Sunday, February 11, 2018

AZAM FC WATUA BUKOBA, TAYARI KWA MCHEZO WAO NA KAGERA SUGAR KESHO JUMATATU.

Na Faustine Ruta, Bukoba.


KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, imetua Mjini Bukoba asubuhi hii ikitokea Jijini Dar es salaam. Tayari kwa mchezo wao na Wenyeji wao Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba kesho jumatatu. Azam FC katika mchezo uliopita ilifungwa na Simba bao 1-0. Msimu uliopita Kagera Sugar ilifungwa na Azam Fc bao 3-2 kwenye Uwanja wa Kaitaba na msimu huo huo Kagera Sugar waliwafunga bao 1-0 Azam Fc na kuumaliza msimu huo wakiwa nafasi ya tatu.  

Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) msimu wa 2013/2014, wataendelea kuikosa huduma ya Nahodha Himid Mao ‘Ninja, aliyepewa mapumziko maalum kufuatia majeraha ya goti la mguu wa kulia yanayomsumbua, pamoja na mshambuliaji Wazir Junior na beki Daniel Amoah, ambao nao ni majeruhi.

 Aidha itamkosa nahodha wake msaidizi, Agrey Moris, aliyekusanya kadi tatu za njano, zinazomfanya kukosa mechi moja ijayo, lakini wachezaji wengine wote waliobakia wapo fiti kwa ajili ya mchezo huo, ukiondoa majeruhi wa muda mrefu Joseph Kimwaga, ambaye anaendelea na programu ya mwisho (recovery) ya kurejea dimbani kwenye ushindani. 

Mpaka sasa Azam FC imejikusanyia jumla ya pointi 33 kwenye nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi ikiwa sawa na Singida United iliyonafasi ya nne, ikizidiwa pointi nane na Simba iliyojikusanyia pointi 41 kileleni huku Yanga ikiwa nafasi ya pili kwa pointi zake 34.

Walipowasili asubuhi hii kwenye Uwanja wa Ndege mjini Bukoba, Picha na Faustine Ruta, Bukoba.
Kocha wa Azam Fc Idd Nassor Cheche akiteta jambo na mwandishi wa habari(hayupo pichani) mara baada ya kutua kwenye Uwanja wa Kaitaba. Kocha huyo  amesema kilichowaleta ni pointi tatu hakuna kingine huku akiwamiminia sifa wenyeji wao kuwa ni timu nzuri na kwa sasa ipo kwenye sehemu mbaya hivyo mechi hiyo itakuwa  ngumu lakini watafanya jitihada na hatimae wazoe pointi zote tatu.
Mshambuliaji wa Timu ya Azam Fc Mbaraka Yusuph nae ameambatana na kikosi hicho. Mbaraka Yusuph alikuwa mchezaji wa zamani wa Timu ya Kagera Sugar.
Wachezaji wa Azam Fc wakiteta Jambo na Kocha wao Idd Nassor Cheche mara baada ya kutua kwenye Uwanja wa Ndege mjini Bukoba.

No comments: