Thursday, September 21, 2017

WANAOPISHA MRADI MKUBWA WA UCHIMBAJI MADINI YA ‘KINYWE’ KIJIJI CHA EPANKO KUFAIDIKA KWA KUJENGEWA NYUMBA ZA KISASA ENEO MBADALA


Na John Nditi, Ulanga.
KAMPUNI ya TanzGraphite imesema itawajengea nyumba zenye hadhi ya juu kaya za  kijiji cha Epanko, wilayani Ulanga , mkoani Morogoro  zinazohama kwa kupisha mradi mkubwa wa uchimbaji wa madini ya Kinywe (Graphite) na itahakikisha kuwa,  maisha ya watu wanaohama yanabaki kama ilivyokuwa awali ikiwa na  kuboreshwa zaidi.

Meneja Mahusiano wa TanzGraphite, Bernard Mihayo , alisema hayo kwenye taarifa ya Kampuni hiyo  katika  kikao cha tisa cha kikosi kazi kilichokutana  Septemba 14, mwaka huu  mjini Mahenge , wilayani humo.

Kikao hicho kilichokuwa ni cha kujadili na kupokea mrejesho wa vikao vya wananchi kuhusu mpango wa uhamishaji makazi (RAP) kupisha mradi wa madini ya kinywe wa Epanko kilihudhuriwa na  wajumbe  wa vitongoji vya  Kazimoto, Epanko A, Itatira , Mbera, Epanko B na Luli .

 Wawakilishi wengine ni kutoka   ofisi ya mkuu wa mkoa wa Morogoro, Ofisi ya madini mkoa , Ofisi ya  wilaya ya Ulanga , halmashauri na wadau wengine wa mradi huo.

Madini ya Graphite ‘Kinywe’ kwa sasa yanahitajika kwa wingi duniani kutokana na matumizi ya  kutengeneza vitu mbalimbali ikiwemo betri za simu , kompyuta mpakato ‘laptop’  na penseli .

Kwa mujibu wa Meneja Mahusiano wa TanzGraphite , utafiti uliofanywa na  Kampuni  hiyo umebaini madini hayo yanapatikana kwa wingi  na kwa ubora zaidi eneo la Kijiji cha Epanko, wilayani Ulanga, mkoa wa Morogoro.

Alisema ,ndani ya eneo linalohitajika kuendesha mradi , lina kaya zipatazo 320 ambazo nyumba zake zimejengwa zaidi kwenye mabonde ambayo pia yanatumika kwa shughuli za kilimo.

Meneja Mahusiano wa TanzGraphite alisema , kaya nyingine zipatazo 80  zinaishi nje ya eneo la mradi , isipokuwa  zinamiliki ardhi na mashamba ndani ya eneo la mradi huo.

Pamoja na hayo alisema, ndani ya eneo la mradi kuna miundombinu ya kijamii kama shule ya msingi, ambayo ndiyo shule pekee iliyopo katika kijiji cha Epanko , Kanisa Katoliki,  na jengo la zahanati ya kijiji ambayo bado haijakamilika.

Naye Mwakilishi wa Afisa Madini Mkazi wa mkoa wa Morogoro, Athuman Kwariko alisema , serikali ipo tayari kusimamia sekta ya madini na inajipanga kuanzisha  Kamisheni ya Madini.

Alisema , madini ni mali ya wananchi na yanakasimiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa manufaa ya watu wote  na  kwa hiyo Serikali  inasisitiza uwekezaji  na  kusimamia sekta ya madini na wananchi kuwa tayari kuwapokea wawekezaji kwa manufaa yao na taifa kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Kamati ya kikao  kazi hicho , Valence Kidumu alisema, pamoja na mipango  mizuri iliyowasilishwa na Kampuni katika  kikao hicho  aliishauri Kampuni  iwasilishe  taarifa hiyo kwenye  kikao cha Baraza la Madiwani kinachotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

“ Taarifa hii tuliyoipokea leo hapa ni nzuri na unaungwa mkono na wajumbe wote , lakini ni vyema Kampuni ikatoe pia  kwa Madiwani kwenye  kikao cha baraza kinachotarajia kufanyika  Oktoba  mwaka huu kwa kupata baraka zao” alisema  Kidumu ambaye pia ni Ofisa Ardhi wa wilaya hiyo.

Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi Miundombinu Ofisi ya Mkuu wa mkoa  wa Morogoro, Lucas Mwaisaka , aliwataka viongozi wa serikali ya Kijiji Epanko kuitisha kikao  halali utakachoridhia kupitishwa kwa mpango wa uhamishaji wa makazi  ili utekelezaji  uweze  kuanza  na Kampuni hiyo.

Awali  mkuu wa wilaya ya Ulanga, Jacob Kassema alisema, juhudi  kubwa zimefanyika kutoa  elimu ya ushirikishwaji wananchi kuhusu miradi mbalimbali ukiwemo wa Epanko ambapo  asilimia 82 ya kaya za zimekubali kuthaminiwa kupisha mradi uchimbaji wa madini ya Kinywe.
 Kiongozi wa wa kimila wa kabila la Wapogoro wa kijiji cha Epanko , wilaya ya Ulanga, mkoani Morogoro  (Mbuyi ), Redemta Masura ( wapili kushoto) akiwa na viongozi  wa Kijiji hicho wakipitia  taarifa  ya mpango wa uhamishaji makazi kupisha mradi wa madini ya Kinywe wa Epanko , wakati wa kikao cha tisa cha Kikosi Kazi iliyowashirikiasha wajumbe wa kutoka vitongozi sita wa kijiji hicho , viongozi kiserikali na kijamii kilichofanyika hivi karibuni mjini Mahenge.
 Baadhi ya viongozi wa serikali wa wilaya ya Ulanga na mkoa wa Morogoro wakiungana na vitongoji vya kijiji cha Epanko wakiwemo na wakimila na kijamii  kupitia   taarifa  ya mpango wa uhamishaji makazi kupisha mradi wa madini ya Kinywe wa Epanko katika kikao cha tisa cha Kikosi Kazi cha mpango wa uhamishaji makazi  kupisha mradi wa madini ya Kinywe wa Epanko kilichofanyika hivi karibuni mjini Mahenge.
 Baadhi ya viongozi wa kamati ya Kikosi kazi  kutoka serikali  za vitongoji vya kijiji cha Epanko wakiwemo wa kimila na kijamii  wilayani  Ulanga  wakijumuika na wa ngazi ya wilaya hiyo na mkoa wa Morogoro kupitia   kwa pamoja taarifa  ya mpango wa uhamishaji makazi kupisha mradi wa madini ya Kinywe wa Epanko  kilichofanyika hivi karibuni mjini Mahenge.
Katibu Tawala Msaidizi Miundombinu Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Lucas Mwaisaka (kulia) akimkabidhi  Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Epanko, Kata ya Nawenge, wilayani Uanga, Eliza Liwemba, ( kushoto) Mpango wa Uhamishaji Makazi (RAP) wa Mradi wa Madini wa Epanko  wakati wa kikao cha tisa cha Kikosi Kazi cha mpango huo kilichowashirikisha wajumbe wa kutoka vitongozi sita wa kijiji hicho , viongozi kiserikali  ya wilaya  na  mkoa ambacho kilifanyika hivi  karibuni mjini Mahenge. ( Picha na John Nditi).

No comments: