Friday, March 16, 2018

AZAM WAANZA MAANGAMIZI YA KUMUUA MTIBWA KOMBE LA FA

Na Zainab Nyamka,Globu ya Jamii.

Kikosi cha Azam FC, kimeanzamaandalizi ya kuivaa Mtibwa Sugar huku Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Idd Cheche akiahidi mchezo mzuri na kuondoka na ushindi kwenye mtangane wa robo fainali ya kombe la Azam Sports HD dhidi ya Mtibwa Sugar.

Mchezo huo wa hatua ya robo fainali ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup) unatarajia kufanyika Uwanja wa Azam Complex Machi 30 mwaka huu saa 1.00 usiku, ambapo tayari kikosi cha Azam FC kimeshaanza maandalizi tokeo jana jioni.

“Mashabiki waendelee kutusapoti kwa sababu mchezo wa mpira unahitaji sapoti, mchezo wa mpira una wachezaji, una viongozi, una mashabiki na mashabiki ndio wanaoongeza chachu ambayo inakuja kufanya mchezo uwe pendwa duniani.

“Kwa hiyo mashabiki waje kwa wingi watusapoti na sisi tutahakikisha tunawapa furaha ile ambayo wanaitarajia, watarajie mchezo mzuri na wenye ushindi,” alisema Cheche.

Cheche aliyewahi kuwa Kocha Mkuu wa timu ya vijana ya Azam FC (Azam U-20) kabla ya desemba mwaka juzi kupewa nafasi hiyo timu kubwa, alisema mchezo huo utakuwa ni tofauti sana na ule waliocheza kwenye Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) msimu huu na kutoka sare ya bao 1-1.

“Mchezo wa ligi ni tofauti na FA, huu ni mchezo wa mtoano (knockout) lazima mmoja afungwe kama mnatoka sare mnafika kwenye hatua ya penalti lakini sisi tunataka kuhakikisha mchezo tunaumaliza ndani ya dakika 90 lakini kikubwa mno kwanza ni kuanza kuwajenga wachezaji wetu mazoezini kwa sababu mazoezi ndiyo yatatupelekea kufanya vizuri huu mchezo kwa hiyo tuko makini kuhakikisha watu wanafanya mazoezi vizuri ili mechi iweze kuwa nyepesi kwetu,” alisema.

Akizungumzia maandalizi waliyoanza, Cheche alisema kuwa kwa sasa watafanyia kazi mazoezini makosa waliyofanya kwenye mechi zilizopita ikiwemo kuwadukua wapinzani wao Mtibwa Sugar.

“Tunafanyia kazi matatizo tuliyokuwa nayo kidogo kwenye mechi zetu za ligi tulizocheza huko nyuma, kurekebisha makosa, kuangalia kitu gani cha kufanya, kuiangalia Mtibwa uzuri wake na udhaifu wake ili tuandae vijana wetu wahakikishe tunakwenda kuwaangamiza Mtibwa,” alisema.

Msimu uliopita timu hizo zilikutana kwenye hatua ya 16 bora ya michuano hiyo, mchezo ukifanyika kwenye Uwanja wa Azam Complex saa 10.00 jioni na Azam FC ikafanikiwa kuibuka kidedea kwa ushindi wa bao 1-0, liliwekwa kimiani na Ramadhan Singano ‘Messi’, akiunganisha pasi safi ya kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’.

Mshindi wa mchezo huo, atacheza ugenini kwenye nusu fainali na mshindi wa robo fainali nyingine kati ya Stand United na Njombe Mji, mchezo huo ukipigwa Uwanja wa Kambarage, Shinyanga Machi 30 mwaka huu.

No comments: