Friday, December 15, 2017

MWANASHERIA MKUU AWATAKA MAWAKILI WAPYA KUJIARI

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. George Masaju akiwa katika picha ya pamoja na Baadhi ya Mawakili wapya muda mfupi baada ya kukubaliwa na kusajiliwa. Pichani pia yupo Jaji Mkuu Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma na Majaji.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju akizungumza na Mawakili wapya waliokubaliwa na kusajiliwa ambapo katika nasaha zake kwao alisema atawashangaa sana mawakili hao kama watakuwa wazururaji mitaani wakisubiri ajira badala ya kuitumia taaluma yao kujiajiri wenyewe. Hafla ya kuwakubali na kuwasajili Mawakili hao imefanyika leo katika Viwanja vya Karimjee
Sehemu ya Mawakili wapya 296 ambao wamekubaliwa na kusajiliwa kuwa Mawakili wakimsikiliza Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wakashindwa kujizuia kushangilia pale alipowapa changamoto ya kuzitumia fursa zilizopo kujiajiri wenyewe kwa kwenda Mikoani na Wilayani badala ya kung'ang'ania kukaa Dar es Salaam.
Mhe. George Masaju, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, akibadilishana mawazo na Mkurugezi wa Mashtaka ( DPP) Bw. Biswalo Maganga muda mfupi kabla ya hafla ya kuwakubali na kuwasajili Mawakili 296 wapya katika hafla iliyofanyika leo Ijumaa katika Viwanja vya Karimjee.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. George Masaju, amewataka Mawakili wapya kuzitumia fursa nilizopo kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa. Ametoa ushauri huo leo ( Ijumaa) wakati wa hafla ya kuwakubali na kuwasajili Mawakili wapya 296. Hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya Karimjee.

“Niwashauri Mawakili wapya, anzeni kufanya kazi. Itashangaza sana, na nitawashangaa sana kama na nyie mtakaa mtaani mkisubiri kuajiriwa badala ya kutumia taaluma na ujuzi milioupata kujiajiri wenyewe” Mhe. Masaju amewataka mawakili hao wa kike na wakiume, na ambao wengi wao ni vijana wa umri wa kati ya miaka 30 na 40, kwenda mikoani na wilayani ambako amesema, kuna fursa nyingi za kujiajiri na pia kuna wateja wengi wenyeuhitaji mkubwa wa kupata huduma ya za kisheria.

“Nendeni mikoani na wilayani badala ya kung’ang’nia kukaa hapa Dar es Salaam na katika majiji na miji mingine mikubwa hapa nchini. Huko mtapata soko kubwa la wananchi wanaohitaji huduma zenu na wenye uwezo wa kulipia huduma hizo kutokana na shughuli zao mbalimbali zikiwamo za kilimo” amesisitiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa wale Mawakili ambao wataajiriwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na katika Utumishi wa Umma. Mwanasheria Mkuu amesema watatakiwa kuzingatia ipasavyo Maadili ya Msingi yanayosimamia utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Ameyataja Maadili hayo ya Msingi kuwa ni pamoja na; kuwa na uwezo na utaalamu wa kumudu majukumu ipasavyo, kudumu kuwa waadilifu, wanaozingatia maadili a kazi ya Mawakili wa Serikali na Maadili ya Utumishi wa Umma, Kuwiwa kuona haki inatendeka na kutenda haki katika utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku.

Maadili mengine ni; kuhakikisha kuwa, huduma zetu zinafikika kwa urahisi nchini kote na kuwahudumia wananchi na Serikali kwa ufanisi ipasavyo, kuendelea kujiongeza na kuwa wabunifu wakati wa utekelezaji wa majukumu ili kuzikabili changamoto kadhaa zilizopo kwa mafanikio na kudumisha uzalendo kwa kulinda maslahi ya Taifa letu na siyo maslahi binafsi.

Akisisitiza kuhusu Maadili ya Uwakili kwa Mawakili hao wapya na Mawakili wakiwamo wa Serikali na wakujitegemea. Mwanasheria Mkuu amesema, uwakili ni taaluma yenye hadhi ya juu sana duniani kote na hivyo, mtu yeyote anayechagua kujiunga na taaluma hiyo anapaswa kuwa mwelim mwaadilifu, na mwenye kuheshimu na kutunza kwa kiwango cha juu Maadili na Miiko inayoongoza na kusimamia taaluma ya uwakili.

“Mhe. Jaji Mkuu, majukumu yanayoambatana na kazi za Mawakili yanagusa na kuathiri moja kwa moja haki za wateja wao na jamii kwa ujumla. Hivyo, ubora wa huduma inayotegemewa kutoka kwa Mawakili ni ile yenye kiwango cha juu”. Akabainisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Akaongeza kuwa, majukumu ya Uwakili yanaambatana na imani kubwa ambayo mteja na jamii imeiweka kwa mawakili na kwa msingi huo, katika utekelezaji wa majukumu ya kazi za uwakili, kila wakili ahakikishe analinda na kuthamini imani ambayo mteja wake na jamii kwa ujumla imeweka kwake katika jambo analokabidhiwa kulisimamia.

Akisisitiza zaidi kuhusu maadili, Mhe. George Masaju anasema. “ kwa maneno mengine, Wakili anapashwa kuwa mwadilifu, mwaminifu na mtu asiyetiliwa shaka katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku”. Akawakumbusha na kuwashauri mawakili hao wapya na waliopo kazini kwamba, tendo moja la uvunjifu wa miiko ya taaluma na maadili athari yake ni kubwa.

Akaonya kwa kusema “Uvunjifu wowote wa maadili uwe wa makusudi au uzembe utalazimu hatua mahususi kuchukuliwa na mamlaka zinazohusika ikiwamo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambayo haitasita kuchukua hatua dhidi yao kwa mujibu wa Sheria ya Mwakili, Sura 341 na Sheria nyingine za nchi zikiwamo zile zinazohusiana na makosa ya jinai pale inapobainika kuwa vitendo vya Wakili husika vina jinai ndani yake”.

Mhe. George Masaju amewashauri Mawakili wote umuhimu wa kurejea katika misingi ambayo taaluma ya uwakili imekuwa ikiisimamia na kuhakikisha kuwa, kama Maafisa wa Mahakma wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu ipasavyo na kuisaidia Mahakama kutenda haki ipasavyo katika mashauri.

Amewataka pia Mawakili wanaojihusisha na vitendo vya utovu wa maadili na uvunjifu wa miiko ya taaluma ya uwakili na ambao hawajabainika watambue kwamba, vyombo husika vinaendelea kuchunguza na hatua stahiki zitachukuliwa ipasavyo. “Ni muhimu mjisahihishe ipasavyo ili tuweze kuendelea kulinda hadhi ya taaluma ya uwakili nchini, pamoja na imani ambayo wananchi wanayo juu ya tasnia na taaluma hii katika usimamizi wa haki”. Akasihi Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Suala la Maadili kwa Mawakili lilizungumwa pia kwa kina na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma na Makamu wa Raisi wa Chama cha Mawakili Tanganyika ( TLS) Godwin Simba Ngwilimi. Jaji Mkuu, amewaeleza Mwakili hao wapya kwamba, pamekuwapo na malalamiko mengi ya ukiukwaji wa maadili kwa Mawakili. Akasema jumla ya malalamiko 25 yalifikishwa kwenye Kamati ya Mawakili na kufanyiwa kazi ambapo Mawakili wawili wakulikuwa na hatia.

Kwa mujibu wa Jaji Mkuu,malalamiko hayo yanahusu utoaji wa siri za mteja, kukosa umakini na kushindwa kuendesha kesi, kuchukua kesi ambayo mteja hajatoa ruhusa, kuandika mikataba zaidi ya mmoja, kugushi , rushwa na kuchukua fedha za wateja wanapokuwa wameshinda mashauri yao.

Jaji mkuu pia akasema, Mahakama inaandaa utaratibu wa kutoa vitambulisho rasmi kwa Mawakili wote ili waweze kutambuliwa kirahisi wanapoingia katika Mahakama ili kuepusha vitendo vya kitapeli vikiwamo vya watu wanaojifanya Mawakili.

No comments: