Sunday, December 31, 2017

CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) MKOA WA SINGIDA CHAZINDUA KAMPENI ZA UCHAGUZI MDOGO



Baadhi ya wanachama wa CCM waliohudhuria mkutano wa uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa jimbo la Singida kaskazini wakiwa kwenye viwanja vya mkutano uliofanyika katika Kijiji cha Mtinko,singida vijijini juzi.
Baadhi ya wanachama wa CCM waliohudhuria mkutano wa uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa jimbo la Singida kaskazini wakiwa kwenye viwanja vya mkutano uliofanyika katika Kijiji cha Mtinko,singida vijijini juzi.
Naibu katibu Mkuu wa CCM Tanzania bara,Rodrick Mpogolo akizindua kampeni za uchaguzi mdogo wa CCM katika jimbo la Singida kaskazini zilizofanyika juzi katika Kijiji cha Mtinko,singida vijijini. 
Mgombea wa kiti cha ubunge wa jimbo la Singida kaskazini,Justine Monko akiwa tayari amepokea ilani ya chama kwa ajili ya kutekeleza yaliyoainishwa ndani ya ilani hiyo.(Picha zote Na Jumbe Ismailly)



Na,Jumbe Ismailly SINGIDA 

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida kimezindua kampeni zake za uchaguzi mdogo katika jimbo la Singida Kaskazini na kusisitiza juu ya kudumisha amani,utulivu na mshikamano uliopo hapa nchini.

Akizindua kampeni hizo zilizofanyika katika Kijiji cha Mtinko,Singida Vijijini,kwa niaba ya Katibu mkuu wa CCM taifa,Naibu katibu mkuu wa CCM,Tanzania bara,Rodrick Mpogolo alisema idadi kubwa ya wananchi wameendelea kukichagua chama cha mapinduzi kutokana na kuwa na mipango mizuri ya maendeleo.

Alizitaja sababu zingine kuwa ni chama chenye historian a pia kina awamu tano za uongozi na kwamba ni chama kilichokomaa na endapo kitakabidhiwa nchi au ukikabidhi madaraka,watakuwa na uhakika kwamba madaraka hayo yameshikwa na watu waliokomaa.

Kwa mujibu wa Naibu katibu mkuu huyo wakati wote CCM imekuwa ikishughulikia kero za watu na kwa hivi sasa inayo matumaini makubwa ya kubadilisha maendeleo ya nchi na kwamba hivi sasa rais wan chi amekwisha hamisha makao makuu ya serikali yake Mkoani Dodoma,jirani kabisa na Mkoa wa Singida.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Singida,Dk.Rehema Nchimbi pamoja na kuwashawishi wananchi wa jimbo la Singida kaskazini kumchagua mgombe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) lakini hakusita pia kutaja utekelezaji unaofanya na serikali ya chama hicho kwa hivi sasa.

Dk.Nchimbi ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa Mkoa wa Singida aliweka bayana kwamba mradi wa usambazaji umeme vijijini awamu ya pili nay a tatu umeshaanza na tayari zaidi ya shilingi bilioni 71.3 zinatarajiwa kutumika kusambaza nishati hiyo katika vijiji vyote.

“Kwa hivyo nawaombeni wananchi wa jimbo la Singida kaskazini mchagueni mgombea wa CCM kwani mkimleta mtu mwingine haijui ataanza kwanza kujifunzafunza atatuchelewesha,kwa hiyo mleteni Monko ili aendeleze utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi(CCM)”alisisitiza Dk.Nchimbi.

Akimkaribisha Naibu Katibu Mkuu wa CCM,Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida,Juma Hassani Kilimba alisema kutokana na wingi wa wananchi waliohudhuria mkutano huo wa uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo,unadhihirisha wazi kwamba wao tayari kumchagua mgombea huyo wa CCM ifikapo jan,13,mwaka ujao.

Hata hivyo Kilimba alisisitiza huku akijinasibu kwamba chama hicho hakina wasiwasi juu ya kushinda katika uchaguzi huo mdogo kutokana na serikali ya chama hicho kujishusha kwa wananchi wa ngazi za chini.Naye mgombea wa chama hicho Justine Monko kwa upande wake amewahakikishia wakazi wa jimbo hilo kwamba hataweza kuwaangusha endapo watampa ridhaa ya kuwa mbunge wao kwa kumchagua kwa kura za kutosha na za kishindo na hatasita kuwatumikia kwa weledi wa hali ya juu.

“Namshukuru sana Rais wetu Dk.John Pombe Magufuli kwa kuniteua kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Liwale,kanipa nafasi hiyo nimejifunza mengi sana pamoja na namna bora ya kuwatumikia wananchi”alisisitiza Monko.

No comments: