Wednesday, November 1, 2017

SERIKALI YAWASILISHA MUSWADA WA SHERIA YA WAKALA WA MELI WA TAIFA

Naibu Waziri wa Sekta ya Uchukuzi na Mawasiliano wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Mhandisi Atashasta Nditiye (mwenye koti) akifuatilia majadiliano baada ya kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli wa Taifa mbele ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu kwenye kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Pius Msekwa, Bungeni mjini Dodoma. Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Prof. Norman Sigalla King (katikati) akichangia maoni yake kuhusu Muswada huo. Wa kwanza Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Selemani Kakoso.
Mjumbe wa Bodi ya Mamlaka ya Bandari Tanzania Mzee Renatus Mkinga (aliyesimama) akitoa maoni yake mbele ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu kuhusu Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli wa Taifa kwenye kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Pius Msekwa, Bungeni mjini Dodoma. Naibu Waziri wa Sekta ya Uchukuzi na Mawasiliano wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe. Mhandisi Atashasta Nditiye (mwenye koti) akifuatilia majadiliano hayo na wa kwanza kulia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Prof. Norman Sigalla King.
Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu Mhe. Rukia Kassim akichangia maoni yake kuhusu Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli wa Taifa mbele ya Kamati hiyo na wadau wa sekta ndogo ya usafiri wa majini kwenye kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Pius Msekwa, Bungeni mjini Dodoma.


……………..


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imewasilisha Muswada wa Sheria ya Wakala wa Meli Tanzania mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kwenye kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Pius Msekwa, Bungeni mjini Dodoma.

Muswada huo umewasilishwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Nditiye kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Prof. Makame Mbarawa. Wakati akiwasilisha Muswada huo, Mhandisi Nditiye alisema kuwa Muswada huu unapendekeza kutungwa kwa Sheria itakayoanzisha Shirika la Uwakala wa Meli ambalo pamoja na majukumu mengine litakuwa na jukumu la kutoa huduma ya uwakala wa meli na kudhibiti huduma za usafiri na usalama wa vyombo vya majini.

Ameongeza kuwa, Muswada huu utaweka mfumo madhubuti wa uendeshaji wa biashara ya uwakala wa meli na udhibiti wa huduma za usalama wa usafiri wa meli hivyo utaimarisha udhibiti wa sekta ndogo ya usafiri wa meli na kuifanya sekta hii kuchangia vyema katika uchumi na kuongeza pato la Taifa. Muswada huu ni moja ya jitihada za Serikali za kuhakikisha kuwa taasisi zake zinajiendesha kwa faida, kibiashara, kwa ushindani na kutoa gawio kwa Serikali ili iweze kuhudumia wananchi kwa kujenga miundombinu ya kisasa na kuwapatia wananchi huduma mbali mbali za kijamii.

Mhandishi Nditiye aliyataja majukumu ya Shirika kuwa ni pamoja na uhakiki wa shehena inayoingia na kutoka kupitia bandari za Tanzania, uondoshaji shehena za madini, makinikia, wanyama hai, nyara za Serikali, na bidhaa zinazotokana na madini na udhibiti wa watoa huduma katika sekta ndogo ya usafiri majini, usalama wa meli na mazingira ya bahari. 

Muswada huu utaipa mamlaka Shirika ya kutekeleza Sheria ya Bahari ya Mwaka 2003, kufanya ukaguzi wa meli za kigeni na udhibiti wa meli zilizosajiliwa Tanzania, udhibiti wa vivuko vya kibiashara, kuratibu shughuli za utafutaji na uokoaji, kudhibiti, kuratibu na kulinda mazingira ya bahari, kuainisha utaratibu wa kutoa na kuhuisha leseni na udhibiti wa ada na tozo. Pia, Muswada huu unaainisha taratibu na sifa za kampuni binafsi inayostahili kupewa leseni ya uwakala wa meli.


Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu Mhe. Prof. Norman Sigalla King aliwakaribisha wadau wa sekta hii ndogo ya usafiri wa meli ili waweze kutoa maoni yao kuhusu Muswada huo. Rais wa Chama cha Uondoshaji na Usafirishaji wa Shehena Tanzania (Tanzania Freight Forwarders Association) Bwana Stephen J. Ngatunga kwa niaba ya Umoja huo alisema kuwa wanaiomba Serikali kutenganisha majukumu ya Shirika linalotaka kuanzishwa kupitia Muswada huu kwa kulipa majukumu ya kufanya biashara na kuwa mdhibiti wa sekta ili kuepusha mgongano wa kimaslahi. 

Amefafanua kuwa ni vema kwa Serikali kuanzisha Shirika na kuwa na chombo kingine cha kudhibiti sekta hii. Wadau wengine waliotoa maoni yao kuhusu Muswada huu ni pamoja na Chama cha Wanasheria wa Usafirishaji Majini (Maritime Law Association), Baraza la Watumiaji wa Huduma za SUMATRA (SUMATRA-CCC), Mawakala wa Wamiliki wa Meli Tanzania (Tanzania Shipping Agency Association), Taasisi ya Sekta Binafsi (Tanzania Private Sector Foundation), Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Chama cha Wadau wa Usafirishaji Majini Tanzania (Maritime Association of Tanzania).

Aidha, Mhandishi Nditiye amewatoa hofu wadau wa sekta hii na kusema kuwa Serikali imepokea maoni yao na imewataka wadau wafahamu kuwa Serikali haina nia mbaya na wao, inataka kuwe na maslahi mapana na katika miaka iliyopita Serikali imepoteza mapato yake katika Sekta hiii. Dhamira ya Serikali ni kuwa na Shirika litakalodhibiti na kusimamia sekta hii kwa kuwa Serikali inafahamu kuwa wadau wametoa ajira kwa watanzania hivyo Shirika litafanya kazi kwa uwazi kabisa. 

Alisema kuwa Muswada huu utaainisha utaratibu wa kuhamisha watumishi kutoka Idara zinazosimamia usafiri wa majini kutoka Mamlaka ya Udhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) na kuwapeleka kwenye Shirika litakaloanzishwa kupitia mapendekezo ya Muswada huu.

Kikao baina ya Serikali na Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu kuhusu Muswada huo kitaendelea kesho ambapo Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano itahitimisha hoja yake kwa kujibu maoni ya Kamati na wadau kuhusu Muswada husika.


Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

No comments: