Thursday, September 21, 2017

TaSUBa KUFANYA TAMASHA LA 36 LA KIMATAIFA BAGAMOYO

Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBA) (wa pili kushoto) akiongea na Waandishi wa habari kuhusu kufanyika kwa Tamasha la Kimataifa la 36 linalohusu Sanaa na Utamaduni Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) 21 Septemba, 2017 Jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Tamasha la Sanaa na Utamaduni toka Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBA) (kushoto) akitolea ufafanuzi kwa Waandishi wa habari kuhusu kufanyika kwa Tamasha la Kimataifa la 36 linalohusu Sanaa na Utamaduni Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) 21 Septemba, 2017 Jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Waandishi wa habari wakichukua taarifa wakati wa Mkutano wa Waandishi wa habari uliohusu kufanyika kwa Tamasha la Kimataifa la 36 linalohusu Sanaa na Utamaduni Wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO) 21 Septemba, 2017 Jijini Dar es Salaam.PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA-WHUSM


………………………………..


Na. Neema Mathias- MAELEZO


21,Septemba,2017.


Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) imeandaa tamasha la 36 la Kimataifa kuanzia tarehe, 23 hadi 30, Septemba litakalofanyika katika viwanja vya taasisi hiyo mjini Bagamoyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Dkt.Hebert Makoye alisema kuwa tamasha hiyo litakuwa na kauli mbiu isemayo ‘sanaa na utamaduni katika kupiga vita madawa ya kulevya’.

“Kauli mbiu hii ni mahsusi katika kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli za kupiga vita matumizi na usambazaji wa dawa za kulevya nchini” alisema Dkt. Makoye.

Aliongeza kuwa wakati wa tamasha elimu ya kudhibiti matumizi ya dawa za kulevya itatolewa ikiwalenga hasa vijana ambao ndio waathirika wakuu wa dawa hizo ambapo kutakuwa na midahalo na makongamano kuhusu athari za matumizi ya dawa hizo.

Aidha alisema kuwa midahalo na makongamano hayo yatawahusisha vijana ambao watatoa ushuhuda juu ya matumizi ya dawa za kulevya,wamiliki wa vituo vya dawa za kulevya na wanasheria ambao watatoa mada mbalimbali kuhusu suala la dawa za kulevya kwa ujumla.

“Takwimu zinaonesha kuwa, idadi kubwa ya waathirika wa madawa ya kulevya ni vijana, kwa kuwa asilimia kubwa ya nguvu kazi katika tasnia yetu ni vijana tamasha letu mwaka huu limeamua kulenga kutoa elimu kuhusu ubaya wa matumizi ya dawa hizo kwani kupitia sanaa tutaweza kuwafikia vijana kwa kiwango kikubwa zaidi,” alieleza Dkt. Makoye.

Alifafanua kuwa, malengo ya tamasha hilo yamekuwa yakiboreshwa kwa kujikita katika mada mbalimbali ambapo lengo kubwa ni kutunza na kuenzi sanaa na utamaduni wa mtanzania, mwafrika na dunia nzima, pia tunalenga kutengeneza jukwaa ambalo wanafunzi wa TaSUBa watalitumia kupima kiwango chao cha umahiri katika sanaa kwa mwaka katika fani za sanaa za maonyesho na ufundi.

Malengo mengine ni kukutanisha watu wa tamaduni tofauti kutoka sehemu mbalimbali duniani ili kuonyesha utajiri wao wa sanaa na utamaduni pamoja na kutengeneza jukwaaa ambalo ni kiungo cha kujenga mahusiano ya wasanii wa ndani na nje ya nchi kupitia maonyesho ya sanaa kwa lengo la kubadilishana mawazo katika kuendeleza tasnia hiyo.

Vilevile amesema kuwa, mwaka huu wameamua kufanya maboresho katika tamasha hilo ambapo kutakuwa na maonyesho rasmi yatakayofanyika mchana kwa ajili ya watoto na vijana na kutoka katika shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo. 

Kwa upande wake mwenyekiti wa tamasha hilo, John Mponda amesema watakuwa wanaanza kwa warsha ambapo wadau mbalimbali watatoa elimu kuhusu masuala ya jamii kujitambua , kujenga uzalendo na kujitoa katika utumwa wa matumizi ya dawa za kulevya.


Aidha, Mponda ameeleza kuwa katika maonyesho hayo vijana wajasiriamali waliojiajiri watapata muda wa kutangaza biashara zao mbalimbali ikiwemo sanaa, vyakula lishe, vyakula dawa pamoja na kutambua mashirikisho mbalimbali ya sanaa.

Tamasha la mwaka huu litashirikisha vikundi zaidi ya 68 kutoka ndani na nje ya nchi ambapo nje ya Tanzania tutakuwa na vikundi kutoka Kenya, Ufaransa, Uingereza, Zimbabwe, Mayyote pamoja na Korea na litafunguliwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe.

Dkt. Makoye aliwashukuru wadhamini wa tamasha hilo ambao ni pamoja na  Pepsi, CRDB Bank, Azam Group, Azam Tv,TBC, EFM, E TV, Mlimani Media, Habari Cooperation ltd, TSN, Millenium Hotel, Country Club, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Ester decoration.

Taasisi ya Sanaa Bagamoyo TaSUBa ilianzishwa mwaka 2007 kwa malengo ya kutunza na kuenzi utamaduni wa Mtanzania, kuendesha tafiti na shughuli mbalimbali za sanaa na tamaduni na kukuza bidhaa za sanaa.

No comments: