Sunday, December 10, 2017

SERIKALI KUFANYA MAPITIO YA MIRADI YA MAJI KUANZIA MWAKA

Naibu Waziri OR TAMISEMI Mhe. Joseph G.Kakunda akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mkoa wa Arusha, wilaya ya Longido, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Haki kazi Catalyst wa mjini Arusha
Naibu Waziri OR TAMISEMI Mhe. Joseph G.Kakunda akitoa maelekezo kwa watendaji wa maji katika mradi wa maji wilayani Longido
Naibu Waziri OR TAMISEMI Mhe. Joseph G.Kakunda akikagua mradi wa maji wilayani Longido
Naibu Waziri OR TAMISEMI Mhe. Joseph G.Kakunda akipanda kwenye tanki la maji linalojengwa katika mradi wa maji wilayani Longido
Naibu Waziri OR TAMISEMI Mhe. Joseph G.Kakunda akipiga picha na akina mama na watoto wakati waziara yake ya kukagua mradi wa maji wilayani Longido.


Serikali imewaagiza Wahandisi wa maji kuhakikisha wanasimamia miradi ya sekta ya maji nchini inayozingatia thamani ya shilingi na yenye kuleta tija kwa Watanzania.

Akiongea katika ziara yake mkoani Arusha katika wilaya ya Longido Mhe. Joseph George Kakunda, Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, amesema kumekuwepo na ufujaji wa fedha za katika Miradi ya maji nchini na mara nyingi imekuwa sio endelevu na yenye kuleta hasara kubwa kwa Taifa.

“Wahandisi hakikisheni mnasimamia utekelezaji wa miradi ya maji kwa thamani ya shilingi, wale wote wanaojenga miradi hiyo muwasimamie vizuri, fedha tunazozikopa hakikisheni mnazitumia vizuri, acheni kupokea rushwa, nataka kuona Wahandisi wanajenga mradi kwa maslai ya watu wa Longido ili kuondoa kero za maji, zingatieni taratibu, kanuni na sheria ili tupate tunachostahili” 

Mhe. Kakunda amewataka Watendaji na Wahandisi kufanya mapitio ya miradi ya maji nchini ili kuona miradi iliyotekelezwa kwa halali na pia ili iliyotekelezwa kwa wizi ionekane. “haiwezekani tangu tuanzishe Programu ya Maji Vijijini tumekwisha tumia zaidi ya shilingi trilioni 1.6lakini bado kila sehemu kuna shida ya majikwa nini kila mradi una maisha yake kama miaka 10, 15, 20, 25 hili haliwezekani, hatuwezi kwenda namna hiyo, mimi nitapendekekeza tufanya mapitio ya miradi yote ya maji iliyojengwa hasa kuanzia mwaka 2008. Kwanini watu wa kawaida wanajenga mradi mkubwa kutoka kwenye chanzo hadi hapa”

Akiwa kijijini Elondeka, Mhe. Kakunda amepongeza hatua zilizofikiwa za Mradi wa maji unaotekelezwa na Mradi wa Tabia nchi (DCFP)ambao umegharimu kidogo cha fedha shilingi milioni 36 na kushauri wananchi kuulinda siku zote. Pia alikagua mradi wa maji unaotekelezwa na Halmashauri ya wilaya Longido ambao bado haujakamilika.

Akisoma taarifa ya mradi mbelel ya Mheshimiwa Naibu Waziri Kakunda, Mtesigwa Missana ambaye ni Afisa Tarafa Longido amesema kuongezeka kwa kutotabilika kwa tabia ya hali ya hewa yanazidisha changamoto kama vile kubadilisha mtindo wa maisha ya wananchi.

Aidha, Mhe. Kakunda amewaasa wananchi kuulinda mradi wao waliouchagua wenyewe, “toeni ushirikiano kwa mradi huu kwa sababu mmeuchagua wenyewe, lindeni sana mradi huu ili uweze kuhudumia ninyi wenyewe na mifugo, mradi huu una faida kwenu ninyi, mifugo na wanyama wa porini”

Wananchi walibuni Mradi wa tanki la maji lenye ujazo wa mita 50,000 unaotekelezwa na Mkandarasi J.J.Gwakisa ambao upo katika hatua za mwishoni. Mradi wa huo wa maji unaopata maji toka katika bomba lililotoka kwenye chanzo naotarajiwa kuhudumia watu 4,814 kwa mujibu wa takwimu za sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Longido Mhe. Daniel Njungolo amesema wilaya ya Longido inakabiliwa na changamoto ya kuwa na watumishi wengi wanaokaimu na kufanya maamuzi yao kuwa sio ya kuridhisha na pia sekta ya afya imekumbwa na uhaba mkubwa wa watumishi na kuathiri kabisa utolewaji wa huduma ya afya wilayani humo kwani zaidi ya asilimia 15 ya watumishi wa sekta hiyo waliondolewa katika zoezi la vyeti bandia.

Mheshimiwa Kakunda anaendelea na ziara yake ya kikazi katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha kujionea hali ya utendaji na kukagua miradi ya maendeleo ikiwemo shule, miradi ya maendeleo na miradi ya tabianchi Mkoani Arusha.

No comments: