Monday, February 5, 2018

MAHAKAMA YAMUACHIA HURU ALIYEPEPERUSHA BENDERA YA TANZANIA BILA KIBALI

Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii

MAHAKAMA  ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachiwa huru mfanyabiashara Abdullah Hauga (73) aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi wa kupeperusha bendera ya Tanzania bila kibali.

Hatua hiyo imekuja baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka(DPP) Nolle Prosequi kuwasilisha chini ya kifungu cha sheria namba 91(1) cha mwenenendo wa makosa ya jinai kuwa hana nia ya kuendelea na mashtaka dhidi ya Hauga.

Kabla ya kuachiwa, Mahakama ilitupilia mbali hati ya kuzuia ya dhamana ya DPP na  kisha kutoa masharti ya dhamana kwa washtakiwa.Mbali ya Hauga mshtakiwa mwingine ni Mkurugenzi wa Meli ya Lucky Shipping, Issa Haji (39).

Mapema, Wakili wa Serikali, Salim Msemo alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Victoria Nongwa kwamba shauri hilo limeitishwa kwa ajili ya uamuzi kuhusu DPP kuzuia dhamana kwa washtakiwa.Katika uamuzi wake, Hakimu Nongwa amesema alisikiliza hoja za pande zote mbili na pia amesoma uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ambayo imemuondolea DPP mamlaka ya kuzuia dhamana.

Hakimu Nongwa amesema Mahakama ya Rufaa ndio ya juu nchini, hivyo maamuzi yake lazima yaheshimiwe kwani kuzuia dhamana kwa washtakiwa ni kuwanyima haki.Amesema kibali cha DPP kimewasilishwa wakati Mahakama ya Rufaa nayo imetoa uamuzi kuhusu suala hilo.

Kitendo cha kuweka certificate ya kumnyima mshtakiwa dhamana kwa kesi ambayo inadhaminika ni kukiuka katiba, kinamyima mshtakiwa haki ya kuwa wanasikilizwa kwenye masuala ya dhamana."Mahakama imeangalia kosa hilo la kupeperusha bendera na uamuzi wa Mahakama ya Rufani, pia imeangalia umri wa washtakiwa na kujiuliza kwa makosa waliyofanya na huku hamna kiasi chochote kilochowekwa, na  DPP amezuia dhamana bila kueleza sababu,".

Kutokana na hatua hiyo, Hakimu Nongwa amesema anatupilia mbali kibali cha DPP kuzuia dhamana kwa washtakiwa na anawapa masharti ya dhamana.Katika masharti hayo ya dhamana, Washtakiwa wametakiwa kusaini bondi ya Sh.milioni 10 kila mmoja na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya sh. Milioni 10 kila mmoja.

Aidha washtakiwa wametakiwa wasitoke nje ya nchi bila kibali cha Mahakama.Hata hivyo, baada ya kueleza hayo, Wakili Msemo alieleza Mahakama kwamba DPP hana nia ya kuendelea na mashtaka dhidi ya mshtakiwa wa pili ambaye ni Hauga."DPP anaondoa mashtaka hayo kupitia kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai,"Kutokana na hatua hiyo, Hakimu Nongwa alimuachia huru Hauga, huku mshtakiwa wa kwanza akichiwa kwa dhamana. Kesi imeahirishwa hadi Februari 18, mwaka huu.

Washtakiwa wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 2 ya mwaka 2018 ambapo wametenda makosa mawili.Inadaiwa walijihusisha na mtandao wa kiuhalifu ambapo walilitenda kati ya July 19 mwaka ,2017 na Januari 1 mwaka 2018 maeneo ya Dar es Salaam.Inadaiwa katika tarehe hizo walishauri, walitoa msaada na maelekezo ya kutenda kosa la jinai ambalo ni kupeperusha bendera ya Tanzania katika meli ya HUIHANG 68 ambayo awali iliitwa GREKO-02 bila kibali.

Pia kosa jingine la kupeperusha bendera ya Tanzania bila kibali, ambapo inadaiwa walilitenda kati ya Julai 19, mwaka 2017 na Januari 1,mwaka 2018.Wankyo alidai  washtakiwa walipeperusha bendera ya Tanzania katika Meli ya HUIHANG 68 ambayo awali ilijulikana kama GREKO-02.

No comments: