chuki na kuleta ushawishi wa uasi dhidi ya serikali iliyopo madarakani kisheria

Nchimbi aliendelea kudai, katika tarehe hiyo hiyo na maeneo hayo mkoani Dar es Salaam, Mbowe alitoa matamshi ya kupandikiza chuki na dharau dhidi ya mamlaka halali ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania.

Katika shitaka la saba, Mbowe anakabiliwa na tuhuma za kutenda kosa la kushawishi kutendeka kwa kosa la jinai, ambapo amedaiwa siku hiyo, akiwa pia amejumuika na wengine ambao hawako mahakamani, aliwashawishi wakazi hao wa Kinondoni, kutenda kosa la kufanya maandamano na mkusanyiko usio wa halali.

Mshtakia Msigwa anadaiwa kushawishi raia kutenda kosa la jinai shtaka analodaiwa kutenda February 16, mwaka huu katika maeneo hayo hayo ya Viwanja vya Buibui wilayani Kinondoni Dar es Salaam,Imedaiwa siku hiyo Msigwa aliwashawishi wananchi wa Kinondoni kutembea mbele ya umma wakiwa na silaha.

Washitakiwa wamekana mashitaka hayo na upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa shauri hilo umekamilika hivyo wanaomba ipangwe kesho au keshokutwa kwa ajili ya kuwasomea maelezo ya awali.

No comments: