Thursday, February 15, 2018

WABUNGE CCM WAMIMINIKA KUMUOMBEA KURA MTULIA UBUNGE JIMBO LA KINONDONI

Na Said Mwishehe,Globu ya jamii


CHAMA Cha Mapinduzi(CCM) kupitia viongozi wake wa ngazi mbalimbali wameendelea kunadi sera za maendeleo na kumuombea kura mgombea wao wa ubunge kwenye uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kinondoni jijini Dar es Salaam huku baadhi yao wakisema uchaguzi huo ni sawa na usajili wa dirisha dogo.

Hivyo wanatumia usajili huo kwa ajili ya kumpata Mtulia ambaye wanaamini ni mtu sahihi kwa maendeleo ya wananchi wa Kinondoni kwani alikokuwa awali hakuwa nafasi ya kushirikiana na Serikali ya Rais ,Dk.John Magufuli kufanya maendeleo.

Wakizungumza kwenye kampeni za uchaguzi huo unaotarajia kufanyika Februari 17(Jumamosi ya wiki hii), viongozi wa CCM wakiwamo baadhi ya mawaziri ambao wamefika kwenye kampeni hizo kwa nafasi zao za ubunge,wamewaambia wananchi hao Mtulia ndio mtu sahihi kwao.

Mgeni rasmi kwenye kampeni zilizofanyika leo Kata ya Ndugumbi ambaye pia ni mbunge wa Mbinga Sixtus Mapunda amesema anatambua uwezo wa Mtulia na hivyo ni vema wananchi wakamchagua ili awatumikie kikamilifu.

Amewaeleza wananchi kuwa uchaguzi mkuu ulishafanyika mwaka 2015 na sasa ni uchaguzi mdogo ,hivyo Chama ambacho kimepewa dhamana ya kuongoza ni CCM na kwa maana hiyo Mtulia akiwa mbunge atashirikiana na viongozi wengine kuleta maendeleo ya wananchi.

Amefafanua anaufananisha uchaguzi huo na usajili wa dirisha dogo ambapo tayari CCM wanayo timu nzuri yenye ushindani wa hali ya juu na iliyokuwa na ari ya kuwatumikia wananchi,hivyo kwenye usajili huo wanamtaka Mtulia kuboresha timu yao.

"CCM ni timu ambayo inawachezaji wazuri na waliotumia kwenye kila idara na kama mnavyojua kwenye usajili mdogo lazima msajili mchezaji ambaye atakuwa na uwezo na anaendana na kasi na timu ambayo tunayo.Hivyo Mtulia ni mtu sahihi kwetu.

"Kule alikokuwa mwanzoni hakuwa na uwezo wa kufanya maendeleo kwani kila akitaka kufanya wenzake wanamzuia kwa kigezo kuwa yakipatikana maendeleo ya Kinondoni upinzani hautakuwa na nafasi mwaka 2020.Hivyi akiwa CCM atafanya maendeleo kwa kasi kubwa na tutampa ushirikiano kadri ya uwezo wetu,"amesema Mapunda.


BASHE ATAKA POLISI KUFANYA UCHUNGUZI

Kwa upande wa Mbunge wa Nzega Mjini mkoani Tabora, Hussein Bashe ameendelea kuwasisitiza wananchi wa Kinondoni kuhakikisha wanamchagua Mtulia, Februari 17 mwaka huu ambayo itakuwa siku ya Jumamosi.

Ametumia nafasi hiyo kuwaambia wananchi wa Kinondoni kuwa katika Jimbo la Siha tayari wameshafanya uamuzi kuwa siku hiyo ya uchaguzi watamchagua mgombea ubunge wa CCM, Dk.Molleli.

Mbali ya kumuombea kura Mtulia, Bashe amesema kwa niaba ya wana CCM wa Kinondoni wanatoa pole kwa familia ambayo wameondokewa na mtu wao muhimu ambaye amekutwa amekufa kwenye ufukwe wa Koko jijini Dar es Salaam.

Mtu huyo ambaye ni kada wa Chadema amekutwa amekufa kwenye ufukwe huo, hivyo Bashe ameliomba Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kufanya uchunguzi ili waliouhusika wakamatwe na kuchukuliwa hatua.

"Kumekuwa na tabia ya ajabu sana kila inapofanyika chaguzi mdogo kumekuwa na matukio ya uhalifu na kinyama ambayo hufanywa na baadhi ya watu na wenzetu wa upande wa pili wanaleta lawama kwetu."Tunalaani tukio hilo la mauji ambalo limefanywa kwa mtu huyo na tunaomba Polisi wafanye uchunguzi wao wa kina ili waliohusika wachukuliwe hatua,"amesema Bashe.

Wakati huohuo Bashe ameitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC) kuhakikisha kwenye uchaguzi huo unafanyika kwa amani na utulivu na haki itendeke."CCM tumejiandaa kwenye uchaguzi huo na hatuna wasiwasi maana mgombea tuliyenaye anatosha,"amesema.Pia ametumia nafasi hiyo kumwambia Mtulia kuwa kwa miaka miwili aliyokuwa upande wa pili, amepoteza muda wake na sasa amekuja upande sahihi na atakapochaguliwa kuwa mbunge ahakikishe anatatua kero za wananchi.


JAFO AELEZEA UWEZO WA MTULIA


Mbunge wa Jimbo la Kisarawe ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(Tamisemi) Suleiman Japo amesema kwa dhati ya moyo wake alikuwa anamuomba Mungu afike kwenye jimbo la Kinondoni kumuombea kura Mtulia kwani anatambua uwezo wake.

Amewaambia wananchi wa Kinondoni wafanye wanaloweza wao kwa kumpa kura Mtulia na amewapa siri kuwa mgombea huyo wakati akiwa mbunge wa upinzani alikuwa anafanya kazi kwenye mazingira magumu.

"Ameamua kuja CCM ili kuhakikisha anatawatumikia wananchi, Mtulia amefanya hivyo kwa kutambua kuwa juhudi zinazofanywa na Rais ,Dk.John Magufuli katika kuwatumikia watanzania, kwa mtu mwenye akili timamu lazima aunge mkono jitihada hizo.

"Rais Magufuli ana nia nzuri na wananchi na kwa Mtulia kwa kutambua hilo ameona ni vema aungane na Rais pamoja na CCM ili kuleta maendeleo ya wananchi.Mchagueni Mtulia muone mambo mazuri yatakavyokwenda.

"Mipango ya kuendeleza Jiji la Dar es Salaam inayofanywa na Rais , Mtulia ameona ni vema akaunga na jitihada hizo za Serikali kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Kinondoni. Mtulia anao moyo wa dhati wa kuwatumikia wananchi wa Kinondoni,"amesema.


NAIBU SPIKA AUNGURUMA

Wakati huohuo, Naibu Spika wa Bunge ,Dk.Tulia Ackson amesema wabunge wa CCM wamejitokeza kwa wingi kwenye kampeni hizo kumuombea kura Mtulia na kwa kutumia wingi huo akiwa mbunge watampa ushirikiano mkubwa.

Amewaambia wananchi wa Kata ya Ndugumbi kuwa viongozi wa ngazi mbalimbali na wenye kutoa maamuzi Serikali wote wapo CCM na kwamba Mtulia akiwa mbunge watakuwa naye karibu naye.

"CCM ndio Chama kinachozungumzia maendeleo ya wananchi na ndio chama pekee chenye Ilani inayozungumzia maendeleo na kwa mazingira hayo Mtulia akiwa mbunge atapa msaada wa kila aina kuhakikisha wananchi wa Kinondoni wanakuwa na maemdeleo.

"Kata ya Ndugumbi diwani wake ni wa CCM, hivyo Mtulia akiwa mbunge itakuwa rahisi kwenye kuwasiliana na kutatua changamoto za wananchi.Mtulia atakuwa na uwezo wa kupiga simu kwa Waziri Mkuu muda wowote kwa ajili ya kuelezea changamoto za wananchi.Hivyo niwaombe wananchi Jumamosi ya wiki hii mjitokeze kwa wingi kumpigia kura,"amesema Dk.Mtulia.

Amesema kinachofanyika sasa ni usajili wa dirasha dogo na usajili huo mchezaji ambaye anasajili huwa ni hatari na kutumia nafasi hiyo kuelezea uwezo wa Mtulia kwenye kuwatumikia wananchi

Amesema kuwa upinzani umekosa ajenda na ndio maana kila wanapokwenda kwa wananchi wanadai Mtulia ni msaliti ambapo amehoji amemsaliti nani."Mtulia hataki kufanya makosa na ndio maana ameamua kuja CCM  ambako naamini atashirikiana na Serikali kufanya maendeleo.Kule

upinzani kila ambacho atalifaka kufanya kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wenzake wanamwambia usifanye maana CCM watashinda kwenye uchaguzi mkuu ujao.

"Hivyo Mtulia ameona umuhimu wa kushughukulikia matatizo ya wananchi na ndio maana ametafuta sehemu sahihi ambayo anaweza kufanya yale ambayo anaamini yatakwenda iwapo atakuwa mbunge wa CCM,"amesema Mapunda.

No comments: