Friday, January 19, 2018

KIWANDA CHA DANGOTE CHAAGIZWA KUWALIPA KWA WAKATI WACHIMBAJI WA JASI

Kampuni ya Saruji ya Dangote imetakiwa kuwalipa kwa wakati Wachimbaji wa Madini ya Jasi ili kuwawezesha kulipa kodi zao kwa Serikali kulingana na taratibu zilizopo.

Hayo yamesemwa tarehe 19/01/2018 na Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko alipotembelea kiwandani hapo wakati wa ziara yake ya kutembelea Mikoa ya Lindi na Mtwara.Naibu Waziri amesema kuwa, lazima Wachimbaji Wadogo wapate malipo yao kwa wakati baada ya kuuza madini ili kuwawezesha kulipa kodi za Serikali pamoja na kurejesha mikopo yao kwa wakati katika Benki walizokopa.

Pia, Naibu Waziri Biteko ameutaka uongozi wa kiwanda hicho kuandaa rasimu ya Mkataba ndani ya kipindi cha wiki mbili na kueleza kuwa, kuwepo kwa mkataba huo ambao kutawawezesha Wachimbaji wadogo wa madini ya Jasi kutatua changamoto zilizopo baina yao na Kiwanda husika.

“Andaeni rasimu ya mkataba ili kila moja auze madini yake kwa bei inayoeleweka bila kuoneana na kila moja apate faida anayostahili,” amesema Biteko.Ameongeza kuwa zipo changamoto za Wachimbaji wadogo kutokuwa na umoja na hivyo kuwataka kuwa na umoja ili waweze kufanikiwa katika shughuli zao ikiwemo kuwepo na bei moja ya madini yao.

Aidha, Naibu Waziri Biteko amewataka wananchi na Wachimbaji wadogo kuacha tabia ya wizi ambayo imelalamikiwa na uongozi wa Kiwanda hicho. Kwa upande wake, Mkurugezi Mtendaji wa Mitambo ya uzalishaji wa katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote, Hemendra Raithatha amesema kuwa kulikuwepo na tatizo la malipo isipokuwa hivi sasa tatizo limeshughulikiwa, na kuahidi kuwa wachimbaji wa madini watalipwa kwa wakati.

Pia, Raithatha ameongeza kuwa, kiwanda hicho kipo tayari kufanya kazi na Wachimbaji wa Jasi kwa kuwa mali ghafi nyingi za kutengeneza Saruji zinatoka kwa wachimbaji hao jambo ambalo linaimarisha mahusiano kati ya pande husika.Aidha, ameishukuru Serikali kwa Mahusiano mazuri kati yake na Kiwanda hicho na pia amemshukuru Naibu Waziri kwa kutembelea kiwanda hicho. 

Mbali na Naibu Waziri, ziara hiyo imehudhuriwa pia na Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kusini, Mayigi Makolobela, Watumishi wa Wizara ya Madini, Uongozi wa Halmashauri ya Mtwara, Uongozi wa Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Jasi na Kamati ya Ulinzi na Usalama.

Naibu Waziri amefanya ziara yake ya siku tatu katika Mikoa ya Lindi na Mtwara ambayo ililenga kukutana na wadau wa sekta hiyo na kukagua shughuli zinazofanyika ikiwemo kufahamu changamoto wanazokabiliana nazo.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kushoto) akisaini kitabu cha wageni katika ukumbi wa Kiwanda cha Saruji cha Dangote wakati alipofanya ziara yake kiwandani hao. Wa kwanza kushoto ni Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kusini, Mayigi Makolobela. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mtwara Vijijini, na wa pili kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mitambo ya Uzalishaji Kiwanda cha Saruji cha Dangote, Hemendra Raithatha.
Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kusini, Mayigi Makolobela akimweleza Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa nne kulia) katika eneo la uzalishaji la Block 1 la Kiwanda cha Saruji cha Dangote. Wengine katika picha ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mitambo ya Uzalishaji, Hemendra Raithatha (mwenye suti nyeusi). Wa kwanza kulia ni Mwenyekiti wa Wachimbaji Wadogo wa Jasi, Peter Ludvick, Wafanyakazi wa Wizara ya Madini, Wafanyakazi wa Kiwanda cha Dangote na Uongozi wa Wachimbaji Wadogo.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (mbele) akiongoza kikao baina yake na Uongozi na Wafanyakazi wa Kiwanda cha Saruji cha Dangote, Wafanyakazi wa Wizara ya Madini, pamoja na Uongozi wa Wachimbaji wa Madini ya Jasi.
Eneo la uzalishaji Kitalu Na. 1 katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote.

No comments: